KIONGOZI MBIO ZA MWENGE ALIPONGEZA KANISA KATOLIKI




Kiongozi wa mbio za Mwenge kitaifa mwaka 2017 Bw. Amour Ahmad Amour amelipongeza Jimbo Katoliki Ifakara kwa kuendeleza mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya Good Samaritan kwa ajili ya matibabu ya wagonjwa wa Kansa iliyopo katika Halmashauri ya mji wa Ifakara.
Bw. Amour amesema hayo hivi karibuni kwenye Msafara wa Mwenge wa Uhuru ulipofika katika eneo la ujenzi wa mradi huo na kuweka jiwe la msingi ambapo ujenzi huo unatarajiwa kukamilika kabla ya mwezi Desemba mwaka huu.
Aidha Kiongozi huyo wa mbio za Mwenge Kitaifa kwa mwaka huu amesema kuwa kukamilika kwa Hospitali hiyo kutasaidia watu wengi kupata huduma kwa urahisi kwani huduma zitakuwa zikitolewa bila malipo  ambapo wananchi wengi wenye matatizo ya Kansa kutoka maeneo yote nchini watahudumiwa bure wakiwa hospitalini hapo.
“Nawapongeza sana na nawaomba msichoke kufanya vitu vizuri kama hivi, kwani kukamilika hapa kutasaidia wananchi wa Ifakara, Kilombero, Morogoro na Tanzania nzima tena kuna watu wengine watatoka kwetu Zanzibar kuja hapa na tunawaomba muwapokee,” amesema Amour.
Pia Amour amewataka wananchi wote wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara na Wilaya ya Kilombero kwa ujumla kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Kanisa Katoliki kwa kuwezesha huduma mbalimbali hususani za afya kwa jamii.
Katika Risala iliyosomwa na Padri Jerish Geory kwa niaba ya Jimbo Katoliki Ifakara, amesema kuwa  mradi huo ulianza mwaka 2015 na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.
Aidha ameeleza lengo la mradi huo kuwa ni kutoa matibabu kwa wananchi wa hali ya chini ambao hawana uwezo wa kwenda kupata matibabu katika hospitali mbalimbali zilizopo mikoa ya mbali.


Risala hiyo pia ilibainisha utekelezaji wa mradi kuwa mradi huo kuwa mpaka kukamilika kwake unatarajiwa kuwa na majengo 11 ikiwa ni pamoja na wodi 4, jengo la utawala, jengo la mapokezi, jengo la mikutano, chumba cha upasuaji pamoja na miundombinu mingine ya msingi,  ambapo mpaka sasa zaidi ya Majengo 9 yapo katika hatua za umaliziaji.
Naye  Mkuu wa Wilaya ya Ulanga aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya  Kilombero Bwana Jacob Kasema amesema kuwa anathamini uwepo wa Jimbo Katoliki na kuomba makanisa mengine kuunga mkono jitihada mbalimbali ili kusaidia kupunguza changamoto za afya,  elimu na maji kwa jamii. 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU