KONGAMANO LA WAWATA LAWANUFAISHA WASIOJIWEZA



Wanawake Wakatoliki Tanzania, (WAWATA) Kanda ya Mashariki wametoa zawadi ya vitu mbalimbali kwa kituo cha  watoto yatima cha Mtakatifu Elizabeth kilichopo Parokia ya Mbingu jimboni Ifakara  vyenye thamani ya zaidi ya shilingi Laki tano ili kuwasaidia watoto hao kuzikabili changamoto mbalimbali kituoni hapo.
Msaada huo umetolewa mwishoni mwa mwezi Juni, wakati WAWATA wakihitimisha kongamano la Wanawake wakatoliki ikiwa ni sehemu ya Hija katika kituo hicho kinachomilikiwa na shirika la  masista wa upendo wa Mtakatifu Fransisko.

Msaada uliotolewa ni pamoja na; Sukari mifuko miwili, mafuta ya kula ndoo 2, sabuni ya unga mifuko 2, Sabuni za mche box 4, Magodoro madogo 20, Vitenge pande 24 na Juisi dazani 12 .
Akikabidhi msaada huo kwa niaba ya wanawake hao Mwl. Faith Peter   kutoka Jimbo Katoliki Ifakara ameupongeza uongozi wa kituo hicho kwa kazi wanayoifanya na kuongeza kuwa kimsingi hilo ni jukumu la jamii hasa akina mama.
Akipokea msaada huo  msimamizi wa kituo hicho, Sista Maria Anatolia Mgubike, amewashukuru wanawake hao kwa upendo wao, na kuonesha kujali huduma hiyo, na kuongeza  kuwa kituo hicho hadi sasa kina miaka 14 tangu kuanzishwa , na kimepokea watoto 168 mpaka sasa, ambapo kati yao 20 wamefariki.
Akizungumza na Kiongozi, Katibu wa WAWATA Jimbo Katoliki Ifakara, Mwl. Longina Mbano amesema kuwa pia  wamepeleka misaada mingine katika vituo viwili, kimoja ni Gereza la Kiberege, ambapo walipeleka vitu vyenye thamani ya shilingi 227,000/-, na kituo cha pili ni Kituo cha kulelea watoto wenye ulemavu wa akili cha Bethlehemu, kilichopo Parokia ya Kibaoni, Jimbo Katoliki Ifakara, ambacho kilipata vitu vyenye thamani ya shilingi 194,000/-
Kwa upande wake Mwenyekiti wa WAWATA Kanda ya Mashariki mama Rose Mpembe, amemshukuru Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara, Mhashamu Salutaris Libena kwa kushirikiana na kina mama hao tangu walipofika mpaka siku ya mwisho na kuongeza kuwa Kongamano hilo limefana sana huku wakipendekeza Kongamano lijalo lifanyike jimboni Zanzibar.
Baadhi ya Mada zilizowasilishwa katika Hija hiyo ni pamoja na Mwanamke mkatoliki mwenezaji wa huruma ya Mungu, iliyowasilishwa na padri Thadei Memba, katika mada hiyo kulikuwa na hoja kama; Dhana ya huruma ya Mungu, Dhana ya wanawake kutoka katika katiba ya WAWATA, Sifa za mwanamke, Matendo ya huruma, Namna ya kueneza huruma ya Mungu, na mwisho Padri Memba alitaja kumbukumbu mbalimbali za Mama Bikira Maria ambazo Kanisa linazienzi katika kumkumbuka mama Maria.
Aidha kina mama hao walipata fursa pia ya kujifunza mada ya kumkomboa mwanamke kiuchumi, mada iliyowasilishwa na padri Sirili Njau, mada aliyoigawa katika sehemu tatu, Mama ni nani? Ni mambo gani amekosa mpaka akombolewe na Namna ya kujikomboa.
Kongamano la WAWATA Kanda ya  Mashariki linajumuisha majimbo Katoliki 6, Dar es salaam, Tanga, Zanzibar, Morogoro, Mahenge na Ifakara, ambalo limefanyika Jimbo  Katoliki Ifakara. Kongamano hilo lilianza Juni 23, kwa Ibada ya Misa takatifu iliyoongozwa na Askofu wa Jimbo hilo, Mhashamu Salutaris Libena iliyofanyika katika Parokia ya Ifakara.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU