“MAKATEKISTA WATHAMINIWE” ASKOFU KYARUZI



Askofu wa Jimbo Katoliki Sumbawanga Mhashamu Damian Kyaruzi amewataka wakristo nchini kujali na kuthamini utume unaofanywa na makatekista nchini kwani una mchango mkubwa katika kukuza na kutetea imani ndani ya Kanisa.

Ameyasema hayo juma hili wakati wa maadhimisho ya misa ya kuwatuma makatekista watatu waliohitimu masomo yao kutoka katika majimbo ya Mpanda na Sumbawanga katika kituo cha malezi cha Mt. Augustino kilichopo Matai jimboni Sumbawanga.

“Makatekista ni muhimu na wanahitajika katika Kanisa ukilinganisha na uhaba wa mapadri tulionao, na ukatekista ni wito na wito lazima upaliliwe, mapadri na walei tuwathamini hawa watu ili waweze kututumikia katika mahitaji yetu ya kiroho”. Amesema Askofu Kyaruzi.

Askofu Kyaruzi amewataka makatekista kutumika kikamilifu kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake kwa kuimarisha imani za wakristo kwa kukumbuka viapo na kutenda kazi ya bwana wakisaidiana, kutiana nguvu na wenza wao ili kutekeleza wajibu huo kwa kutambua kuwa ukatekista si kazi ambayo inatumikiwa kipindi cha miaka kadhaa tu bali kwa hali yake ukatekista ni maisha, wito unaopaswa kujaliwa na kuthaminiwa  kwa thamani kubwa.

Akiwapongeza makatekista hao wahitimu mkuu wa Chuo hicho cha makatekista padri Fabian Mwiga amewaasa makatekista kuwajibika katika maeneo yao na  wasibweteke na kuonekana ni mahohehahe katika vijiji bali wafanye kazi za kimaendeleo na zaidi walei na viongozi wa vigango wawasaidie katika kufanikisha miradi itakayowezesha kutunza familia zao kwani muda mwingi wanatumika katika Kanisa.

Wakitoa shukrani zao kwa uongozi na walimu wa Chuo cha Matai, makatekista wahitimu ambao ni katekista Jastini Bilia parokia ya Mamba Jimbo Katoliki Sumbawanga, katekista Cosmas Shirinde wa parokia ya Mamba Jimbo Katoliki Mpanda na katekista Daudi Magazini  wa parokia ya Mt. Fransisko wa Asizi Jimbo Katoliki Sumbawanga, wameahidi kuwa mfano bora kwa waamini watakaowatumikia ili kukuza imani na kuzidi kumtangaza Kristo kwa watu wote.







Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU