Ask. Ruzoka: Vijana ni mashahidi wa imani

ASKOFU Mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora amewaasa waamini wa Parokia ya Kipalapala kuishi maisha ya Upendo na moyo wa ustahimilivu katika familia zao.
Ametoa rai hiyo hivi karibuni alipoadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na kutoa Sakramenti ya Kipaimara kwa watoto 112 parokiani hapo
Akitoa mahubiri katika Misa hiyo Askofu Ruzoka amewaomba watoto na vijana waliopewa Sakramenti hiyo kuishi maisha ya kusameheana, kwani katika maisha ya pamoja kuna uwezekano mkubwa wa kutofautiana, hivyo inapotokea kukoseana na chuki jambo la msingi ni kusameheana na kuanza maisha upya.
Akifananisha dhambi ya wana wa Israeli na kosa alilofanya Mfalme Daudi, Askofu Ruzoka amesema kuwa hao walitenda dhambi lakini hawakukata tamaa, bali  walitubu. Amewaasa waamini kukimbilia huruma ya Mungu pale wanapotambua kuwa wametenda dhambi.
“Hata kama tukitenda dhambi sisi siyo wa kwanza wala wa mwisho. Sisi ni viumbe dhaifu, hivyo kutenda dhambi kupo, cha msingi ni kuchukua hatua baada ya kutenda dhambi.  Tusipende kutulia katika maisha ya dhambi” ameeleza Askofu Ruzoka.
Aidha Askofu Ruzoka amewaonya watoto na vijana hao kujiepusha na dhambi ya ubaguzi, na kuwa hawapaswi kuwatofautisha binadamu wenzao kwa misingi ya chimbuko lao kwani hakuna myahudi wala myunani, bali wote ni wa Mungu.
Askofu Ruzoka pia amewataka watoto hao waende kuwa mashahidi wa Imani, wajiepushe na chuki, masengenyo, waende wakamshuhudie Kristo katika mazingira yao.
Pia amewaasa watoto na vijana hao kufanyia kazi ndoto zao, wasiishi kwa mapigo ya moyo bali waishi kwa malengo katika maisha yao.
Ibada hiyo pia imehudhuriwa na Paroko wa Kipalapala Padri Thomas Mambo, Gombera wa Seminari Kuu Kipalapala Padri Herman Kachema, Kaimu Gombera Padri Philipo Ntulama, na Padri Andrea Mlele, mlezi wa vijana nyumba ya malezi Kipalapala.   


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU