Kanisa kuadhimisha siku ya maskini duniani



BABA Mtakatifu Fransisko ametoa ujumbe wake kwa Siku ya Kwanza  ya Maskini Duniani inayoadhimishwa Jumapili ya 33 ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa Novemba 19, 2017 na kusema kuwa ‘Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli’.
Kauli mbiu ya maadhimisho ni “Tusipende kwa neno bali kwa tendo”. Baba Mtakatifu anasema, upendo wa namna hii unahitaji jibu makini, kwani umemiminwa bila madai yoyote na uko tayari kuwasha moyo kwa mwamini yoyote licha ya dhambi na mapungufu ya kibinadamu. Hili linawezekana ikiwa kama neema ya Mungu na upendo wenye huruma unapokelewa moyoni na kusaidia kuongoza utashi na vionjo vya upendo kwa Mungu na jirani!
Baba Mtakatifu anaendelea kusema, Kanisa daima limekuwa likisikiliza na kujibu kilio cha maskini na wahitaji kama inavyoshuhudiwa kwenye Kitabu cha Matendo ya Mitume, kwa kuwachagua Mashemasi saba walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho na hekima, ili waweze kutoa huduma kwa maskini, hii ni alama ya kwanza ya huduma kwa maskini kutokana na utambuzi kwamba, maisha ya Kikristo yanafumbatwa katika udugu na mshikamano.
Mwinjili Luka anatoa kipaumbele cha kwanza katika Injili yake matendo ya huruma, changamoto kwa waamini hata katika nyakati hizi kuwa ni mashuhuda wa huruma ya Mungu.  Mtume Yakobo anaonya tabia ya kuwapendelea matajiri kwa kuwavunjia heshima na kuwabeza maskini, lakini hawa ndio matajiri wa imani na warithi wa ufalme wa Mungu. Anakumbusha kwamba, imani bila matendo imekufa.
Baba Mtakatifu anakiri kwamba, kuna wakati katika historia ya Kanisa, waamini walimezwa na malimwengu, lakini Roho Mtakatifu akawasaidia kukumbatia mambo msingi, kiasi cha kuibua waamini ambao walijisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa maskini. Wakaandika historia ya Ukristo kwa unyenyekevu na kiasi; kwa ukarimu na upendo; wakawahudumia ndugu zao maskini kwa ari na moyo mkuu.
Amesema Siku ya Maskini Duniani iwe fursa ya kushikamana kwa kujenga na kudumisha utamaduni wa watu kukutana na kusaidiana, kama alama ya urafiki, umoja na udugu unaovunjilia mbali kuta za utengano kwa sababu mbali mbali. Maadhimisho haya yakamilishwe kwa namna ya pekee Kanisa linapoadhimisha Siku kuu ya Yesu Kristo Mfalme wa Ulimwengu.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU