Askofu amwomba IGP Sirro Kanda Maalumu Ngara


ASKOFU wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara, Mhashamu Severine Niwe-Mugizi, amesema ana imani na uongozi wa Mkuu mpya wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro na amemuomba kuunda kanda au mkoa maalumu wa kipolisi katika Jimbo hilo ili kukabili matukio ya kihalifu yakiwamo ya uingizaji silaha haramu nchini.
Maeneo mbalimbali ya mipakani mwa nchi hususani katika mikoa ya Kagera na Kigoma yamekuwa na matukio mengi ya kihalifu yanayodaiwa kuchangiwa pia na wahamiaji haramu au wakimbizi toka nchi jirani za Rwanda, Burundi na hata Uganda.
Hivi karibuni, Rais John Magufuli amemteua aliyekuwa Kamanda wa Polisi Kanda Malumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simon Sirro, kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania akichukua nafasi ya Ernest Mangu ambaye taarifa ya Ikulu ilisema, atapangiwa kazi nyingine.
Wakati watu mbalimbali wakimhimiza kutupia macho na kusafisha maeneo mbalimbali yanayolalamikiwa yakiwamo mauaji yanayofanywa na watu wasiojulikana huko Kibiti na maeneo mengine mkoani Pwani, malalamiko ya raia kubambikwa kesi, ujambazi wa kutumia silaha na uhusiano mbaya na baadhi ya vyama vya siasa na jeshi lake, yeye mwenyewe amesema amejipanga kupambana na matukio ya kihalifu hata kama ni kwa ubaya.
Akizungumza kwa simu na KIONGOZI toka Rulenge, Mhashamu Niwe-Mugizi amesema katikati ya juma kuwa, ingawa mara nyingi amekuwa akitoa ombi hili lakini halitekelezwi, hataacha kutimiza wajibu wake wa kusema na kukumbusha yale anayoona yanafaa kwa ustawi wa jamii.
“Hiki kilio changu sasa kimekuwa kama machozi ya samaki hata yakitoka, hakuna anayeyaona maana yote yanaishia majini tu. Nimesema mpaka sasa nimechoka, lakini hakuna anayejali sijui tunasubiri lipi litokee,”amesema.
Mhashamu Niwe-Mugizi amesema Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara ambalo kikanisa linahusisha wilaya za Ngara, Chato na Biharamulo, ni eneo lenye changamoto nyingi za kiusalama kwa kuwa lipo jirani na nchi ambazo mara nyingi zina migogoro na hivyo, kuingilika kirahisi na wahamiaji haramu au wakimbizi ambao baadhi yao huwa na silaha haramu zinazotumika kufanya uhalifu nchini.
“Ngara ni eneo hatarishi kutokana na kuwa jirani na nchi za Rwanda, Burundi na Uganda na kutokana na mwingiliano wa watu, ni vigumu kuwadhibiti na hivyo usalama unakuwa kidogo. Wakimbizi wengi wanapita hapa kwenda kwenye makambi. Huu mwingiliano rahisi, unatuweka sisi watu wa maeneo haya katika hatari,” amefafanua.
“Namuomba sana huyu IGP mpya, atusikie ili tusisubiri mpaka jambo lifumuke na mambo yaharibike, eti ndipo tuanze kukimbia kama zimamoto. Ndiyo maana ninaliomba Jeshi la Polisi na Serikali kwa jumla, waliangalie eneo hili kwa jicho makini kabisa na kulifanya kuwa Kanda au mkoa maalumu wa kipolisi. Hii itaimarisha usalama eneo hili.”

Amesema kutokana na mwingiliano uliopo na nchi jirani, anaamini kuwa silaha nyingi zinazotumika katika maeneo mbalimbali nchini kwa mambo ya kihalifu, zinapita maeneo hayo na hivyo, lazima kushtuka mapema badala ya kusubiri madhara zaidi kutokea.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU