“WAWATA HIMIZENI MIITO”



WITO  umetolewa kwa   wanawake  wakatoliki nchini  kuhimiza miito mitakatifu  kuanzia ngazi za familia, jumuiya ndogo ndogo,vigango, parokia hadi  majimboni ili Kanisa liweze kupata hazina kubwa ya mapadri na masista watakaolitumikia kimwili na kiroho pamoja na  watu wake.
Aidha imeelezwa kuwa  mapadri na masista  waliopo umri unazidi kuongezeka na hivyo Kanisa linahitaji vijana wa kike na kiume  watakaoandaliwa  katika malezi na kusomeshwa  katika  Seminari  mbalimbali ili waweze kushika majukumu ya kichungaji na kitume katika Kanisa mahalia.
Hayo yamesemwa na Katibu  wa Wanawake Wakatoliki Taifa(WAWATA) ambaye pia ni  Mwenyekiti wa WAWATA Jimbo Kuu Dar es Salaam, Bi.Desderia Mahita  wakati  wa hitimisho la Kongamano la siku  tatu la Kanda ya Nyanda za Juu Kusini  lililofanyika jimboni Mbeya na kuwashirikisha  wanawake  wa majimbo 8 ya Jimbo Kuu Katoliki Songea.
Majimbo ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini katika Jimbo Kuu Songea  yaliyoshiriki katika  Kongamano hilo  tangu Juni 23 hadi 25 ni pamoja na Jimbo Katoliki Mbeya, Lindi, Mtwara, Tunduru Masasi, Njombe, Iringa, Mbinga na Songea lenyewe ambapo zaidi ya  wanawake 1000 walishiriki.
Katibu huyo ambaye ni mlezi  wa WAWATA  Kanda  ya Nyanda za Juu  Kusini  amewaalika wanawake  wote kuwa  wanapohitimisha Kongamano hilo  wabebe jukumu  la kwenda kuhimiza miito mitakatifu katika familia zao na jumuiya ndogo ndogo.
“Akina Mama ni jukumu letu kwenda kuhimiza miito mitakatifu, chukueni hiyo  kazi na mjiulize je Jumuiya, Kigango, Parokia na Jimbo lina mapadri na masista  wangapi na mkawahimize  watoto waende seminari isiwe kwa fasheni  bali mkaguswe mioyoni mwetu na tuombe baraka za Mwenyezi  Mungu  tuishi maisha ya familia takatifu kama ya Yesu, Maria na Yosefu, tuhimizane  na tukahimizane  kufunga na kubariki  ndoa,”amesisitiza.
“Wanawake Wakatoliki tuwe  wakamilifu yaani tusiwe eti  misa ya kwanza tunasali kanisani na misa ya pili tunaenda kwenye maombi  katika madhehebu  ambako tunakatazwa kuvaa rozari  na  tunakatiwa na rozari…lakini tuwe watu wa msamaha, sisi wanandoa enzi zetu wakati tunafanyiwa mafundisho ya ndoa tulikuwa tunafundishwa  na mababa kuwa tukigombana ndani ya nyumba tuhakikishe tunapatana  kabla ya jua halijazama,” amefafanua Bi.Mahita.
Ameongeza,”Tuweke jitihada katika kuwalea mapadri wetu kwani  wamewaacha Baba, Mama na ndugu  zao wanalitumikia Kanisa,  hivyo padri  akifiwa, kuuguliwa, akihitaji msaada wowote uwe wa usafiri... wewe kama WAWATA toa  msaada haraka.”
Kwa upande wao, Katibu wa WAWATA  Jimbo Kuu Songea na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Bi.Imelda Mbawala amesema  katika Kongamano  wanajifunza na kubadilishana uzoefu, mada mbalimbali  huku wakiongozwa na kauli mbiu  MWANAMKE MKATOLIKI MWENEZAJI  WA HURUMA  YA MUNGU, ambapo wamechagua viongozi wapya  wa WAWATA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ambapo Mwenyekiti ni, Bi. Rita Materu kutoka Jimbo Katoliki Iringa, Makamu Bi. Teresia Chilumba(Lindi), Katibu Bi.Imelda Mbawala(Songea), Katibu Msaidizi, Bi.Agness Hyera(Tunduru Masasi) na Mtunza hazina  ni Bi.Rebeka Kapinga(Mbinga).
Naye, mlezi wa WAWATA, Sista Verena Kwimba amewaagiza masista kuwasaidia wanawake kufahamu  kuwa kufunga  siyo sala  na sadaka tu bali  pia na kusamehe yote,”tuwasaidie wanawake kama wanatoa sadaka na kusali wakati wa mfungo lakini wakitoka na manung’uniko  mfungo wao unakuwa ni bure unafutwa.”
Mwenyekiti wa WAWATA  Jimbo la Mbeya,Bi. Everada Mangwala amesema katika kongamano hilo  wamefanya matendo ya huruma ya kuwatembelea  watoto yatima  katika kituo cha Igogwe na kuwapelekea mahitaji mbalimbali ikiwemo chakula,seminari ndogo ya Mbalizi kituo cha Yatima Iyunga,walitembelea kituo cha malezi cha watawa wa kike.
Bi.Mangwala  ametoa  wito kwa wanawake kuanza  kujiwekea  akiba kidogo kidogo  ili wapate kuwatolea wahitaji  katika Kongamano la Kanda ya Kusini, mwezi Juni  mwaka 2018 linalotarajiwa kufanyika jimboni Mbinga  kwani kuhitimishwa kwa Kongamano la Mbeya ndiyo mwanzo wa maandalizi ya lile la Mbinga.
Katika ibada hiyo  viongozi wastaafu  wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini akiwemo aliyekuwa Mwenyekiti  wa WAWATA wa  awamu iliyopita ambaye pia ni Mwenyekiti  wa Jimbo Katoliki  Mtwara, Bi. Verena Mahundi na Mweka hazina Bi. Agness Ng’owo wa  Parokia ya Makambako, Jimbo Njombe kwa niaba ya  viongozi wenzao  wastaafu  wameomba  mshikamano uendelee kudumu  huku  wakifafanua zaidi kuwa  WAWATA  siyo kuvaa  sare za vitenge tu bali ni mwanamke yeyote mkatoliki mbatizwa aliyefikisha  umri wa miaka  18 kuusimamia na kuutekeleza kwa uadilifu utume wake kwa Kanisa.

















Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU