Kahama wamkumbuka Mtakatifu Karoli Lwanga





Padri Peter Kadundu wa Jimbo Katoliki Kahama amewataka  waamini  kuwa mashuhuda wa imani kiroho na kimwili  kwa kuishi maisha ya matendo mema ya sala ya kumpendeza Mwenyezi Mungu na kuwa na upendo kwa  watu wote.

Padri Kadundu ambaye ni makamu wa Askofu amesema hayo alipokuwa akihubiri kwenye adhimisho la misa takatifu ya kumkumbuka Mtakatifu Karoli Lwanga iliyofanyika katika Kanisa kuu la Mtakatifu Karoli Lwanga, parokia ya Kahama mjini.

Katika homilia yake, padri Kadundu amesema katika maisha wakristo wanapaswa kuyajua na kuyatambua mambo matakatifu kisha kuyatangaza  na kumuomba Roho Mtakatifu awajalie kuwa wamoja wenye moyo uliojaa  furaha na undugu.

Amesema wakristo wamefundishwa Katekisimu na kuipokea,  wanapaswa  kuishika kwa kutambua  kuwa kuna Mungu, Yesu Kristo na Roho Mtakatifu  na ndiyo maana Mtakatifu Karoli Lwanga na wenzake walikubali kufa kifo cha mateso makali ya kuchomwa  moto na kuungua kwa kukiri imani hiyo.

Kwa upande wake akizungumza na waamini baada ya misa hiyo takatifu, paroko wa  parokia ya Mtakatifu  Karoli Lwanga Kahama Mjini, Padri Robart Lujula amewataka waamini kuishi maisha matakatifu ya kiroho na kimwili kwa kutenda mema katika jamii.

Parokia ya Mtakatifu Karoli Lwanga iliyopo Kahama mjini ilianzishwa mwaka 1965 wakati huo ikiwa chini ya Jimbo Kuu Tabora  hadi mwaka 1990 ilipomegwa na kuwa chini ya Jimbo Katoliki Kahama chini Askofu wa kwanza mwasisi hayati Askofu  Mateo Shija.




Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU