Vyanzo vya hukumu za kesi za ukatili wa watoto kuchelewa vyabainishwa

n Na James Stanley, Moshi
TATIZO la jamii kushindwa kutoa ushahidi kwenye kesi zinazohusu ukatili dhidi ya watoto na wanawake ni kichocheo cha kutosikilizwa ama kuchelewa kwa kesi hizo na watuhumiwa kutochukuliwa hatua za kisheria.
Hayo yamesemwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Bernad Mpepo wakati wa kikao na watetezi wa haki za binadamu kilichoandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la kutetea haki za binadamu na jinsia mkoa wa Kilimanjaro (KWIECO).
Amesema kesi nyingi zinachukua muda mrefu na nyingine kufutwa kutokana na kukosekana kwa ushahidi jambo linalowanyima haki waathirika wa ukatili huo.
Awali akitoa taarifa kwa wadau wa haki za binadamu wakiwemo polisi, wanasheria, maofisa ustawi wa jamii na wataalamu wa sheria toka nchini Kanada, Mkurugenzi wa Kwieco, Elizabeth Minde amekosoa Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971.
Minde ameiomba Serikali kufanya marekebisho ya sheria zinazochangia kuongeza matukio ya kikatili ikiwemo sheria hiyo  na sheria nyingine kandamizi pamoja na kuwawezesha kitaalamu waendesha mashtaka na maofisa ustawi wa jamii ili kurahisisha utendaji na upatikanaji wa haki kwa waathirika wa ukatili nchini.
Amesema Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 inamtambua mtu mwenye umri kuanzia miaka 14 kuwa anaweza kuolewa jambo ambalo linakinzana na Katiba ya Tanzania inayomtambua mtu mzima kuwa ni kuanzia miaka 18.
Minde amesema umri wa miaka 14 umebainika kuwa na changamoto kubwa kwa wasichana wanaoolewa na wengine kuozeshwa bila ridhaa yao kwa lengo la wazazi wa msichana kupata mali kutoka upande wa muoaji wakati kwa umri huo wasichana wengi bado hawajapevuka vizuri kuweza kutumikia majukumu ya ndoa.

Naye mwanaharakati wa haki za binadamu kutoka shirika la NAFGEM, Francis Selasini amesema ipo haja kwa mahakimu kupewa mafunzo maalumu ya taratibu za kisheria hasa katika kesi zinazohusiana na haki kwa wanawake na watoto, madaktari na wauguzi  pamoja na maafisa ustawi wa jamii wanaohudumia watoto na wanawake ambao wamekuwa wakifanyiwa vitendo mbalimbali vya kikatili.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU