WAWATA WAASWA KUJITOA KWA HALI NA MALI




CHAMA cha kitume cha wakina mama  wa Kanisa Katoliki Tanzania(WAWATA) kimetakiwa kuwa mfano wa kuigwa katika uinjilishaji kwa kujitoa kwa hali na mali na kuwafikia waamini wengi zaidi.
Akizungumza katika tamasha  lililoandaliwa na WAWATA dekania ya Ubungo na kufanyika katika Parokia ya Mtakatifu Gaudence Makoka jijini Dar-es-salaam, Mwenyekiti wa WAWATA dekania ya Ubungo Bi.Judith Mndolwa amewataka WAWATA popote walipo katika parokia, kanda, dekania na jumuiya kuacha kuwa watu wa matukio pekee kwa kuhudhuria matamasha na kusahau wajibu wao.
Ameongeza kuwa WAWATA wanapaswa kukutana mara kwa mara, kushauriana, kujitoa kwa wahitaji na pia wawe na moyo wa msamaha.
Pia amebainisha kuwa ni jukumu la WAWATA kuhakikisha kuwa vijana wa kike kuanzia miaka 14-18 wanaandaliwa kuwa mbadala katika utume hapo baadaye.
Katika tamasha hilo WAWATA walikuwa wakisherekea mwaka Mtakatifu wa huruma ya Mungu na kumuenzi somo wao ambaye ni mama Bikira Maria na Mgeni rasmi katika tamasha hilo alikuwa Padri Sahayaraj Michael CMF Paroko wa Parokia ya Kimara. Wageni wengine waliohudhuria ni pamoja na mapadri Evarist Tarimoi, Padri John Slinger wa Parokia ya Tandale pamoja na watawa.
Kwa upande wake Padri Sahayaraj Michael katika mahubiri wakati wa ibada ya misa takatifu  katika tamasha hilo amewataka WAWATA kuwa na utii, utulivu na upole kwa maana mwanamke mtulivu  ni tunu ya Bwana (Yb Sira 26;13-14) na pia amewataka wajue wajibu wao katika familia na wasisahau familia zao kwa ajili ya Malimwengu (Petro 3;1-4).
Kuhusu changamoto ya fedha inayowakabili WAWATA, mgeni rasmi amewashauri kujitoa wao kwa wao kulingana na kazi zao kwani kufanya hivyo kutawafanya wafikie malengo.
Kutokana na ushauri mzuri wa mgeni rasmi Padri Sahayaraj Michael CMF harambee ilifanyika kwa ajili ya kutunisha mfuko wa WAWATA dekania, hivyo zikapatikana fedha tasilimu shilingi 345,550, ahadi za WAWATA parokia 13 shilingi 3,900,000 na wageni waalikwa mbalimbali na watu binafsi ahadi shilingi 1,465000 na kufanya jumla ya fedha tasilimu kuwa 955,750, ahadi 5,365,000 na jumla kuu shilingi 6,320,750.
Pia WAWATA wamefanya matendo ya huruma kwa chama cha kitume  cha Vicent wa Paulo kwa ajili ya wahitaji  mbalimbali Parokia ya Makoka ambapo wametoa mchele kilo 100, maharage kilo 100, sukari kilo 100, chumvi kilo 50 na sabuni za kufulia na kuogea vyote vikiwa na thamani ya shillingi 660,000.

Philipo Josephat, Dsm









Comments

  1. inapendeza sana akina mama kujitokeza katika kumtumikia Mungu, Kwani inatia moyo hata katika kizazi hiki ambacho hakimjui Mungu. mama akiwa mtumishi mzuri wa Mungu basi hata mtoto atafuata malezi mazuri ya mama! kwa upendo wa kristo tunamtumikia na kuwajibika!

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU