Miaka 100 ya Upadri: Maelfu Geita kushuhudia maajabu Nyamatongo






Maelfu ya wakazi wa mkoa wa Geita, wakiwemo wakristo na waamini wa dini mbalimbali zikiwemo dini za asili wanatarajiwa kushuhudia maajabu ya kituo cha Hija cha msalabani Nyamatongo katika Parokia ya Nyantakubwa Jimboni Geita, ambapo ndani yake wataadhimisha misa Takatifu itakayoongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Geita Mhashamu Flavian Kassala.

Wakristo wakatoliki wanafanya Hija hiyo kuanzia Jumamosi hii wakiadhimisha miaka 100 tangu kuwapata mapadri wa kwanza waafrika kutoka Kanda ya Ziwa, na pia miaka 150 tangu ukristo uingie Tanzania Bara. Eneo la Nyamatongo limesifika siku nyingi kutokana na msalaba ulioachwa na wamisionari tangu mwaka 1880-81 wakijaribu kuanzisha misheni hapo japokuwa haikufanikiwa.

Miongoni mwa masimulizi yaliyoenea hapo na kuwavuta watu wengi kutamani kufika hapo ni kifo cha ajabu cha Padri Andreas Combarieu, aliyefia hapo kwa homa ya ini, na kwa amri ya Mtemi Rwoma wa Karumo, alitupwa ziwani katika kisiwa cha Juma, usiku, lakini asubuhi yake wakamkuta anaelea ufukweni.

Wakazi hao, wakiwemo waamini wa dini zingine wamepanga kwenda kuona hicho kinachowavuta wakristo wengi kumiminika kila siku eneo hilo na kushinda huko kuanzia asubuhi hadi joni wakipanga mawe na kutengeneza barabara kwa ajili ya kuandaa tukio kubwa la misa Takatifu itakayofanyika jumamosi hii.

Akizungumza na Gazeti hili, Paroko wa Parokia ya Nyantakubwa jimboni Geita Padri George Nkombolwa amesema tukio hili ni fursa ya kuwajenga kiimani waamini wa Geita, lakini hata wafuasi wa dini nyingine wana hamu kubwa ya kuona  jinsi wakatoliki wanavyoheshimu msalaba wa Yesu na hivyo kuamua kulitunza eneo la msalabani.

Padri George Nkombolwa ambaye pia ni Mkurugenzi wa Uchungaji jimboni amesema kuwa Nyamatongo ni Mlango wa imani kwa kanda ya ziwa, kwani hapo walikaa mapadri watatu, Augustine Levesque, Ludovick Girault na Andreas Combarieu wa shirika la wamisionari wa Afrika (White Fathers) waliokuja na  msafara wa kwanza mwezi Desemba mwaka 1878 wakaenda Uganda, na baada ya kukataliwa Uganda, walikuja Karumo wilayani  Sengrema na wakakaa hapo Nyamatongo msalabani.

Miongoni mwa mambo wanayofanya wakristo wa Parokia ya Nyantakubwa katika maadhimisho hayo ni pamoja na kujenga makumbusho (MUSEUM) itakayotoa masimulizi juu ya Padri huyo Andreas Combarieu na mapadri walioishi hapo

Comments

  1. Ama hakika ni chanzo Bora kuenea kwa Imani kwa Kanda ya ziwa na tunamshukuru sana fr.George kwa kujitoa kwake kuhakikisha eneo hilo linaendelea kimiundombinu ambayo itakidhi mahitaji ya mahujaji wote kwa Jimbo la Geita .Ee Mungu uibariki Imani katoliki

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU