ASKOFU LEBULU ASHAURI MAPADRI WAPEWE USHIRIKIANO KULIIMARISHA KANISA



ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha Mhashamu Josaphat Lebulu  amewataka waamini nchini kuonyesha umoja na mshikamano kwa mapadri ili kuleta maendeleo ya parokia na jamii kwa ujumla.

Askofu Lebulu ameyasema hayo kwenye Misa Takatifu ya uzinduzi wa parokia mpya ya Mtakatifu Yuda Thadei Ilboru Jimbo Kuu Katoliki Arusha ambayo imezaliwa kutoka Parokia ya Loruvani zamani ikiwa kigango cha Ilboru.

Katika misa hiyo mapadri wawili wamesimikwa ambao watakabidhiwa parokia hiyo mpya, padri Simon Amsi ambaye atakuwa paroko na padri Euzeb Mapua ambaye atakuwa msaidizi wa paroko, wote wametoka katika Shirika la Wanakanuni wa kawaida wa Mtakatifu Victor wa Kanuai ya Mtakatifu Augustino (CRSV) Jimbo Katoliki Mbulu ambayo makao yake makuu yapo nchini Ufaransa.

Akizindua Parokia hiyo Askofu Lebulu amesema kuwa waamini wote bila kujali umri wanapaswa kuwapa ushirikiano mzuri mapadri kwa kushauriana nao changamoto mbalimbali zinazojitokeza jambo ambalo litaleta manufaa kwa parokia na kuwepo kwa maendeleo.

“Parokia nyingi ambazo zimekuwa na maendeleo ni kutokana na mshikamano wa wakristo baina yao na mapadri bila kuwepo na chuki wala ubaguzi huku wakihitaji manufaaa ambayo yametokana na nguvu zao, lakini kama waamini hawatakuwa na upendo kwa viongozi wao, maendeleo wanatayasikilizia kwenye vyombo vya habari.” Amesema.

Aidha amewasihi waamini kuiendeleza parokia hiyo kwa kujenga miundombinu ya kutosha huku wakiwatia moyo mapadri wapya jambo ambalo litasababisha nao kuwa na vigango ambavyo vitazaliwa na parokia hiyo.

Naye Abate Mkuu wa Shirika la Wanakanuni wa kawaida wa Mtakatifu Victor wa Kanuai ya Mtakatifu Augustino (CRSV) kutoka nchini Ufaransa, Hugues Paulze d'Ivory ambaye amekuja kwa ajili ya tukio hilo amemshukuru Askofu Josaphat Lebulu kwa kuwapokea mapadri katika Jimbo lake.

Amesema Shirika hilo ambalo lilianza miaka 30 iliyopita nchini Ufaransa  litahakikisha linaonyesha mshikamano wa kutosha kwa utii na unyenyekevu huku akiwasihi wakristo kuwa na umoja ili kazi ya Mungu isonge mbele.

Kwa upande wake paroko mpya padri Simon Amsi akitoa shukrani zake, amesema kwamba atahakikisha anafanya kazi ya Mungu kadri awezavyo pamoja na msaidizi wake padri Euzeb Mapua .

Amewataka wakristo kuwapa ushirikiano wa kutosha ili kazi ya Mungu isonge mbele na kwamba wawe wakristo wa kusali.

Katika tukio hio, pia Askofu Mkuu Josaphat Lebulu amewapa wanafunzi 44 Sakramenti ya Komunyo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU