Halmashauri ya Walei Sumbawanga waaswa kushirikiana







WAAMINI wa Jimbo Katoliki Sumbawanga wamefanya ufunguzi wa Jubilei ya miaka 50 ya kituo cha Halmashauri ya Walei na vyama vya kitume jimboni humo.

Akiongoza mamia ya waamini katika uzinduzi wa jubilei ya kituo cha walei jimboni Sumbawanga iliyofanyika hivi karibuni sambamba na sikukuu ya mashahidi wa Uganda katika Kanisa la Katandala lililo katika jengo hilo la walei, Askofu wa Jimbo Katoliki Sumbawanga  Mhashamu Damiani Kyaruzi amesema kuwa  kituo cha walei jimboni humo ni cha kwanza katika majimbo yote tangu kupandwa kwa mbegu ya imani nchini Tanzania.

Askofu Kyaruzi  amesema kuwa Kanisa lilikabidhiwa mikononi mwa walei toka Mtaguso wa pili wa Vatikani juu ya hati ya harakati za kitume, majukumu na wajibu wa walei ambapo kwa misingi hiyo walei ni mitume na wamisionari, kwa maana hiyo Kanisa ni la walei huku  makreli na watawa wakiwa ni wahudumu tu ndani ya Kanisa.

Aidha Askofu Kyaruzi amekemea tabia ya viongozi mbalimbali pamoja na walei katika Kanisa wanaopinga na kukwamisha juhudi za maendeleo zinazofanywa na vyama vya kitume katika kwa sababu mbalimbali ambapo ametoa kauli mbiu ya jubilee ya walei inayosema “Ni wajibu wetu kufundishana imani, kufundishana imani ni wajibu wetu”.

“Kwa namna zozote zile asiwepo padri yeyote, mtawa wala mlei mwenyewe anayeweza kuzuia na kuzima maendeleo na shuguli za walei katika Kanisa,” Amesema Askofu Kyaruzi.

Akieleza historia ya kuanzishwa kwa huduma za walei jimboni Sumbawanga Mkurugenzi wa walei  jimboni Padri Didas Nandi amesema kuwa kituo hicho kilianza mwaka 1967 na Mkurugenzi wa kwanza wa utume wa walei na vyama vya kitume padri Gerald Nolf kwa idhini ya Askofu wa kwanza mzalendo hayati Mhashamu Kalolo Msakila.

“Kituo kimekuwa kikitoa  huduma mbalimbali za kiroho na kimwili kwa walei kama vile ibada na misa, semina, mikutano, makongamano na sherehe mbalimbali za ndoa, kipaimara pamoja na huduma za malazi kwa walei wanaotoka maeneo mbalimbali ya Jimbo na nje.” Amesema padri Nandi.

Wakieleza changamoto mbalimbali zinazokwamisha kusonga mbele ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo za walei, Mwenyekiti wa jubilei hiyo Joachim Luis amesema kuwa ushirikiano duni wa maparoko, viongozi wa parokia na jumuiya ni moja ya sababu zinazozorotesha na kukwamisha mipango ya walei katika Jimbo.

Kamati mbalimbali zimeanzishwa jimboni humo kusaidia kufufua imani kwa waamini, kuimarisha utume wa walei jimboni, ili kusimamia maendeleo ya walei ndani ya Jimbo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jengo jipya la walei litakalokuwa na ghorofa 3 huku likikadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni nne (4), ambapo tayari ujenzi huo umekwisha kuanza.








Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU