Mwezi Juni ni wa heshima kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu (2)



HAPO ndipo Bwana wetu Yesu Kristo alipomwambia Mtakatifu Margareta Maria Alakoki kuwa ataiweka siku maalum ya kufanya malipizi ya pekee kwa kufidia madharau na mabaya mengine yote yaliyokuwa yametendwa dhidi yake. Siku hiyo ndio ile Ijumaa ya kwanza inayofuata, baada ya sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo kama ilivyokwisha kudokezwa hapo awali.
Ibada ya heshima kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu inaidhinishwa rasmi na Papa: Baada ya kifo cha Margareta Maria Alakoki hapo tarehe ya 17 ya mwezi wa Oktoba, mwaka wa 1690, Mashirika ya Kitawa tu ndiyo yaliyokuwa yameruhusiwa na Roma kuadhimisha misa maalum kwa heshima ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Lakini kuanzia mwaka 1856 Baba Mtakatifu Pius wa 1X aliliruhusu Kanisa Katoliki kwa jumla wake popote ulimwenguni kuwa na adhimisho la Misa Maalum kwa heshima ya Moyo Mtakatifu wa Yesu.
Baba Mtakatifu Pius wa X aliamuru ile ibada ya kuuweka wakfu ulimwengu wote kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu iliyofanywa kwanza na Papa Leo wa X111  irudiwe kila mwaka. Baba Mtakatifu Pius wa X1 katika Waraka wake wa Kipapa wa tarehe ya 8 ya mwezi wa Mei, mwaka wa 1928 “Miserentissimus Redemptor”-Mwokozi aliyejaa huruma- alikiri kuwa ni kweli Bwana wetu Yesu Kristo alikuwa amejidhihirisha mwenyewe alipomtokea Margareta Maria Alakoki na kutoa ahadi za neema kwa wale watakaouheshimu moyo wake.
Waraka huo wa Baba Mtakatifu  Pius wa X1 ulikuwa unarudia tena na tena yale mazungumzo kati ya Bwana wetu Yesu Kristo na Mtakatifu Margareta Maria Alakoki yakithibitisha umuhimu wa kuuheshimu Moyo huo wa Bwana wetu Yesu Kristo kwa fidia ya dhambi zetu.
Siku ya kumbukumbu ya miaka 100 ya kuanzishwa kwa sherehe ya Moyo Mtakatifu wa Yesu iliyozinduliwa na Baba Mtakatifu Pius wa 1X, Baba Mtakatifu Pius wa X11, aliwaeleza waamini Wakatoliki wote kwa kinaganaga sana, katika Waraka wake wa Kipapa “Haurietis aquas” wa mwezi Mei, mwaka wa 1956 umhimu wa ibada hii ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. 
     Baba Mtakatifu Benedikti wa XVI alimpelekea barua ya pongezi Padri Kolvenbach, Mkuu wa Majesuiti, kwa kumbukumbu ya miaka 50 tangu ulipotolewa ule Waraka wa Kipapa “Haurietis aquas” na Baba Mtakatifu Pius wa IX. Baba Mtakatifu Benedikti wa XVI alikuwa ameongelea, katika barua ile ya pongezi, kwa marefu na mapana, umuhimu wa kuwa na ibada hii ya Moyo Mtakatifu wa Yesu.
     Mwanzo wa Ibada ya Moyo Mtaktifu wa Yesu na kuenea kwake: Ingawa dalili ya ibada hii ya Moyo Mtakatifu wa Yesu ilianza kuonekana kuanzia kwenye karne ya  kumi na moja na kumi na mbili kule Bara la Ulaya,  hapa nchini kwetu Tanzania iliingia kwenye kati ya mwaka 1917 na mwaka 1919. Ibada ya Moyo Mtakatifu wa Yesu ilianza na utoaji wa heshima kwa Madonda Matakatifu ya Bwana wetu Yesu Kristo na hasa utoaji wa heshima kwa lile Donda lake la ubavuni.
Mtakatifu Bernardo wa Klervo (1090-1153) anaonekana kujitokeza mara nyingi zaidi katika hizo karne za mwanzo wa hiyo ibada. Hata hivyo inaonekana ni mashirika ya nyumba za kitawa tu yaliyoanza kujitokeza sana katika uzingatiaji wa ibada hii. Mashirika yaliyokuwa yamejitokeza zaidi ni yale ya Kifransiskani, Kidominikani, Kijesuiti na ya Kibenediktini.
     Aliyekuwa wa kwanza kabisa kuweka msingi wa kiteolojia wa ibada hii alikuwa  mtawa mmoja wa shirika la Kijesuiti aliyeitwa Kasper Druzbicki (1590-1662). Kasper Druzbicki, katika kitabu chake “Meta Cordium- Cor Jesu” yaani, “lengo la mioyo yetu ni Moyo wa Yesu,” ndimo kulikokuwa msingi wa Kiteolojia wa ibada hii ya Moyo Mtakatifu wa Yesu.
Muda mfupi baada ya Kasper, alijitokeza Jean Eudes aliyetunga hata sala za ibada kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu na akapendekeza kuwe na sikukuu maalum kwa ibada hiyo. Jean Eudes alikuwa pia shabiki sana wa heshima kwa Moyo safi wa Bikira Maria.
Jinsi muda ulivyozidi kupita mgawanyo wa heshima zake kwa mioyo hii miwili ilizidi kuwa wazi zaidi na ilipofika tarehe ya 31 ya mwezi Agosti mwaka 1670 uamuzi wa kuwa na sherehe mbili tofauti ulikuwa umefikiwa na kulianzishwa rasmi sikukuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu.
     Hata kabla ya kujitokeza Mtakatifu Margareta Maria Alakoki (1647-1690) ambaye Bwana wetu Yesu Kristo alikuwa ameamua kumtumia zaidi katika kuendeleza ibada ya heshima kwa moyo wake, kulikuwa na watakatifu wengine kadhaa pamoja na Wenyeheri ambao pia walihusika kwa namna moja au nyingine katika kuikuza ibada hii hasa kwa kujihusisha wenyewe katika kuizingatia.
Baadhi ya watakatifu na Wenyeheri hao ni kama Mtakatifu Lutgarda(1298); Mtakatifu Mektilda(1298); Mtakatifu Getruda(1301); Mwenyeheri Maria wa Moyo Mtakatifu (1863-1899); Mwenyeheri Estelle Faguetta (ca1840) na wengine.
     Baada ya uchunguzi wa Kanisa Katoliki kwa muda wa kutosha kama ilivyo kawaida yake, ibada hii ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, iliidhimishwa rasmi kama ilivyokwisha kudokezwa hapo awali na ikaendelea kuenea katika nchi mbalimbali  Tanzania ikiwa moja ya nchi hizo.
     Kuanzia kwenye miaka ya 1850 hivi, vikundi vya waamini, mashirika ya kidini na hata majimbo ya nchi yamejitoa wakfu kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu. Mwaka 1873 nchi ya Ecuador, ilikuwa nchi ya kwanza ulimwenguni kujitolea wakfu kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu.
   Ahadi kwa wenye mazoea ya kuwa na ibada ya Moyo Mtakatifu wa Yesu: Kuna ahadi lukuki zilizotolewa na Bwana wetu Yesu Kristo kwa wale watakaokuwa na mazoea ya kufanya ibada kwa heshima ya Moyo Mtakatifu wa Yesu. Ahadi  alizozitoa kupitia kwa Mtakatifu Margareta Maria Alakoki zilikuwa kumi na mbili na ziliorodheshwa na kupangwa katika jedwali hapo mwaka 1863.
Mwaka 1882 alitokea mfanyabiashara mmoja wa taifa la Kimarekani aliyegharamia kuzitasfiri na kuziandika ahadi zile zote katika lugha 238 na zikasambazwa ulimwenguni kote.
Mwadhama Adolph Kadinali Perrand hakupendezwa na kile kitendo cha usambazaji wa ahadi hizo katika zile lugha kwa sababu baadhi ya ahadi zilikuwa na maneno ambayo yalileta maana tofauti na alivyotaka kueleza Mtakatifu Margareta Maria Alakoki. Mwadhama Adolph Kadinali Perrand akaagiza ahadi zichapwe kwa kutumia maneno yale yale ya asili aliyoyatumia mwenyewe Mtakatifu Margareta Maria Alakoki.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU