MIAKA 50 YA UCHUNGAJI: PADRI SHAO AMSHUKURU MWENYEZI MUNGU



Padri Pius Shao anayefanya utume katika Jimbo Kuu Katoliki Arusha, ameadhimisha miaka hamsini (50) ya Upadri, adhimisho ambalo limekwenda sambamba na Misa Takatifu kumshukuru Mungu kwa yote aliyomjalia katika kipindi chote hicho.
Akimwakilisha Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Arusha,  Wakili wa Jimbo hilo  (Vicar General) Padri Simon Tenges katika mahubiri yake, amemfananisha padri Shao na mmoja kati ya wagonjwa kumi wa ukoma walioponyeshwa na Yesu na kurudi  kumpa Yesu Kristo shukrani.
Padri Pius amefanya mengi katika Jimbo Kuu Arusha, hasa wakati akiwa Mkuu wa Idara ya Uinjilishaji ambapo ametembelea parokia na vigango mbalimbali katika Jimbo lenye ukubwa wa Kilometa za mraba 64,340 akiinjilisha kwa kina. Amechangia kufunguliwa parokia mpya ya Enduimet na vigango vyake wakati huo huo akiimarisha parokia nyingine mpya ya Kamwanga na vigango vyake.
Pia Padri Simon Tenges amemfananisha na askari hodari aliye vitani anayetetea watu wake bila kuangalia kabila lao, dini,  mila au desturi huku akisaidia pia ujenzi wa Hospitali yenye hadhi, shule ya chekechea na kuboresha mazingira ya asili ya maeneo ya wakaaji wake.
Hata hivyo padri Pius Shao amekumbana na vizingiti vingi vya mazingira, mila na tamaduni hasa zile potovu, na ameweza kukabiliana navyo kikamilifu, hii ni pamoja na kuweka watu wa matabaka, hulka na tabia tofauti katika kundi moja linalopendana na kusaidiana.
Kwenye Misa hiyo ya kumshukuru Mungu, wamehudhuria mapadri kadhaa wa Jimbo Kuu Arusha na wana jubilee wenzake wawili kutoka Jimbo Katoliki Moshi, padri Caetan Kazi na Everist.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU