Ask.Mapunda: Mkiongozwa na Roho Mtakatifu hamtaishi kwa mazoea

ASKOFU Edward Mapunda wa Jimbo Katoliki Singida amewaasa waamini kumpokea Roho Mtakatifu kwa furaha na shukrani, huku wakikubali maisha yao kuongozwa na Roho Mtakatifu, ambaye anafanya mabadiliko katika utume na maisha.
Ameeleza hayo hivi karibuni, alipofanya ziara ya kichungaji katika Parokia ya Kristo Mfalme ya Kibaoni iliyopo Singida, ambapo pia amewapa Sakramenti ya Kipaimara waamini 229 wengi wakiwa ni watoto na vijana.
Askofu Mapunda ameeleza kuwa Kipaimara hukamilisha sakramenti za kumwingiza muumini katika ukristo, hivyo wanaopokea sakramenti hiyo kwao ni neema na furaha; kwa kuwa Roho Mtakatifu yule yule aliyewashukia mitume, ndiye wanayempokea hata hii leo.
Aidha Askofu Mapunda amewaasa waamini kuwa wapya katika maisha ya huruma, kusameheana, utakatifu na hivyo kutafuta kwanza ufalme wa mbingu.
“Tupambane na makandokando ya maisha, hatuna sababu ya kuogopa majaribu, vishawishi na mateso. Mungu ndiye anayetia nguvu kwenye udhaifu hadi uongofu kwenye dhambi”, amesema Askofu Mapunda.
Parokia ya Kibaoni imefikisha mwaka moja tangu izinduliwe mwaka 2015 na Askofu Mapunda ambaye pia amefikisha mwaka moja tangu kusimikwa kuwa Mchungaji Mkuu wa jimbo hilo.
Awali parokia hiyo ilikuwa ni kigango cha Parokia ya Kanisa Kuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, Singida. Ndani ya kipindi cha mwaka moja zimezinduliwa parokia mbili mpya katika mji wa Singida nyingine ikiwa ni Parokia ya Mtakatifu Yosef Mfanyakazi iliyoko Mandewa, na hivyo kuwa na parokia 3 hadi sasa mjini.
Parokia ya Kibaoni ina waamini 3,150, vigango 14, jumuiya ndogondogo 51 vyama vya kitume 11 na makatekista 18. Mapadri wanaohudumu katika parokia hii ni Paroko Patrick Nkoko, na wasaidizi wa Paroko Padri  Patrick Njiku na Padri Pasian Mwanga.
Katika kipindi cha mwaka moja kuna wakatekumeni 78, waliopata sakramenti ya ubatizo ni 472, ndoa 33, mpako wa wagonjwa 10, waliopokelewa ukatoliki 62, waliorudi kwa msamaha 14 na waliofariki ni 13. Aidha parokia ina waseminari 2 katika seminari ya Mtakatifu Wiliam Diagwa, 5 katika seminari ya Mtakatifu Patrisi Dung’unyi.
Taasisi za kijimbo zilizopo ndani ya mipaka ya parokia ni pamoja na sekondari ya Mpinda (wavulana), chuo cha ualimu cha Mtakatifu Bernard na sekondari ya Mtakatifu Karoli Boromeo (mchanganyiko). Parokia inatekeleza miradi mbalimbali ikiwamo ukamilishaji ujenzi wa Kanisa la Parokia, ujenzi wa nyumba ya mapadri, ujenzi wa makanisa vigangoni, ununuzi wa gari kwa ajili ya huduma za kichungaji na ufundishaji dini.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU