WATAWA WAEPUKE UBINAFSI-ASKOFU CHENGULA




ASKOFU wa Jimbo Katoliki Mbeya Mhashamu Evarist Chengula  amewapongeza wajubilanti 6 kwa kutimiza miaka 25 ya nadhiri ya utawa huku akibainisha kwamba hiyo siyo kazi  rahisi  kwa mapenzi yao bali wanapaswa kumshukuru  Mwenyezi Mungu  na kuendelea kumuomba awasaidie  ili wazidi kusonga mbele  kwa kushirikiana katika mashirika yao.

Askofu Chengula  ameyasema hayo  wakati wa Homilia  ya adhimisho la misa takatifu  ya miaka 25 ya utawa  na kuweka nadhiri za daima  kwa masista sita  wa Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume wa Mbeya  iliyofanyika katika  Kanisa Kuu la kiaskofu  la Mtakatifu Anthony wa Padua Parokia ya Mbeya Mjini.

Wajubilanti hao walioadhimisha  miaka 25 ya utawa na kula kiapo cha nadhiri za daima ni Sr.Astrida Katimbuka, Sr.Asteria Nyamwela, Sr.Victoria Aswile, Sr.Yosepha Ayobangila, Sr.Adelphina Kipangula na Mkurugenzi wa Idara ya Mawasiliano Jimbo Katoliki Mbeya, Sr,Joyce Nchalla  wote wa Shirika la Bikira Maria Malkia wa Mitume wa Mbeya
.
Amesema kutimiza miaka 25 ya  utawa kwa kuachana  na   kila kitu katika ulimwengu na kuamua kumtegemea Mwenyezi Mungu  na kuwaletea  watu neema ya kiroho na kimwili si kazi ndogo, hivyo  amewapongeza na kuwaalika  kuendelea   kumtegemea na kumuomba Mama Maria  kama alivyofanya kwa  Elizabeth awaongoze  katika kuendelea  kuwatendea mema  wengine.

Amesema  nguvu zao hazingetosha kufikia  miaka 25 hiyo bali ni kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, lakini kadri miaka inavyozidi kusonga mbele kuna hatari ya baadhi ya watawa  kuwa na roho ya mgando ya uvuguvugu, hivyo  amewakumbusha kuwa  duniani ni mahali pa kutafuta ukamilifu.

“Mmetembea  na kufanya kazi hiyo  kwa miaka 25 kwa kutembea na Mwenyezi  Mungu, hivyo muamshe nguvu  hiyo ndani ya  mioyo yenu, ninyi mnayaona kama mambo ya kawaida lakini muelewe  hayo mambo hayazoeleki wala si ya kawaida  kwani  sisi tulio nje tunayaona siyo ya kawaida, kumbuka wazazi wenu, ndugu, jamaa na marafiki wameacha kazi zao wamekuja kuwashuhudia  kuwasikia  na mnavyojivunia   kwamba mtaendelea tena kwa  kumtegemea Mwenyezi Mungu katika maisha hayo,”

“Nawatakia ujumbe mwema wa Mama Maria daima kuona mnawajibika kuwaletea watu neema na popote mtakapokuwa  lazima iwe sababu ya majirani kupata neema, neema ya kutambua uwezo wake Mwenyezi Mungu kama Mama Maria alivyofanya kwa Elizabeth.”

Askofu Chengula  amewaasa watawa kuwa sehemu ya faraja  kwa maisha ya  wenzao watakao kumbana na magumu akibainisha kuwa ikitokea basi wasimuache mwenzao anahangaika ili asijisikie mpweke akakata tamaa lakini kama watamfuata Mama  Maria itakuwa ni rahisi kwao kwenda kuzungumza na mwenzao aliyepo kwenye matatizo na siyo ya kimali  au kimwili  bali ni katika mambo ya kiroho.

“Sote tunajuwa kuwa watawa wameingia utawani  kwa ajili ya kuwa wakamilifu kama Mungu Baba na tukiona ndugu yetu hafuati mfumo huo, huo  ni umaskini  lazima kwenda kumsaidia na kumsalimia  siyo lazima kumpigia kelele, ila  Roho wa Bwana anayekuwa ndani yetu ndiye atakayemsukuma, atakayemfanya atambue kwamba yeye ameingia katika Shirika kwa ajili ya  kujikamilisha, wengine wanasema kujitakatifuza, kukamilisha utakatifu,”amesisitiza.

Amewaalika  kuwa  kielelezo cha upendo  katika  utume huo kwa  kutembeleana  na kuwasihi endapo itatokea  mwenzao  katika hali ya kibinadamu   hataki kukutana na Roho Mtakatifu, kwa kuwakwepa  wajue kuwa anakumbana na nguvu ya kiza, wasimtenge bali wawe naye kwa njia ya kumuombea na kuzungumza naye daima.

Aidha Askofu Chengula  amesema  watawa  wanaoadhimisha  nadhiri ya miaka 25  waepuke  kufanya utume kwa mapenzi yao  na kupitia siku hiyo  inawakumbusha  wengine kuacha  mapenzi  yao  na kutakiwa kufuata  mapenzi ya Shirika  ambalo linaongozwa na Kanisa.

 “Chagueni  viongozi  kwa  manufaa ya shirika  na mjue  kuwa mbele yenu pamoja na Mama Maria ni kazi moja kuwachagua watu watakaowasimamia muwe wakamilifu siyo kufanya katika mapenzi yetu, na siyo kuchagua  watu wa  mkoa gani, au vijana, hapana tufurahi, tuwe watu wa kushukiwa na roho,”Amefafanua.

Amebainisha  kuwa  viongozi watakaokuwa wanawachagua  wajue kuwa wameshukiwa na Roho Mtakatifu ili awasaidie, huku akiendelea kuwasisitiza kuzingatia  na kuziishi kanuni za Kanisa na Shirika lao katika muongozo wa pamoja  hasa katika kukazia juu ya kusali.






Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU