“Mkakati wa miaka 100 utanusuru mazingira” TEC



Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Padri Raymond Saba amewataka viongozi wa serikali na umma nchini kushirikiana na wadau katika kupanga mikakati ya miaka 100 ya utunzaji wa mazingira na siyo kuweka mikakati ya miaka mitano au kumi.
Padri Saba amesema kuwa kinachochangia kuendelea kuharibika kwa mazingira  ni kutokana na serikali kuweka mikakati ya mazingira ya miaka mitano mitano badala ya kuweka mikakati ya miaka 100, ambayo inadumu na kutekelezwa kwa muda mrefu.
Katibu Mkuu huyo ameyasema hayo wakati wa Kongamano la mazingira kwenye maadhimisho ya Siku ya mazingira kitaifa yaliyofanyika wilayani Butiama mkoani Mara kuanzia Juni Mosi hadi 4 mwaka huu, alipokuwa akizungumzia nafasi ya imani ya dini katika kuhifadhi mazingira.
Padri Saba amebainisha kuwa suala la mikakati ya miaka 100 litaweza kusaidia katika kuboresha usimamizi mzuri wa uoto wa asili na utunzaji wa mazingira, kwa kuwa kila kiongozi anayeingia madarakani  anaingia na sera yake, ambayo anaitekeleza kwa muda wa utawala wake yaani miaka mitano au kumi tu, na akishaondoka sera ile inakuwa haitumiki tena, lakini mikakati ya muda mrefu ikiwekwa itaboresha hali ya mazingira.
Aidha padri Saba ameshauri kuwa ili kuweka msisitizo mkali juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira na uoto wa asili kwa ujumla ni vyema somo la mazingira liwepo kwenye mitaala ya elimu kuanzia shule ya awali hadi ngazi za juu, na kuwashirikisha wadau mbalimbali, ili  hata mwanafunzi awe na ufahamu mzuri juu ya suala zima la utunzaji wa mazingira, katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi tangu akiwa mdogo.
“Kama kungekuwepo na mikakati  ya mazingira ya miaka 100 tungeweza  kufaulu, lakini sera ya miaka mitano haitekelezeki na ndio maana tumefika hapa tulipo, na tusiongelee mabadiliko ya tabia nchi bali tuongelee tabia za watu, na tukiamua na  tukashirikiana kwa pamoja kuanzia elimu ya awali pamoja na wadau wa mazingira tutafaulu kutunza mazingira, kwani Kanisa tumekuwa  tukijitahidi kushauri watu wabadilike, na inawezekana kabisa watu kubadilika na mazingira yetu yakabaki na uoto wake wa asili,” Amesema Padri Saba.
Wakichangia mjadala huo wa nafasi ya imani ya dini  katika kuhifadhi mazingira, wadau mbalimbali wa mazingira wamesema kuwa bado viongozi wa dini hawajafanikiwa sana kwa kuwa binadamu amekuwa mharibifu wa kwanza wa mazingira na wao hawajawashauri waamini kupanda miti ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi .
Wadau hao wamesema kuwa hata katika uumbaji Mungu aliumba kila kitu na mwanadamu alikabidhiwa mazingira yakiwa safi bila uharibifu wowote, lakini  ndiye amekuwa kwa kwanza kuharibu ambapo waliwaomba viongozi wa dini kusimama na kukemea uharibifu huo, kwani hata madhara ya mabadiliko ya tabia nchi yanayotokea sasa ni kutokana na mwanadamu kuharibu mazingira.
Patrick Kihoza kutoka Chuo kikuu cha Mzumbe amesema kuwa  viongozi wa dini wana nafasi nzuri ya kuonya juu ya uharibifu wa mazingira kama wataamua kwa pamoja kulisimamia, kwa kuwa kila jambo linapoonekana kuwa gumu viongozi wa dini wamekuwa wakilifanya kuwa jepesi kwa kuwaasa waamini wao makanisani na misikitini juu ya madhara ya uharibifu wa mazingira na matokeo yake yamekuwa yakionekana, hivyo amewaomba kusimama na kukemea suala la uharibifu wa mazingira ili kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU