WANACHUO 2,739 WASITISHIWA MIKOPO

BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imesitisha kwa muda mikopo kwa wanafunzi 2,739 walioshindwa kujitokeza wakati wa kuhakiki wanufaika wa mikopo hiyo.

Aidha, imetoa siku saba kuanzia jana kwa wanafunzi ambao hawakuhakikiwa kwenda kuhakiki katika vyuo vyao, vinginevyo mikopo yao itafutwa na kutakiwa kurejesha kiasi walichokopeshwa na kuchukuliwa hatua za kinidhamu.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Jerry Sabi, alisema hatua hiyo imetokana na kuwatilia shaka wanafunzi walioshindwa kujitokeza kuhakikiwa.

“Tumesitisha mikopo kwa wasiohakikiwa kwa sababu hatujui kama ni wanafunzi halali au hewa. Tunataka kuwahakiki pia kwa kuwa hatujui kama wakati tunahakiki wengine walikuwa wagonjwa au wamerudia mwaka au wana sababu nyingine,”alisema.

Mei mwaka huu, Wizara ya Elimu, Sayansi,Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, aliagiza kufanyika uhakiki kwenye taasisi za elimu ya juu nchini kubaini kama kuna uwepo wa wanafunzi wasiostahili kupata mikopo.

Kuanzia Mei 30, mwaka huu, HESLB ilifanya uhakiki katika vyuo 26 na tayari imeshafanya uchambuzi wa uhakiki kwa vyuo 18 kati ya hivyo.

Akizungumzia uhakiki huo, Sabi alisema ulifanywa na timu maalumu iliyoundwa na Bodi kwa kuhakikiwa mwanafunzi husika na kubaini kuwa wanafunzi 2, 739 hawakujitokeza kuhakikiwa. Aliongeza kuwa, Uchambuzi katika vyuo vinane unaendelea.

Hata hivyo, bodi hiyo haikueleza ni wanafunzi wangapi walihakikiwa katika vyuo ambavyo kazi ya uhakiki imefanyika. Alisema bodi itafanya uhakiki wa awamu ya pili ili kujiridhisha kabla ya kuwatangaza kuwa ni wanafunzi hewa na fedha ambazo zitakuwa zimeokolewa kutokana na kuwabaini wanafunzi hao.

Alisema majina ya wanafunzi ambao hawakujitokeza kuhakikiwa wakati wa uhakiki vyuoni yamewekwa kwenye tovuti ya Bodi na pia katika vyuo ambavyo vitafanya utaratibu wa awamu ya pili ya uhakiki.

Alivitaja vyuo vilivyohakikiwa, kufanyiwa uchambuzi wa awali na idadi ya wanafunzi ambao hawakujitokeza kuhakikiwa kwenye mabano kuwa ni Chuo Kikuu cha Dodoma (763), Chuo Kikuu cha Katoliki Ruaha (126), Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino- Mwanza( 232), Chuo Kikuu cha Mzumbe (66) na Chuo Kikuu cha Teofilo Kisaji-Mbeya (130).

Vingine ni Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino-Mbeya (21), Chuo cha Mtakatifu Yohane- Dodoma (262), Chuo Kikuu cha Mkwawa (103), Chuo Kikuu cha Iringa (100) na Chuo Kikuu cha Tiba-Bugando (43), Chuo Kikuu cha Arusha (55), Chuo Kikuu cha Jordan (128), Chuo Kikuu cha Makumira- Arusha (98), Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (385), Chuo cha Ufundi Arusha (22), Chuo Kikuu cha Waislamu-Morogoro (130), Chuo cha Uhasibu (57) na Chuo Kikuu cha Mount Meru (17).

Sabi alisema kutokana na kuwepo wanafunzi ambao hawajajitokeza, muda wa uhakiki umeongezwa hadi Agosti, mwaka huu.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU