“Utandawazi uwe na kiasi” Ask. Msonganzila

Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila amewakumbusha watawa na mapadri kuweka mipaka ya dhati kati yao na  Mungu, na kuacha kutumia muda mwingi katika utandawazi huku kiapo chao kikiwa ni uaminifu, unyeyenyekevu na kuwa na maisha ya sala.

Askofu Msonganzila ameyasema hayo wakati wa ibada ya kufunga lango la Huruma iliyofanyika katika Kanisa la Kiabakari ambapo mahujaji  kutoka sehemu mbalimbali wamefika kanisani hapo, kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa mambo mengi aliyowatendea katika kipindi chote cha kuadhimisha ibada Takatifu ya Huruma ya Mungu.

Askofu Msonganzila amesema utandawazi unaonekana kuwachukulia muda mwingi baadhi ya mapadri na watawa hadi kusababisha muda wa maisha ya sala  ya kila siku kupungua kutokana na kutumia muda mwingi katika utandawazi ambapo amewasihi kujitahidi kuepuka mazingira yoyote ambayo yanaweza kuwa kikwazo kwao na kuwafanya kutokuwa karibu na Mungu.

“ Kiapo chenu ni uaminifu kwa Mungu ukichanganya maisha hayo mliyonayo itakuwa ni masikitiko makubwa sana,wekeni mipaka ya dhati kati yenu na mitandao,  kwa kuongeza maisha ya sala kila siku na kupokea  Huruma ya Mungu kwa kusaidiana ninyi kwa ninyi, kutoachana na kuheshimiana ninyi wenyewe,” amesema Askofu Msonganzila.

Amesema kuwa ni kitu cha msingi sana kuacha dhambi  na pia hakuna sababu ya kuona aibu kuiacha, kwa kuwa  dhambi imekuwa kikwazo kikubwa kwa watu wengi kutoingia mbinguni, hivyo kuna kila sababu ya kuiacha na kuwa karibu na Mungu  kwani  mara nyingi watu wameonekana wema, wapole, wenye unyenyekevu  kwenye jumuiya na kanisani  kumbe  upole huo na utakatifu huo unafunikwa kwa ngozi ya kondoo ndani ni simba huku moyoni ikiwa  imejaa chuki, ubinafsi na uchoyo.

Aliongeza kuwa mapadri na watawa hawana budi  kuepuka roho za chuki, hasira, ubinafsi bali  wajitahidi kuonja huruma ya Mungu kila mahali, hasa sehemu za kazi kwa kudumisha upendo wa kweli  katika maisha yao ya kila siku.


Paroko wa parokia ya Kiabakari Padri Woicheck amemshukuru Baba Askofu wa Jimbo hilo kwa kukubali parokia yake kuwa kituo kikubwa cha Hija  ambacho kina lengo la kupokea makundi mbalimbali ya mahujaji kutoka ndani na nje ya Jimbo ya Musoma.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU