“VUNJENI USIRI MMALIZE MIMBA ZA UTOTONI” ASKOFU MKUDE




Mhashamu Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro amekemea tabia za baadhi ya wazazi wanaowaficha watu wanaowapa mimba mabinti zao kwa kupewa fedha kidogo au vitu mbalimbali ili wasifikishwe kwenye mkono wa sheria na kuchukuliwa hatua stahiki.
Hayo amesema hivi karibuni kwenye mahubiri yake alipokuwa akitoa Sakramenti ya kipaimara kwa vijana zaidi ya 200 katika parokia ya Watakatifu Mashahidi wa Uganda iliyopo  Kidodi mkoani Morogoro.

Askofu Mkude amesema mwamko mdogo wa wazazi kulimaliza tatizo hilo ndio chanzo kikuu cha ongezeko la mimba za utotoni ambalo linaweza kutatulika endapo wazazi na walezi watatoa ushirikiano kwa taasisi mbalimbali ambazo zipo katika mapambano.

“wazazi mmekuwa mstari wa mbele kukatisha ndoto za watoto wenu kwa kutotoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria hasa pale unapogundua binti yako ana ujauzito na mhusika anajulikana, unakubali upewe fedha kidogo au nafaka kama debe la mahindi au mpunga  ili myamalize kifamilia bila kujua unatengeneza mabinti wasiosoma na watoto waishio katika mazingira hatarishi,” amesema Askofu Mkude.

Amesema Taasisi mbalimbali zimejitolea kupambana na mimba za utotoni ili watoto wa kike wafikie malengo yao kwa kusoma lakini inapotokea binti kapata mimba iwe kwa kubakwa au kwa njia nyingine, aliyempa mimba akija na mali kidogo ukweli hupindishwa na wengine huwatisha mabinti ili wapindishe ukweli bila kuangalia upande wa pili.

Askofu Mkude  amesema waathirika wanapohojiwa wamekuwa wakikiri kuwa wazazi wamehusika kwa njia moja au nyingine kwa mtu aliyewapa mimba kutokuchukuliwa hatua stahiki za kisheria na kuendelea kuwaharibu wengine matokeo yake ni ongezeko la mabinti wasiosoma na ongezeko la watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

“viongozi wa dini, taasisi mbalimbali na serikali zinatoa elimu dhidi ya mimba za utotoni pia kutambua haki za watoto ikiwemo kulindwa na kupata elimu bora, hivyo wazazi acheni kuwaficha wanaokatiza ndoto za watoto wetu wa kike kwa vitu ambavyo unapewa unatumia na havikufikishi popote wakati ukiwa mtetezi wa binti na akapata elimu huoni kama atakuwa msaada mkubwa kwa familia na jamii pia?,” amehoji Askofu Mkude.

Amesema takwimu zinaonyesha mimba badala ya kupungua  zinaongezeka na kusema umefika wakati wazazi na walezi kuwalinda watoto na kuacha kuhadaika na hivi vitu wanavyopewa ili kuwaficha waharibifu halafu wanakuja kulalamika baadaye binti hapati elimu tena, mtoto aliyemzaa hana matunzo, hamna uwezo wa kumtunza.
Pia amesema wazazi wakitumia vyema elimu wanayopewa na taasisi mbalimbali zinazopiga vita mimba za utotoni ni rahisi wao kukaa na watoto wao kuyarudia yale waliyoambiwa na elimu kuendelea kutolewa shuleni na nyumbani hivyo hata watoto itakuwa ngumu kushawishika na watu hao pia kuwaepusha na magonjwa ya maambukizi.
Tatizo la mimba za utotoni limekuwa likiongezeka siku hadi siku huku chanzo kikubwa kikitajwa ni wazazi na walezi ambao wamekuwa wakiwaficha wanaowapa mimba kwa kupokea fedha, nafaka ili wayamalize kifamilia au kutokuwataja kabisa wanapofika kwenye vyombo vya sheria na kusababisha kuwepo kwa mabinti wasiosoma pia kuongezeka watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi.

 Na Josephine Burton, Morogoro.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU