Askofu Ruzoka akikabidhi kituo cha afya Kaliua majengo yenye thamani ya shilingi 700,000,000



Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora Mhashamu Paulo Ruzoka hivi karibuni amekabidhi majengo mapya katika kituo cha afya Kaliua yenye thamani ya shilingi milioni mia saba (700,000,000) ikiwa ni juhudi ya kumkomboa mwanadamu dhidi ya adui maradhi.
Akikabidhi majengo hayo mapya Askofu Mkuu Ruzoka amesema Kanisa Katoliki linashirikiana na Serikali ya Tanzania katika juhudi za kumkomboa mwanadamu dhidi ya maradhi ili aweze kujipatia maendeleo kwa wakati, na kwa mantiki hiyo Jimbo Kuu Katoliki Tabora limeendelea kukuza maendeleo kwa kutoa huduma za afya, elimu, maji safi na salama na nyanja zingine za kijamii.
Askofu Mkuu Ruzoka amewaagiza waganga na wauguzi wa kituo hicho cha afya kutunza miundo mbinu yote ya kituo na kutoa huduma yao kwa weledi ili huduma iende sambamba na miundo mbinu mipya iliyokabidhiwa.
Pia Askofu Mkuu Ruzoka aliwataka waganga na wauguzi kulenga zaidi watu wa kipato cha chini katika kuwapa huduma bora akinukuu maneno toka mwinjili Matayo kuwa chochote mlichomtendea mmoja wa hao wadogo mlinitendea mimi.(Mt.25:31-46)
Baadhi ya majengo mapya aliyoyabariki na kukabidhi ni jengo la wagonjwa wa nje yaani (OPD) , wodi ya wakina mama, wodi ya wanaume, wodi ya watoto, wodi ya wakina mama wajawazito na chumba cha kuhifadhia maiti (mortuary), vyote vikiwa na thamani ya shilingi milioni 700 za kitanzania.
Akitoa mahubiri yake katika Misa Takatifu ya kukabidhi majengo hayo, Askofu Mkuu Paulo Ruzoka ameiomba Serikali kuhakikisha inatoa ulinzi wa watanzania na mali zao ili Kanisa lipate mazingira rafiki ya kumletea maendeleo mtanzania, kwani pasipo na amani hakuna maendeleo yoyote yanayoweza kufanyika.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka ametoa wito kwa waamini wote kutumia kituo hicho cha afya ili kuboresha afya zao na kupuuza baadhi ya watu wanaowagiribu watu wasitumie huduma za afya kwa kisingizio cha Mungu peke yake kuwaponya bila msaada wa huduma za kitabibu.
Naye Katibu wa afya Jimbo Kuu Tabora padri Alex Nduwayo akitoa taarifa yake amesema kuwa kituo bado kina changamoto kama vile uchakavu wa baadhi ya majengo kama vile chumba cha upasuaji, vifaa tiba nakadhalika.
Mganga Mkuu wa mkoa wa Tabora aliyetoa salamu kwa niaba ya Serikali amepongeza juhudi zilizofanyika kuboresha miundo mbinu hiyo na kuahidi kuongeza wahudumu katika kituo cha afya na kuwapa changamoto ya kuangalia upya huduma za kituo hicho hasa upande wa mama na mtoto ili kupunguza rufaa za hospitali jirani ya wilaya ya Urambo.
Kituo cha afya Kaliua kilianzishwa kama zahanati tarehe 2.7.1962 na aliyekuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Tabora Hayati Marko Mihayo chini ya usimamizi wa masista wa Grail. Mwaka 1971 kituo kilichukuliwa na Serikali na watumishi wote kulipwa mishahara na serikali, ambapo tarehe  15.8.1997 Serikali ilikabidhi kituo kwa Jimbo Kuu Tabora chini ya uongozi wa Hayati Askofu Mkuu Mario A. Mgulunde na shirika la masista wa Mabinti wa Maria walianza kutoa huduma  mpaka leo hii.
Jimbo Kuu Katoliki Tabora limetekeleza mradi huu kwa ushirikiano na Baraza la Maaskofu Katoliki Italia (CEI).  Hafla hiyo ilihudhuriwa pia na Mbunge wa Kaliua Mh.Magdalena Sakaya , mwakilishi wa Mkuu wa wilaya ya Kaliua, na mwakilishi wa Mkurugenzi wa Kaliua.

Kituo hicho cha afya kinatarajiwa kupanda hadhi na kuwa Hospitali hivi karibuni.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU