Mariathon 2017 yavuka malengo



Uongozi wa Redio Maria Tanzania umewashukuru wadau wake wote, waliopo ndani na nje ya nchi kwa kuiwezesha redio hiyo kufikia malengo yake, kupitia Kampeni ya Mbio za Mama Maria (Mariathon 2017), kwa kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi milioni 480.

Akizungumza na Blog hii juma hili Rais wa Redio Maria Tanzania, Bw. Humphrey Kira amesema kuwa, katika Kampeni hiyo kwa mwaka 2017, waliadhimia kukusanya kiasi cha shilingi milioni 450,000, kwa kipindi cha wiki 6, japo walitambua haitakuwa kazi rahisi kutokana na hali halisi ya uchumi ilivyo.

“Hakika utume wa Uinjilishaji unaofanywa na Redio Maria Tanzania na dunia nzima ni utume wa kipekee sana, kwani mambo mengi yanayotukia yanazidi akili za kibinadamu. Redio hii inaongozwa zaidi na nguvu ya Kimaria, Marian Spirit, maana hata ukiangalia hali halisi ya uchumi wa wadau wetu siyo nzuri, lakini kwa nguvu za Mungu, malengo tuliyoyapanga yamefikiwa na kupitiliza,” amesema Kira.

Akifafanua matumizi waliyolenga kuyatekeleza kutokana na kiwango walichokuwa wamejipangia katika kampeni hiyo, Bw. Kira ameyataja kuwa ni pamoja na kulipia Masafa (50,000,000), Matumizi ya Mwezi Mei (90,000,000), Kuchangia Mfuko wa Umisionari (150,000,000) na Vifaa vya kuboresha Mitambo (160,000,000).

Aidha, Rais huyo wa Radio Maria Tanzania, kupitia Gazeti hili la Kiongozi ameendelea kutoa wito wake kwa wadau wa Radio hiyo, waelendee kutenga muda wao adimu kwa kuipenda na kusikiliza vipindi mbalimbali vinavyorushwa na Redio Maria Tanzania, ili kila mmoja aweze kushiriki jukumu la  Uinjilishaji na zaidi sana kuuchuchumilia utakatifu ambao kila mmoja anauhitaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Matangazo Redio Maria Tanzania, Padri John Maendeleo wa Shirika la Roho Mtakatifu, ameendelea kuwaalika mapadri watawa na walei mbalimbali wenye ujuzi kuitumia Radio Maria Tanzania, katika kuwalisha wasikilizaji wake Kiroho na Kimwili kwa kushiriki kuandaa vipindi na vikarushwa na radio hiyo.

“Napenda kuwaalika Mapadri, watawa wenzangu, walei na wote wenye ujuzi mtumie radio hii kuandaa vipindi ili kwa pamoja tutekeleze lile agano la Kristo la kuhubiri habari njema kwa watu wote mpaka nje ya mipaka yetu,” amesema Padri Maendeleo.

Mbio hizo za Mama Maria, Mariathon 2017 zilizinduliwa rasmi Aprili 28 mwaka huu, na kufungwa Juni 16 mwaka huu na rais wa Redio Maria Tanzania, Bw. Humphrey Julius Kira. Mbio hizo zilishirikisha Majimbo/mikoa 14 Bara na Visiwani, ambapo Jimbo Kuu Katoliki Songea ambalo Mariathon ya mwaka jana 2016 lilikuwa la mwisho, mwaka huu limeshika nafasi ya kwanza Kitaifa, likichukuwa nafasi hiyo toka kwa Jimbo Katoliki Mbeya ambalo limeshuka na kushika nafasi ya 8.

Nafasi ya Pili imechukuliwa na Jimbo Mtwara, huku Moshi likishika nafasi ya 3, Iringa(4), Mbinga(5), Arusha(6), Mpanda(7), Singida(9), Zanzibar(10), Mwanza(11), Dar es Salaam(12) na mikoa mingine imeshika nafasi ya 14. 

Kiasi hicho cha shilingi milioni 480 kilichokusanywa kwa majuma 6 kimepatikana kupitia njia zifuatazo, Money box, Vibubu, Bahasha, Michango Binafsi na Harambee mbalimbali zilizofanywa kwenye Parokia mbalimbali za majimbo tajwa hapo juu, 100200 kupitia mitandao ya air tel money, tigo pesa na m-pesa, ambapo Parokia ya Roho Mtakatifu Segerea imefanikiwa kwa mara nyingine tena kutetea nafasi yake ya kwanza kama ilivyokuwa Mariathon ya mwaka jana. 

Mbio hizi za Mama Maria huzihusisha Redio Maria zote ulimwenguni kila mwaka mwezi Mei ambao ni Mwezi wa Rosari Takatifu, na hii hufanyika kwa heshima ya Mama Bikira Maria, ikiwa na lengo la kuhamasisha uchangiaji kwa ajili ya kuendeleza Utume wa Radio Maria Tanzania na Ulimwenguni kote.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU