Majaliwa: Hatutawavumilia waajiri wasiotoa mikataba

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali haitawavumilia waajiri ambao hawatoi mikataba ya ajira kwa wafanyakazi wao na amewaonya waache tabia hiyo mara moja.

Ametoa agizo hilo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Sita wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) katika ukumbi wa Mwalimu Julius K. Nyerere ulioko Chuo cha Mipango, nje kidogo ya mji wa Dodoma.

“Nitoe wito kwa waajiri wote ambao wamekuwa na tabia ya kutokutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi wao, waache tabia hiyo mara moja, kwani Serikali haitamvumilia mwajiri wa namna hii,” ameonya.

Akijibu hoja ya waajiri kutokutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi ambayo iliibuliwa kwenye risala yao, Waziri Mkuu amesema kifungu cha 14 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya mwaka 2004  kinaelekeza aina mbalimbali za mikataba inayotakiwa kutumika kuajiri wafanyakazi.

“Kisheria mwajiri anao wajibu wa kuhakikisha kila mtumishi wake ana mkataba wa kazi kwa maandishi. Pia ninawaagiza maafisa wa kazi wanaohusika na kaguzi za kazi kote nchini, wahakikishe kila mwajiri anafikiwa wakati wa ukaguzi na hatua stahiki zinachukuliwa kwa wote wasiotekeleza matakwa ya Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini,” amesisitiza.

Akijibu hoja kuhusu wafanyakazi kuwekwa ndani kiholela, kunyanyaswa, kushushwa vyeo na kusimamishwa kazi na wanasiasa, Waziri Mkuu amesema Serikali chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe Magufuli itaendelea kuzingatia utawala wa sheria na kanuni za utawala bora ili kuhakikisha kuwa haki za wafanyakazi zinalindwa ipasavyo.


Kimsingi watumishi wanasimamiwa na mamlaka za kinidhamu na sheria mbalimbali ambazo hazina budi kuangaliwa kwa pamoja kabla ya kuchukua hatua. Ninawaagiza viongozi wenzagu wa kisiasa na walioko katika wizara na taasisi zote za Serikali, mikoani, wilayani, kwenye idara za Serikali na Halmashauri wazingatie utawala wa sheria wakati wa kushughulikia masuala mbalimbali yanayohusu wajibu na haki za wafanyakazi,” amesema huku akishangiliwa.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU