“iishini imani katoliki” Askofu Mkuu Paulo Ruzoka

Askofu Mkuu Paulo Ruzoka wa Jimbo kuu katoliki Tabora amewaasa waamini wote kuishi Imani katoliki katika kuwajali watu wenye shida mbalimbali katika jamii ili kuendelea kuuenzi mwaka wa huruma ya Mungu katika maisha yao.
Kauli hiyo ameitoa katika eneo la mlima wa Maongozi ya Huruma ya Mungu Ifucha katika parokia ya Ipuli Jimboni Tabora wakati wa kuhitimisha mwaka wa huruma ya Mungu kijimbo.
Kabla ya adhimisho la Misa Takatifu Askofu Mkuu Paulo Ruzoka, mapadri, watawa na waamini walipanda mlimani na kubariki msalaba mtakatifu ambao unaashiria uwepo wa huruma ya Mungu kupitia Kristo Yesu aliye uso wa huruma ya Mungu kwa wanadamu wote.
Mara baada ya Kubariki msalaba mtakatifu, Misa Takatifu iliadhimishwa na mahubiri yake yakalenga uzinduzi wa kituo hicho cha Hija kuwa waamini wote wanaalikwa kufika eneo hilo ili kusali, kutafakari maisha yao ili kuwa tayari kumrudia Mungu na kupata utulivu ndani ya nafsi zao.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka amesema dunia ya leo na watu wa leo wanakosa amani na utulivu wa roho matokeo yake ni hasira mioyoni mwa wanadamu hivyo ni vema waamini wakafika eneo hilo na kusali ili wapate utulivu au wapoze roho zao na ndiyo maana halisi ya neno IFUCHA NG'HOLO tuliza roho au poza roho.
Akitoa mahubiri yake wakati wa Misa Takatifu , Askofu Mkuu amesema kanisa mama au mzazi anayesaidia waamini kuitwa watoto wa Mungu kupitia sakrament za kanisa, hivyo waamini wapokee sakramenti kwa moyo wa imani na uchaji ili ziwasaidie katika safari yao ya kumwendea Mungu.
Sambamba na hilo Askofu Mkuu amewakumbusha mapadri wote kuwa makini wanapoadhimisha sakramenti hizo hasa sakramenti ya Kitubio ambayo kwayo waamini wanapokea huruma ya Mungu anayechukua mizigo yao kwa upole na unyenyekevu.
Katika sherehe ya kuhitimisha mwaka wa Huruma Mungu Kijimbo, pia sherehe ya familia ya Mungu kwa wanajimbo ilifanyika ambapo waamini walichangia fedha na vitu ili kusaidia gharama mbalimbali za uendeshaji wa ofisi ya Askofu.
Katika adhimisho hilo la Misa Takatifu pia wageni mbalimbali walialikwa wakiwemo viongozi wa serikali, viongozi na waamini wa dini na madhehebu mbalimbali toka mkoani Tabora na wenyeji wa eneo hilo la kijiji.
Matarajio ni kuwa kila mwaka tarehe na mwezi huo waamini wote wa Jimbo kuu Tabora watakuwa wakienda hija katika eneo hiloEneo hilo ambalo limewekwa chini ya usimamizi wa watakatifu Yohana Paulo wa pili na Terezia wa Calcata.

Naye Mkuu wa wilaya ya Tabora Manispaa Mwl Queen Mlozi akiongea kwa niaba ya Serikali amesema hitimisho la mwaka huu wa huruma lisaidie wananchi kuacha vitendo viovu hasa mauaji yanayoiweka Tabora kuwa kinara kwa mauaji ya walemavu wa ngozi albino, wazee na vikongwe kwa imani za kishirikina.
Pia amewahimiza wana Tabora wajiepushe na matukio ya ujambazi, mimba za utotoni kwa watoto wa kike na kuwapa nafasi sawa ya kusoma kama ile ya watoto wa kiume na kuwataka wazazi kuwaruhusu watoto wa kike kupewa nafasi ya kuvaa kile alichokiita magauni manne kwa utaratibu wa serikali.
Mkuu wa huyo wa Wilaya amewaomba wana Tabora kujipanga ili kunufaika na ujio wa barabara za lami, huduma bora za reli, ujio wa ndege za serikali, na uhamiaji wa makao makuu ya serikali Dodoma vyote vimsaidie mwana Tabora kuboresha maisha yake, kutoka alipo na kwenda mbele.

Pia amethibitisha kwamba serikali ya Tanzania inatambua michango ya afya, elimu, maji na huduma zote za jamii zinazotolewa na kanisa na kwamba serikali ipo tayari kutoa ushirikiano utakaohitajika.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU