Liganga yanufaika na Mradi wa Maji Mtiririko





JUMLA ya shilingi milioni 270 zimetumika kukamilisha mradi wa maji ya mtiririko katika Kata ya Liganga mkoani Ruvuma.
Akihubiri katika Misa Takatifu wakati wa sherehe za uzinduzi wa mradi huo wa maji, Padri Dominikus Nyoni ambaye ni Paroko wa Parokia ya Liganga Jimbo Kuu Katoliki Songea amesema kuwa jamii nzima ya Kata ya Liganga haina budi kumshukuru Br. Dr Ansigar OSB kwa kufadhili mradi huo wa maji.
Amesema Br. Dr Ansigar OSB kwa muda wa miaka 30 amekuwa akifanya kazi kubwa ikiwemo ya kuiongoza hospitali ya Peramiho kama Mkurugenzi wa hospitali hiyo. Amefafanua kuwa, Br.Dr Ansigar OSB amejishughulisha kuongeza majengo ya hospitali na kuongeza idadi ya madaktari katika hospitali hiyo.
Ameongeza kuwa licha ya kazi yake ya udaktari Br.Dr Ansigar OSB amejitahidi kuwaletea wananchi wa Tarafa ya Ruvuma maendeleo ikiwemo upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama.
Aidha katika sherehe hizo za uzinduzi wa maji ya mtiririko Br.Dr Ansigar OSB ametoa baiskeli kumi na tatu {13} kwa wahudumu wa afya msingi majumbani ili ziwasaidie katika kutoa  huduma za afya katika vijiji  vya Tarafa ya Ruvuma na amegawa vyeti kwa wahudumu wapya 25 wa afya msingi majumbani.
Kwa upande wake Br. Dr Ansigar OSB amesema kuwa kwa kiasi kikubwa magonjwa mengi yamepungua kama vile magonjwa ya ngozi, malaria, kuhara, Ukimwi na kifua kikuu. Katika sherehe hizo ametoa wito kwa wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya, na ameahidi mwaka huu kuendelea kuchimba pampu nyingine nane {8} katika kata zote zilizopo katika Tarafa ya Ruvuma.
Akizungumza kwa niaba ya serikali, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Songea Bwana Venance Komba amesema serikali inatambua mchango wa Br. Dr Ansigar OSB kwa wananchi wa Tarafa ya Ruvuma. Amesema serikali itahakikisha inasimamia na kuvitunza vyanzo vyote vya maji ili huduma hiyo ya maji ya mtiririko iweze kuwa endelevu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU