Miaka 100 ya Upadri/ 150 ya Uinjilishaji: Waamini watakiwa kuvienzi vituo vya ukuaji wa Imani



Wakristo nchini wametakiwa kujali na kuthamini vitovu  na vyanzo vya ukuaji wa imani katika majimbo mbalimbali nchini ili kuimarisha uinjilishaji.

Wito huo umetolewa na Padri Cosmas Makasi parokiani Kate katika Kanisa la Jiweni Kamba wakati wa maadhimisho wa mwaka wa mapadri kijimbo na Hija iliyohusisha mapadri wote wa Jimbo Katoliki Sumbawanga iliyofanyika hivi karibuni.

Padri Makasi amesema kuwa katika kuadhimisha Jubilei ya miaka 150 ya ukristo na miaka 100 ya upadri ni vyema wakristo hasa waamini wakatoliki kuheshimu misingi na vitovu vya imani vilivyoanzishwa na mapadri weupe (White Fathers) na kuviendeleza.

“Ni wajibu wetu wakristo wakatoliki nchini kote tunapoadhimisha jubilei ya miaka 150 ya imani yetu na miaka 100 ya mapadri kutunza na kuendeleza maeneo, miradi, makanisa na huduma mbalimbali walizoziasisi watangulizi wetu ambao walitufanya kuitambua imani na kwa kufanya hivyo tutakua tunatunza kumbukumbu ya imani yetu kwa vizazi vijavyo katika historia ya Kanisa," amesema padri Makasi.

Maadhimisho ya miaka 100 ya upadri jimboni Sumbawanga yamefanyika katika Kanisa la kwanza kujengwa jimboni Sumbawanga ambalo limependekezwa kuwa Kanisa la Hija lililopo maeneo ya Jiweni Kamba mwambao mwa ziwa Tanganyika lililopo katika parokia ya Kirando jimboni Sumbawanga.

Akihitimisha Kongamano hilo la mapadri lililojumuisha mapadri wa Jimbo Sumbawanga, Mwenyekiti wa mapadri jimboni humo padri Joachim Sangu amesema kuwa katika kila mwaka   kupitia Dominika ya Moyo Mtakatifu wa Yesu jimboni Sumbawanga ni siku ya  mapadri kijimbo ambapo hufanya Hija, mafungo na mikutano ya ndani vyote vikiwa na lengo la kutakatifuza mapadri ili waweze kujitakasa na kwenda kuwatakasa waamini na kuendeleza huduma za kichungaji Jimboni.

"Tumeamua kufanya Kongamano hili katika maeneo haya ya Jiweni Kamba mahali ambapo ndipo kiini cha ukristo jimboni Sumbawanga kwa kuwa na Kanisa la kwanza, nyumba za watawa na mapadri, kwa ufupi tumekuja huku kufanya Hija yetu na mafungo kwa sababu Kanisa linaadhimisha miaka 150 ya ukristo na 100 ya upadri, hivyo tukijua kuwa chanzo cha upadri Jimboni Sumbawanga ni maeneo haya na mapadri weupe wengi wamelala hapa, hivyo kwa neema sala na maombezi ya mama Bikira Maria msimamizi wa Jimbo letu atujalie mastahili katika utume wetu kwa Kanisa," Amesema Padri Sangu.

Jimboni Sumbawanga, Jiweni Kamba ni sehemu ambapo Kanisa la kwanza lilijengwa baada ya kusimikwa kwa mbegu ya imani zamani ikijulikana kama Jimbo la Kalema kabla ya kugawanywa kwa Jimbo Sumbawanga na Jimbo Katoliki Mpanda.

Sehemu hii yenye historia nyingi katika ukuaji wa mkoa wa Rukwa na Kanisa la Sumbawanga imependekezwa kuwa sehemu ya Hija kijimbo ili kukumbuka na kuendeleza mbegu ya imani iliyopandwa na mapadri weupe nchini Tanzania na hasa kwa Jimbo.








Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU