Buriani Naibu Askofu Mdai


WAKRISTO wakatoliki Jimbo Katoliki Mahenge wamepata pigo baada ya kuondokewa na Naibu Askofu wa Jimbo hilo Padri Kalistus Mdai  ambaye  pia alifanya kazi ya ukufunzi katika Seminari ya Kasita, pia Mshauri Mkuu wa Askofu wa Jimbo Katoliki Mahenge.
Kifo cha Naibu Askofu huyo kimetokea Mei 20, Jumamosi akiwa safarini kuelekea katika hospitali ya rufaa ya Mt. Francis Ifakara kwa ajili ya kupatiwa matibabu
Akizungumza kwa niaba ya Askofu wa Jimbo Katoliki Mahenge na Jimbo Katoliki Ifakara,  Naibu Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Padri Boniventura Mchalange amesema kuwa Mapadri wa majimbo hayo mawili wameupokea kwa masikitiko makubwa msiba huo kwani wamempoteza mtu muhimu hususani katika suala la usuluhishi.
“Tumeumia kwa kweli na tumepata pigo kwani msuluhishi wetu mkubwa ametutoka, nafikiri itatuchukua muda mrefu sana kuweza kumsahau,” amesema Padri Mchalange, Naibu wa Askofu Jimbo Katoliki Ifakara.
Aidha Naibu Askofu huyo amesema mapadri kwa ujumla wametoa pole kwa wote waliopokea msiba huo na wale wote waliotoa ushirikiano mpaka kufikia hatua ya kuuaga mwili pamoja na kushiriki mazishi.
Marehemu Padri Kalistus Mdai alifariki akiwa jimboni Mahenge na mwili wake ukasafirishwa mpaka jimboni Ifakara ambapo Mei 24 ilifanyika ibada ya kuuaga mwili huo katika Kanisa la Mt. Andrea ambalo ni Kanisa Kuu la Jimbo Ifakara, kabla ya kurudishwa jimboni Mahenge na kufanyiwa ibada ya kuuaga Mei 25 katika Kanisa Kuu la Jimbo.
Wasifu wa Marehemu
Padri Kalistus Mdai alizaliwa tarehe 18 Januari 1939 na alisoma katika shule ya seminari Kasita iliyopo jimboni Mahenge na alipata Daraja takatifu la upadri tarehe 15 August 1966 katika Kanisa la Kwiro ambalo ni Kanisa Kuu la Jimbo Mahenge.
Mnamo Mwaka 1967 alianza kazi ya utumishi kama Paroko Msaidizi katika Kanisa la Mt. Andrea Ifakara mpaka mwaka wa 1970 alipoteuliwa kuwa Leacture wa Kwanza Mwafrika katika Seminari ya Kasita, akiwa seminarini hapo  alipewa Cheo cha Umonsinyori (MSGR).
Mwaka 1979 Aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Mahenge Askofu  Iteka alimtoa Msgr Mdai katika Seminari ya Kasita na kumsogeza Kwiro katika Kanisa Kuu la Jimbo, ambapo alikuwa Naibu Askofu pia Mshauri Mkuu wa Askofu kwa kipindi chote.
Msgr Mdai amefariki akiwa na umri wa miaka 78, atakumbukwa na wakristo wengi kwani ni miongoni mwa wakristo wachache wanaofahamu juu ya Historia ya Jimbo Katoliki Mahenge na lile la Ifakara.
Atakumbukwa pia wakati akiwa Mkufunzi katika Seminari ya Kasita kwa kusaidia mapadri wengi kufanikisha azma yao ya kuwa mapadri.

Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema, Amina.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU