Benki ya Mkombozi kutoa gawio Julai

Benki ya Biashara ya Mkombozi inatarajia kutoa gawio kwa wanahisa wake kuanzia mwezi Julai mwaka huu.
Mwenyekiti wa Bodi ya Benki hiyo, Bw. Method Kashonda amesema wametoa ratiba ya utoaji wa gawio kama ilivyoelekezwa na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), hivyo wanatoa gawio kuanzia tarehe 6 Julai mwaka huu.
Kutokana na ratiba hiyo amesema tarehe ya kutangaza gawio ni Mei 27 mwaka huu ambayo itafuatiwa na ununuaji wa hisa pamoja na gawio kuanzia Mei 27 hadi Juni 15.
Mwenyekiti huyo ambaye alikuwa akizungumza katika mkutano mkuu wa benki hiyo ambao uliwaleta pamoja mamia ya wanahisa Jijini Dar es Salaam, amesema ununuzi wa hisa bila gawio utaanza tarehe 16 Juni mwaka huu.
“Kufungwa kwa kitabu cha orodha ya wanahisa ni Juni 20 mwaka huu na kufungua tena kitabu cha orodha ya wanahisa ni Juni 21 mwaka huu,” amefafanua Mwenyekiti huyo.
Amesema pia baada ya hatua zote hizo kukamilika, wanahisa wanatarajiwa kupokea gawio lao kuanzia Julai 6 mwaka huu.
“Gawio litalipwa moja kwa moja kwenye akaunti ya mwanahisa au kwa kupitia M-Pesa, Airtel Money au Tigopesa,” amesema Mwenyekiti na kuongeza kuwa benki hiyo imetangaza gawio la shilingi 20 kwa kila hisa.
Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo Bi. Edwina Lupembe akielezea utendaji wa benki kwa kipindi kilichoishia tarehe 31 Disemba 2016, amebainisha kuwa benki hiyo ilifanikiwa kukusanya amana za jumla ya shilingi bilioni 102.55 na kutoa mikopo na karadha ya jumla ya shilingi bilioni 73.80. Jumla ya Rasilimali za benki zilifikia shilingi bilioni 128.17 ikilinganishwa na shilingi bilioni 111.31 iliyokuwepo mwaka 2015.
“Hadi kufikia mwaka 2016, miaka minane baada ya kuanzishwa benki hiyo ilikua na matawi 6 na vituo vya kutoa huduma za kifedha viwili katika mikoa mitano ya Tanzania. Benki hii ilipata faida baada ya kodi ya shs. Bilioni 1.04 mwaka 2016,” amesema.
Benki ya Biashara ya Mkombozi ilianzishwa mwaka 2009 na Kanisa Katoliki Tanzania na taasisi zake kwa madhumuni ya kusaidia wafanyabiashara wadogo, wa kati na wakubwa kupata huduma za kifedha. 
Ili kutanua wigo zaidi, waanzilishi wa benki hiyo walitoa nafasi kwa watanzania wengine wakiwemo wafanyabiashara na wawekezaji kununua hisa zake ili kuongeza nguvu.

Benki ya Mkombozi ina matawi matano na vituo viwili vya huduma za kifedha katika mikoa ya Dar es Salaam, Bukoba, Moshi, Mwanza na Morogoro.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU