MAFRATERI WAWE NA MALENGO ENDELEVU



Mafrateri wa seminari Kuu ya Mtakatifu Paulo Mtume Kipalapala wameaswa kuwa na malengo endelevu katika maisha yao ya kila siku ili kuweza kuhimili changamoto za maisha yao hapo baadaye.
Rai hiyo imetolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora Mhashamu Paulo Ruzoka hivi karibuni katika Adhimisho la Misa Takatifu aliyoiadhimisha seminarini hapo.
Askofu Mkuu Ruzoka amesema kila mwanadamu anapaswa kuishi mwenyewe katika maisha yake ya kila siku na si kuishi maisha ya mtu mwingine au maisha tegemezi ambayo si rahisi kumfanya mtu huyo kujiletea mafanikio.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka amewaomba mafrateri kuishi maisha adilifu yatakayowasaidia kufikia lengo kuu yaani uzima wa milele na hasa wajihoji daima nipo wapi? naenda wapi? aina hii ya maswali ni muhimu katika safari yao ya kuelekea maisha ya upadri, bila hivyo wataishia kutapatapa.
Askofu Mkuu Ruzoka pia ametoa wito kwa wabatizwa wote wajibu wa kusaidiana na kuelekezana yale yanayotupeleka katika uzima wa milele.
Katika mahubiri yake Askofu Mkuu amewasisitiza mapadri, mafrateri, watawa na wahudumu wa seminari daima kuchangamkia sakramenti za Kanisa bila kusahau sakramenti za upatanisho na Ekaristi Takatifu zinazotupatia uwepo wa Kristo Yesu katika maisha yetu ya kila siku.
Akilinganisha wito wa Ibrahim, Askofu Mkuu ametoa wito kwa kila mkristo kujitahidi kudumu katika Imani na Utii kwa Mungu hasa wakati wa changamoto tunazokutana nazo katika maisha na daima tuyapokee mapenzi ya Mungu bila kukata tama, kwani yote kwa Mungu yanawezekana.
Aidha mafrateri wameelezwa umuhimu wa kujiwekea utaratibu mzuri katika maisha yao ili waweze kutumia muda wao vizuri ili kuhimili changamoto za ulimwengu wa leo.
Wakati huohuo, Askofu Mkuu Ruzoka ametoa wito kwa kila mkristo kuiombea nchi yetu amani na utulivu kwani pasipo na amani hakuna maendeleo.
Mwaka huu 2017 mafrateri 24 toka majimbo mbalimbali Tanzania wamehitimu malezi yao seminarini hapo. Mahafali hayo yamehudhuriwa na mapadri, watawa, mafrateri na wahudumu wa seminari.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU