REDIO MARIA YASHEREHEKEA MIAKA 21 YA UINJILISHAJI MAKINI



Vyombo vya Mawasiliano vya Kanisa nchini, vimeshauriwa kuwa makini katika kuandaa na kutangaza habari zake, ili kuepuka kutoa habari ambazo zinaweza kuipotosha jamii, badala yake viandike habari za kuimarisha mahusiano mema na zenye mashiko.
Wito huo umetolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Mbeya Mhashamu Evarist Chengula (I.M.C) wakati akifungua rasmi Hija Takatifu kwa Mahujaji, wanaoshiriki Hija kuelekea Sherehe za Miaka 21 ya Redio Maria Tanzania, inayoendelea katika ukumbi wa shule ya Sekondari ya wasichana Loleza Mkoani Mbeya.
Askofu Chengula amesema kuwa suala la kutangaza Habari kwa njia ya vyombo mbalimbali ni hamu ya Kristo mwenyewe, kutawanya habari zake katika ulimwengu wote, jambo ambalo hata wakristo wa kwanza walifanya kazi hiyo ya kupeleka habari njema katika nyakati zao.
Amesema kuwa Redio Maria Tanzania ilianzishwa hapa nchini kutokana na msukumo uliotolewa kwenye Sinodi ya kwanza ya Afrika yenye kuhamasisha utangazaji wa habari njema kwa njia ya vyombo vya habari katika nchi za Afrika na ulimwengu mzima.
Aidha Askofu Chengula amewataka wakristo, marafiki na wadau wa Redio Maria Tanzania, kumshukuru Mungu na kufurahi kwa pamoja katika kufanya sherehe za miaka 21, tangu kuanzishwa kwa Redio hiyo na kwamba uwepo wake umedhihirisha kweli Sauti ya Kristo katika jamii, pamoja na makundi mbalimbali ya wahitaji kwa kuwapatia Habari njema.
Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Matangazo Redio Maria Tanzania Padri John Maendeleo, CSSp, amebainisha kuwa wadau wa Redio hiyo hapa nchini, waendelee kujitoa kwa hali na mali katika kuhakikisha wanashiriki katika uendeshaji wa chombo hicho ili Injili inayohubiriwa mahali hapo iwafikie walio wengi zaidi huku akiwaalika kushiriki maadhimisho ya miaka 21 tangu kuanzishwa kwa Redio hiyo hapa nchini.
Hija hiyo iliyoanza Juni 27 mwaka huu itamalizika Julai 2, imewashirikisha mahujaji wapatao 150, kutoka katika Majimbo ya Singida, Mpanda, Zanzibar, Mtwara, Iringa, Ifakara, Mbinga, Moshi, Jimbo Kuu Katoliki Arusha, Mwanza, Songea, Dar es Salaam na wenyeji Jimbo katoliki Mbeya.
Mahujaji hao wamepata nafasi ya kushiriki semina mbalimbali kutoka kwa mapadri ambapo Padri Cyrilo Mwalyolyo ambaye ni Mkurugenzi wa Walei Jimbo Katoliki Mbeya, ametoa mada inayohusu Nafasi ya Mlei katika Kanisa, padri Lucas Wakuganda, akatoa mada inayohusu Mkristo na Visakramenti huku padri Frank Mnyema akatoa mada ya Mkristo na Ushirikina na padri Thelesphory Mtweve akatoa Mada ya Mkristo na Uchumi.
Mbali ya kufunga na Kusali, Mahujaji hao wamepata nafasi ya kutembelea maeneo ya Hija ikiwa ni pamoja na kupanda Mlima Loleza, kwenye Kimondo huko Mbozi na Daraja la Mungu huko Kiwira.
Kilele cha Maadhimisho ya Miaka 21 ya Uinjilishaji wa Radio Maria Tanzania, kinatarajiwa kufanyika Julai 2 mwaka huu, katika Kanisa Kuu la Kiaskofu la Mtakatifu Anthoni Padua, lililopo Mbeya Mjini ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mstaafu Bw. Mizengo Kayanza Peter Pinda.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU