ASKOFU MINDE AWAASA WAZAZI KUCHOCHEA MAADILI




Wazazi wamehimizwa kuchochea maadili kwa watoto katika kipindi hiki ili waweze kuishi maisha yanayompendeza Mungu na jamii kwa ujumla kwani bila hivyo kuutafuta ufalme wa mbingu haitawezekana.

Maneno hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama Mhashamu Ludovick Minde katika adhimisho la ibada ya misa ya kupaa kwa Bwana katika parokia ya Ekaristi Takatifu Kabuhima.

Askofu Minde amesema hata katika uumbaji, Mwenyezi Mungu alimuumba Eva kutoka ubavu wa kuume wa Adam hivyo hata katika maadhimisho ya siku ya kupaa kwaYesu Kristo jamii inakumbushwa kuwa anakwenda kukaa kuume kwa Mungu Baba.

“Baada ya kupaa mbinguni Bwana wetu Yesu Kristo, wafuasi wake walishikamana pamoja nao wanawake na Mariamu mama yake Yesu na ndugu zake, hawa wote  walidumu kwa moyo mmoja katika kusali. Hata sisi inatupasa kusali na kufanya kazi.”

Naye Dekano wa dekania ya Ushirombo ambaye pia ni Paroko wa parokia ya Ekaristi Takatifu Kabuhima padri Salvatore Guerrera, amemshukuru Mhashamu Askofu kwa moyo wa upendo kwa wanaparokia ya Ekaristi Takatifu kwani amekuwa akiwatembelea mara kwa mara na hii inadhihirisha kuwa huwa anawakumbuka katika maombi na sala.


 Amemshukuru pia Sista Mkuu Mama Theresia wa shirika la wamisionari Wabenediktini kutoka Ndanda Mtwara pamoja na watawa wenzake ambao wapo parokiani hapo kwa ajili ya kusalimia na kusali pamoja na wanafamilia wa Mungu.

Na, Shokolo Hosea, Kabuhima Kahama 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU