HIJA JIMBONI MBEYA YATIA FORA, MAHUJAJI ZAIDI YA 485 WASHIRIKI


WITO umetolewa kwa  Wakristo  wakatoliki nchini  kutobaguana kutokana na vyama  vya kitume na badala yake  wamealikwa kumtumia Mama Bikira Maria  kama daraja kufikisha maombi  na sala zao kwa Mwenyezi Mungu.
Akizungumza katika ibada ya misa takatifu  ya hitimisho la Mahujaji wa utume wa Fatima  wa jimbo la Mbeya, Njombe na Tunduru Masasi iliyofanyika katika Kanisa  la Mtakatifu Izidori Mkulima, Parokia ya Izuo, Mkurugenzi  wa Utume  wa Walei, jimboni Mbeya, na vyama vya Mashirika  na jumuiya  za kitume jimbo, Padri Sirilo Mwalyoyo amewataka wakaristo kumtumia Mama Bikira Maria  kufikisha maombi  yao kwa  Mungu ili  wapate kusamehewa.
Padri Mwalyoyo  ambaye pia ni Mratibu  wa Idara ya Uchungaji Jimbo Katoliki Mbeya amewaalika mahujaji  wasiache  kusali rozali kwani kwa imani ya Kanisa  na kupitia mafundisho yake na mapokeo yanawafanya  wapate  ufunuo kamili kujuwa Mungu ni nani.
 “Kipindi cha likizo za kufungwa shule  ndipo ada  za semista  zinahitajika  na ndiyo kipindi ambacho baba  akimuona mtoto anakunja sura  anajuwa muda wa maombi ya ada umewadia  na hivyo watoto wanawatumia mama zao  waweze kufikisha ujumbe kwa baba kwa sababu wanajuwa kabisa mama anajuwa mbinu za kumuingia baba, atamuandalia chakula na vipande vizuri vya kuku na maneno mazuri  na ndipo Mama anaingizia ombi la ada,  na ndivyo  ilivyo hata kwa Mama Maria,” amesema Mkurugenzi huyo huku akishangiliwa na Mahujaji.
Ameongeza,”Na sisi tunamuogopa Mwenyezi Mungu kwa sababu  ya dhambi zetu hivyo, kupitia kwa Mama Bikira Maria atafikisha maombi yetu ya kusamehewa dhambi, katika maandiko tunasoma kuwa Yohane mbatizaji alisema anakuja mkubwa kuliko mimi naye ni Kristo bwana  na  Malaika   waliwaambia wachungaji tumewaletea habari njema amezaliwa mwokozi ambaye ni Kristo na  tunaona pale msalabani Yesu  alimwambia Maria  mtazame Yohane huyu ndiye mwanao na wewe Yohane huyu ndiye Mama yako na Yohane pale pale alimchukuwa  Mama Bikira Maria kwenda nyumbani kwake.”
“Hivyo nawaombeni sanamu ya Bikira Maria inayotembea  na kupitishwa na Radio Maria  muipokee kwa shangwe, muikimbilie na msiikimbie kwa sababu mkiikimbia mtaikuta huko mnakokimbilia na pendaneni muwe  wa  utume  wa moyo mtakatifu wa Yesu, utume wa Francisco wasaikulari, wakarismatiki, utume wa Fatima, Legio Maria,Wanafrancisco, Kwaya au vijana ninyi nyote ni kiungo kumbukeni Yesu alisema mwili wake una viungo vingi  lakini kichwa ni kimoja ambacho ni yeye mwenyewe, kumbukeni ninyi nyote ni viungo katika mwili wa Kristo, hakuna anayemzidi mwenzake,”amesisitiza Mkurugenzi na Mratibu huyo.
Akizungumza wakati wa kumuomba Mkurugenzi Padri Mwalyoyo  kutunuku hati maalum kwa mahujaji, Mwenyekiti wa utume wa Fatima Jimbo la Mbeya,Venance Ntakabile amemshukuru Mhashamu Askofu Evarist Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya ambaye ni Rais wa Utume wa Fatima ulimwenguni nchini Tanzania  kwa ufunguzi wa ibada ya misa takatifu ya Hija  na yote  aliyowaasa watayazingatia  na yataendelea kuwaimarisha.
Mwenyekiti huyo  ametaja masista walioshiriki Hija hiyo kuwa ni watatu na mapadri  sita  ambapo  amesema Hija ya mwaka  huu imetia fora kutokana na  kushiriki  mahujaji  485 kutoka Parokia 35 kati ya Parokia 45 za Jimbo Katoliki Mbeya  wakiwemo na mahujaji  watano  kutoka majimbo jirani ya Tunduru Masasi na Njombe.
Ntakabile amesema katika Hija  iliyofanyika mwaka 2016 katika Parokia  ya Bara, mkoani Songwe jumla ya mahujaji 344 walishiriki  ambapo  pia amemshukuru Mungu kwamba hakuna mahujaji walioumia  na wote wamehitimisha salama.
KIONGOZI  imezungumza na Mahujaji  kwa nyakati tofauti kupata  maoni yao  kuhusu Hija hiyo  ambapo Mzee Elia Mwanjale kutoka Kata ya Kisondela, Parokia ya Kisa,Wilaya ya Rungwe, amesema  wamepata semina  ambayo imewaimarisha kiroho na kiimani.
“Tumejifunza  na kukumbushwa  kuwa wanyenyekevu,wapole,wenye huruma, upendo kwa watu wote na tumeamka salama  na  na tunamshukuru Mungu kwa kuhitimisha  Hija salama  na  tunaahidi kwenda kuwa chachu  ya matendo mema katika nyumba zetu,” amesema kwa furaha.
Mama Mangasila, kutoka Parokia  ya Mwambani, wilaya ya Songwe, mkoani Songwe  amesema kupitia Hija  amekuwa shuhuda mzuri  wa kutofikiwa na homa  nyumbani  kwake  na amekuwa akiyapata mafanikio  ya kupata vyakula na mahitaji muhimu  kwake na familia yake anayoishi nayo ambao ni wajukuu huku mahujaji  wengine  kutoka  parokia hiyo  Teodora Mwatowine na   Neema Ndolomi  wamesema  wamejifunza mengi  kuhusu ukatoliki  na wamewaomba vijana wajiunge katika vyama vya kitume waweze kunufaika.
“Na kupitia maigizo  ya njia ya msalaba  imetumkumbusha  kuwa Yesu  alikufa msalabani kwa ajili ya mateso yao hivyo tusitende  dhambi na kupitia mahubiri ya Mapadri inaendelea kutujenga  katika kutafuta utakatifu wa Mungu,”wamesema.
Enita Nyondo kutokea Jumuiya ya MtakatifuTerezia, Kigango cha Isongole Parokia ya  Itumba, na Marietha Kamwela kutoka Jumuiya ya Mtakatifu Paulo Wilaya ya Ileje, mkoani Songwe wamesema  wamejifunza mengi  katika Hija ya mwaka huu.
“Hakika  Hija imezaa matunda, na wengine wafike katika Hija nyingine  tukipata uzima  na  tunawaomba waume zetu  kushiriki  katika Hija nyingine  panapo majaliwa na  tunakwenda kuwahamasisha  na pia tumejifunza  mahusiano ya Mama Bikira Maria na mwanae Yesu,”wamefafanua.
Wamesema kuwa  kuwa  katika hija hiyo  mahujaji waliofika na waume zao  wamejifunza mengi hivyo wamemuomba mungu na Mama Bikira Maria ili  aweze kuwasaidia katika hija nyingine wakawashawishi  waume zao  kushiriki  na kuweza kuimarisha  kupitia salama,mafungo,maungamo na mafundisho.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Utume wa Fatima Parokia ya Mbeya, Josephine Kamunga kutoka Jumuiya kuu ya Mtakatifu Yuda Tadhei,Sisimba jijini Mbeya  amesema Mama Bikira  ameendelea kumtendea miujiza mingi ya mafanikio katika maisha yake  na kwamba  kwa kasi ya ajabu  katika hija hiyo  wamevuna samaki wengi (wanachama)  na anaamini kwamba  baada ya miaka mitatu  wanaweza kufikia wanautume zaidi ya 1000 huku akiahidi kuendelea  kumtangaza Mama Bikira Maria ndani na nje ya  jimbo na nchi kwa ujumla.
Kutoka Jimbo la Njombe, Parokia ya Matamba, Alubina Mushi  ambaye pia ni mjumbe  wa Utume wa Fatima Taifa  amesema licha ya kupata neema nyingi kupitia Hija hiyo lakini wamejifunza kutoka jimboni na kuwa  katika Hija  ya Jimbo Mbeya  kuna  mahujaji na wana utume  wengi  wakiwemo vijana na   wanaume na hivyo majimbo mengine   wanapaswa kuiga  na kusema mkristo  asiyeingia  katika vyama vya kitume ni sawa na kuingia katika shamba lisilo na mbolea.
Kutoka Jimbo Katoliki Tunduru Masasi, Parokia ya Makulani hujaji Mutali Maria amemshukuru Paroko wake Mwenisawa kumuhamasisha  kufika kujifunza kuhusu  utume wa Fatima na Hija na hakika  wamevuna mengi
Katibu Mtendaji  wa Utume wa Fatima Taifa, Sr.Cecilia Ntongoro  amewaomba mahujaji kuwa mbegu waliyoipanda  iendelee kustawi ndani ya mioyo yao na kuwakaribisha katika Hija  kitaifa  itakayohusisha mahujaji kutoka nchi za jirani  Oktoba,10 hadi 13 mwaka huu itakayofanyika jimboni Mbeya  ili iendelee kustawisha roho zao
Sr.Cecilia  ambaye  pia  ni Katibu wa Utume wa Fatima  kwa Nchi za Kanda ya Afrika amewaalika wakristo wote  kushiriki  Hija  ya kiulimwengu   itakayohusisha Mahujaji wa Nchi za Bara la Afrika na Ulaya inayotarajiwa kufanyika mwaka 2018  nchini Tanzania katika jimboni Mbeya.
Aidha  akitoa shukrani  kwa mahujaji, Paroko wa Parokia ya Izuo, Padri Jeremiah Majengo amewashukuru viongozi wa Utume  wa Fatima Jimbo kwa kupita vigangoni kuelimisha  juu ya ukatoliki ambapo amesema Baba Askofu  Chengula  alitoa Sakramenti  ya Kipaimara kwa wakristo  25, sakramenti  ya  Ekaristi Takatifu  kwa waumini  48,wamebatizwa  wakristo 52, pamoja na kubariki ndoa.
















Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU