ZINGATIENI MAADILI YA UPADRI-ASKOFU RUWA’ICHI




ASKOFU mkuu wa Jimbo Kuu katoliki Mwanza Mhashamu Jude Thadeus Ruwa’ichi  amewakumbusha  mapadri kuepuka  kuweka ubunifu usiokuwa na tija katika uinjilishaji bali ni lazima wafuate maadili ya upadri na misingi ya kanisa  bila kuchoka.
Amewataka wajue kuwa huo ni utume na kwamba wametengwa kwa ajili ya kazi hiyo na sio kazi nyingine.
Ameyaweka hayo bayana katika misa takatifu ya kuazimisha uzinduzi wa Jubilei ya miaka 100 ya upadri Tanzania Bara katika Jimbo kuu katoliki Mwanza iliyofanyika katika parokia ya Sumve jijini Mwanza na kuhudhuriwa na mapadri kutoka parokia zote.
Pia Askofu Ruwa’ichi  amewahimiza mapadri kuwa kazi ya upadri ni wito na Mungu amewatumia wao kueneza injili ulimwenguni kama alivyowatuma mitume kumi na wawili kutoka katika watu dhaifu ambao ni binadamu ili kwenda ulimwenguni kueneza injili na wawe chombo cha uamsho.
Askofu Ruwa’ichi pia amewasihi mapadri kuzidi kumwomba Mungu awape neema na ubunifu bora ili wafanye kazi yao kwa amani ya Mungu, wajitahidi kutafakari juu ya mapana na marefu katika ufanyaji kazi hiyo na wapate kuwa makuhani wa Mungu ili wazishinde changamoto za nguvu za shetani maana “mavuno ni mengi lakini watenda kazi ni wachache”.
Pamoja na hayo Askofu Mkuu Ruwa’ichi amewapongeza mapadri wa kwanza kuinjilisha Tanzania Bara kuwa walitenda kazi bila hofu na walikuwa mstari wa mbele kueneza injili wakati wowote bila kuchoka kupitia utume huo huku akihimiza waamini wote wasafiri pamoja kama familia ya Mungu ili  mwaka wa mapadri ukubalike.
Amewashukuru wana Sumve na mapadri kwa utayari wa tukio hilo huku akiwasisitizia kusafiri pamoja kwa mshikamano wa pekee ndani ya jimbo kuu katoliki Mwanza, katika tafakari, sala na kulea miito ya upadri kwa Taifa lote la Mungu.

Na Maria Emmanuel, Mwanza






Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU