ASKOFU MSONGANZILA AWAKUMBUSHA WAZAZI WAJIBU WAO



Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila amewakumbusha wazazi/walezi kuhakikisha siku haipiti bila kupandikiza kitu kipya cha hekima kwa watoto wao,ili kuwaandaa wawe wazazi wazuri  kwa baadae na kuaondokana na masuala ya ukatili kwa watoto.

Askofu huyo ameyasema hayo kwenye mahojiano maalum na gazeti hili, alipokuwa akizungumzia umuhimu wa kuadhimisha siku ya mtoto wa Afrika ambayo hufanyika kila mwaka Juni 16, kwa ajili ya kuwakumbuka watoto waliouawa kikatili huko Soweto nchini Afrika Kusini na makaburu,wakidai haki yao, ambapo aliwafafanisha makaburu hao na maherode waliotaka kumuua Yesu kwa sababu ya uchu wa madaraka.

Askofu Msonganzila alisema kuwa kitendo cha kuwaua watoto hao kinafafanishwa na Herode alivyotaka watoto wote wa chini ya miaka miwili kuuawa huko Misri, baada ya Yesu kuzaliwa na akashindwa namna ya kumuua na kuamuru watoto wote wa kiume wauawe akijua kuwa hata huyo Yesu aliyekuwa amezaliwa angeweza kuwa miongoni mwa watoto hao wa chini ya miaka miwili.

Anasema kuwa kwa upande wa Kanisa Katoliki kila inapofika Desemba 28 ya kila mwaka huwa wanaadhimisha sikukuu ya  mashahidi wa Yehova ili kuwajenga  na kupata mawazo mbalimbali kutoka kwao kwa kuwa nao wanahaki ya kusikilizwa mawazo yao kuheshimiwa na kulindwa .

“Kero hizi dhidi ya watoto zinatakiwa  zisiwepo kabisa, kutowalinda watoto ili waondoke  katika manyanyaso mbalimbali, ukatili wa kijinsia, mila na desturi  kandamizi ni sawa na uuaji na uherode, jamii inatakiwa  itusaidie tuwe na dira nzuri juu ya mambo haya, ili kuwepo na nguvu ya kupambana na masuala yote ya ukatili wa watoto,” alisema Askofu huyo.

Aliongeza kuwa Taifa  lililo na watoto wasioendelezwa ni sawa na Taifa Gumba, kwani watoto ndio wanaotegemewa wachukue nafasi za viongozi waliopo madarakani,na pia ndio viongozi wa familia, Jumuiya na Taifa kwa ujumla, hivyo malezi ya watoto yasibakie kwa taasisi, bali familia kwa maana ya wazazi  wajipange kulea watoto wao na wasizilazimishe taasisi kuwalelea watoto wao, na ndio maana Kanisa lina mradi wa Gracal Machel Trust ambao unawasaidia watoto walioko nje ya mfumo wa shule kurudi shuleni ili waweze kutimiza ndoto zao.

Meneja wa Mradi wa Gracal Machel Trust (GMT) wa watoto walioko nje ya mfumo wa shule Godfrey  Wawa alisema ujio wa mradi huo utasaidia  watoto 20,000 kuanzia miaka 7-17 waliokosa elimu kwa sababu mbalimbali ikiwemo vitendo vya ukatili walivyokuwa wanafanyiwa majumbani, kuweza kurudi shuleni na kupata elimu hiyo pia kupata haki yao waliyoikosa na hatimaye kutimiza ndoto zao.

Wawa alisema katika kutekeleza mradi huo watahakikisha kila mtumishi atakayefanya kazi kwenye mradi huo, anasaini mkataba wa kuhakikisha haki za mtoto zinalindwa kuanzia kumtambua, kumuandikisha na kumlinda mtoto aendelee kubaki shuleni hadi atakapomaliza elimu yake, kwa kuwa ni haki yake ya msingi kupata elimu hata kama aliikosa hapo nyuma kwa sababu mbalimbali za kifamilia na kijamii.

Alisema kuwa pia kwa sasa wamejipanga kuanza kutoa elimu kwa  kamati za shule zote, kwa walimu wakuu na waratibu elimu kata, ili kumlinda mtoto asikimbie shule,na pia ili wajue njia bora za mkumlinda mtoto awapo  shuleni, ukizingatia kuwa hata Serikali ilishatoa michango mbalimbali mashuleni ambayo ilikuwa ni moja ya changamoto iliyomfanya mtoto huyo ashindwe kuendelea na masomo yake kutokana na hali duni ya kipato cha familia.

Akibainisha changamoto wanazokumbana nazo katika utekelzaji wa mradi huo, alisema  mila na desturi  ni changamoto sana  hasa ya ukeketaji, ambayo inamfanya mtoto kujiona mkubwa baada ya kufanyiwa ukeketaji na kuwa tayari kuolewa katika umri mdogo,watoto wengine kufichwa kwa ajili ya kutumikishwa kazi za nyumbani hasa zaidi kwa mtoto wa kike, ambapo aliwaomba wadau mbalimbali kushirikiana kwa pamoja na kuweka mikakati ya kumlinda na kumtunza mtoto wa Afrika.

Alitoa wito kwa jamii kutambua kuwa mtoto ni binadamu na ni taifa la leo na kesho na jamii inatakiwa kuwekeza kwake, kupiga vita dhidi  ya mila potofu zinazomkandamiza mtoto na umasikini, pia lazima alelewe vizuri ili aendeleze utaifa na utamaduni wa kiafrika sambamba na uzalendo kwa nchi yake.

Akizungumza na  gazeti hili  Ofisini kwake  Katibu wa Mara Alliance ambao ndio watekelezaji wa Mradi wa Mama Gracal Machel Trust na Mkurugenzi  wa kituo  cha sheria na kijamii The Legal  na social Assistance Centre (LSAC) Ostack Mligo ambaye pia ni wakili alisema kuwa hali ya ukatili kwa watoto inaonekana kupungua kwa baadhi ya maeneo kutokana na mashirika kuendelea kutoa elimu, lakini wilaya ya Tarime ni moja kati ya wilaya inayoongoza kwa matukio ya vitendo vya ukatili kwa watoto,  ambapo kwa wiki  moja zaidi ya simu 3-4 zinapigwa na wananchi mbalimbali wakieleza kutokea kwa kitendo cha ukatili ndani ya kata  au eneo fulani katika wilaya hiyo huku wilaya ya Serengeti ikiwa na matukio machache ya ukatili na hii inawezekana ni kutokana na uwepo wa mashirika mengi ya kutetea haki za watoto katika wilaya hiyo.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa kinachochangia kwa asilimia kubwa vitendo vya ukatili kwa watoto ni migogoro ndani ya ndoa pamoja na jamii kutowajibika ipaswavyo katika kutoa taarifa au kukemea hali ya vitendo vya ukatili inapotokea  harafu  mambo hayo yanabakia kama ya kawaida ndani ya jamii na kuonekana  kama ni hali ya kawaida.

Mratibu wa shirika lililoanzishwa na masisita wa Maryknolly Sisters linalofanya kazi katika Wilaya ya Butiama, Manispaa ya Musoma na Musoma vijijini katika Mkoa wa Mara la Watoto Wapinge Ukimwi (WWU) Peter Nyarufunjo alisema kuwa hali ya vitendo vya ukatili katika Mkoa wa Mara bado ni kubwa na hali hiyo inachangiwa sana na watoto kukosa malezi ya wazazi kwani wazazi wanahangaika na suala la kukuza uchumi au kipato ndani ya familia na kusahau umuhimu wa malezi bora kwa watoto wao.

“Wazazi wanaondoka asubuhi kwenda kutafuta riziki hadi jioni  ndio wanarudi ,hawapati muda wa kukaa na watoto ili wapate kujua mwenendo mzima wa makuzi ya watoto wao au kupata habari sahihi za watoto hao, hii ndio imekuwa changamoto kubwa sana,lakini sisi tumeanza kutoa elimu mashuleni kwa kushirikiana na dawati la jinsia  ili kupanua wigo mkubwa wa uelewa juu ya madhara ya  vitendo vya ukatili kwa watoto,”alisema Nyarufunjo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU