Papa hajaruhusu talaka - Ask.Niwemugizi


Ametoa tu mwongozo wa kuendesha kesi  za ndoa zisizo halali

ASKOFU wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara Mhashamu Severine-Niwemugizi ameeleza kuwa, Kanisa Katoliki haliwezi kuruhusu talaka wala kuvunja ndoa yoyoye halali.
Akofu Niwemugizi ambaye ni mtaalamu wa Sheria za Kanisa (Canon law) ameyasema hayo hivi karibuni wakati akizungumza na gazeti Kiongozi kuhusu utaratibu mpya Papa Fransisko alioutoa kuhusu kuendesha kesi za ndoa ya Kanisa Katoliki.
“Papa Fransisko ambaye ndiye kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani pamoja na mamlaka aliyonayo hawezi kamwe kuruhusu talaka wala kutoa shauri la kuvunja ndoa halali kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na Maandiko Matakatifu yanayosema, “Aliyoyaunganisha Mungu mwanadamu asitenganishe,” ameeleza Askofu Niwemugizi huku akifafanua zaidi kuwa;
“Jamii imepokea kwa hisia tofauti matamko mbalimbali ya Papa Fransisko kuhusu ndoa. Wengi wametaka kumtafsiri Papa kwa kutoa majibu wanayotaka kuyasikia lakini siyo maana halisi ya Papa. Lengo lake si kutoa talaka.
Papa ametoa mwongozo mpya wa namna ya kuendesha kesi za ndoa ambazo zilifungwa kinyume na taratibu za Kanisa Katoliki na hizo ndizo mahaka za Kanisa Katoliki zinazishughulikia ili kuzitambua rasmi kwamba zilikuwa si halali.
Kanisa halivunji ndoa kamwe bali linaangalia uhalali wa ndoa ilivyofungwa. Hatuwezi kuibadilisha Biblia kwa kutenganisha watu waliounganishwa na Mungu licha ya changamoto walizonazo.”

Vizuizi vya ndoa
Akizungumzia juu ya ndoa kuwa halali, Askofu Niwemugizi amefafanua kuwa, Kanisa lina taratibu na miongozo ya ndoa.
 Sheria za Kanisa can 1083-1125 zinaeleza utaratibu, uhiari na vizuizi vya ndoa. Huko kuna ufafanuzi juu ya vizuizi 12 vya kufunga ndoa.
Baadhi ya vizuizi hivyo ni  umri wa kufunga ndoa, mtu kulazimishwa kufunga ndoa, kukosea mchumba ikiwa na maana kuwa, mtu anataka kufunga ndoa na mchumba wake anayempenda lakini analetewa mwingine aidha kwa matakwa ya wazazi, jamii nk. ama mapacha wanaofanana nk.
Udanganyifu, pengine mwenzake alikuwa ameshafunga ndoa na mtu mwingine nk. Ndoa kati ya muumuni mkatoliki na muumini wa dhehebu lingine.
“Hapa nieleweke kuwa, kila dini ama dhehebu lina utaratibu wake wa ndoa. Taratibu za Kanisa Katoliki zinamuelekeza muumini wa Kanisa Katoliki anayetaka kufunga ndoa na muislamu, mluteri ama dhehebu lingine kupata kibali kutoka kwa askofu wake wa jimbo ili kwenda kufunga ndoa kwenye dini ama dhehebu lingine nje ya Kanisa Katoliki. Asipofanya hivyo akaenda kufunga ndoa huko bila kibali ama ruhusa ya Kanisa hiyo ndoa inatambuliwa kuwa si halali.”
Kizuizi kingine ni kufunga ndoa na mtu wa karibu wa mwenzi wa ndoa. Ikitokea wanandoa wawili mmoja akaenda mbali na mwenzake huku nyuma mwenzake akaamua kufunga ndoa na ndugu wa mume ama mke wake, hiyo ndoa haikufungwa kwa uhalali.
Kufunga ndoa kwa masharti. Mfano mtu anafunga ndoa ili waishi wawili tu hataki watoto. Ama wanaoana tu ili wapate watoto. Wasipopata kinakuwa chanzo cha migogoro. Hivyo Kanisa halitambui ndoa ya masharti.

Askofu Niwemugizi ameeleza kuwa, Baba Mtakatifu hawezi kukiuka sheria za ndoa na kama akitaka lazima abadilishe sheria zote za ndoa, miongozo na taratibu zake suala ambalo si jepesi kwani Kanisa lina taratibu zake. Hata hivyo Papa hawezi kuruhusu talaka.

Kutengua ndoa isiyo halali
Askofu Niwemugizi amelezea pia mchakato wa mahakama za Kanisa kutangaza ndoa kuwa si halali.

Amesema kuwa, wale wenye migogoro ya ndoa kulingana na vizuizi 12 vya kufunga ndoa kama ilivyoelezwa awali wanapaswa kutoa taarifa kwenye mahakama za ndoa ya Kanisa Katoliki.
Mahakama hiyo itashughulikia suala hilo kwa vigezo na shahidi mbalimbali kulingana na kanuni za Kanisa. Wakijiridhisha na kuona kuwa ndoa ilifungwa kinyume na taratibu, watatangaza kuwa ndoa haikuwepo.

Baada ya kutangaza, kama walikuwa wanamiliki mali, wamepata watoto, mahakama hiyo ya Kanisa inawaelekeza kwenye mahakama ya kiraia ili waweze kuachanishwa na kusaidiwa namna ya kugawa mali na kutunza watoto ili wapate haki zao.

Hata hivyo amekubali utaratibu uliotolewa na Baba Mtakatifu wa namna ya kuendesha kesi za ndoa akisema ni utaratibu unaoeleweka utakaosaidia kurahisisha mchakato mzima wa kesi za ndoa.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU