Sababu za kuondolewa kwa sherehe ya Damu Takatifu ya Yesu kutoka Kalenda Kuu ya Kanisa Katoliki

Utangulizi:
Kwa muda wa miaka 36, kuanzia mwaka 1933 hadi mwaka 1969, Sherehe ya Damu Takatifu ya Yesu ilikuwa ikisherehekewa tarehe kama hii ya leo yaani tarehe ya kwanza  ya mwezi Julai kila mwaka  kwa mbwembwe, kote ulimwenguni katika makanisa ya Kikatoliki. Kuanzia hapo, Kanisa Katoliki halina tena sherehe ya pekee kwa heshima ya Damu Takatifu ya Yesu na badala yake kunakuwa na misa  ya kawaida tu.
Chanzo cha Sherehe ya Sikukuu ya Damu Takatifu ya Yesu:
Sikukuu hii ya Damu Takatifu ya Yesu ilianza kusherehekewa kwanza huko Uhispania kwenye karne ya 16 hivi. Baada ya muda kupita Mtakatifu Gaspari de Bufalo aliipeleka sikukuu hii huko Italia ambako nako ilianza pia kusherehekewa.
Wakati wa fujo za kisiasa na mapigano yaliyokuwa yamezuka mjini Roma, Papa Pius wa X1 alipelekwa uhamishoni Gaeta, mji mmoja katika Visiwa vile viwili vya Sicili hapo mwaka 1849. Katika safari yake hii ya kuhamishwa alikuwa amefuatana na mwenzi wake Padri Giovanni Merlini, aliyekuwa Mkuu wa mapadri wa Shirika la Damu Takatifu ya Yesu. 
Baada ya kuwasili kule Gaeta, Don Merlini alimshauri Papa Pius wa X1 ahaidi kwa kiapo kuwa ataifanya Sikukuu ya Damu Takatifu ya Yesu isherehekewe na Kanisa Katoliki kote ulimwenguni iwapo atafanikiwa kuyatwaa tena Majimbo yake ya Kipapa. 
Papa alilifikiria ombi lile kwa makini sana lakini hakumpa jibu la papo kwa papo. Siku chache baadaye, ilipofika siku ya tarehe ya 30 ya mwezi wa Juni, mwaka wa 1849, Jeshi la Kifaransa liliishinda Roma na likawasambaratisha askari wote waasi wa Jamhuri ya Kirumi na hivyo kuwafanya wasalimu amri. 
Baada ya tukio hilo, Papa Pius wa X1 alimpelekea ujumbe Padri Merlini, yule aliyemshauri atoe ahadi ya kiapo ukiwa kama jibu kwa ombi alilokuwa amempa. Ujumbe huu ulipelekwa na Askofu Yosefu Stella, aliyekuwa wakati huo akishughulika na masuala ya mambo ya ndani ya ofisi ya Papa Pius wa X1. 
Ujumbe wenyewe ulikuwa na maneno kama haya yafuatayo: ‘ Papa haoni kuwa ni jambo la kufaa kutoa ahadi kwa kiapo. Hata hivyo, Papa yuko radhi kutoa kibali mara moja cha kueneza sherehe ya Damu Takatifu ya Yesu kwa mataifa yote ya Kikristo kote  ulimwenguni’.
Tarehe ya 10 ya mwezi Agosti ya mwaka ule ule wa 1849 Sikukuu ya kusherehekea Damu Takatifu ya Yesu iliorodheshwa katika Kalenda Kuu ya Kanisa Katoliki. 
Kalenda hiyo ilikuwa imeonyesha kuwa Sikukuu ya kusherehekea Damu Takatifu ya Yesu  iwe Jumapili ya Kwanza ya mwezi Julai, ambayo ni Jumapili ya Kwanza baada ya tarehe 30 ya mwezi Juni ili iwe kumbukumbu ya ukombozi wa Roma kutoka kwa askari waasi.
Wakati wa kipindi cha utawala wa Papa Pius wa X, tarehe ya kusherehekea Sikukuu hiyo ya Damu Takatifu ya Yesu ilibadilishwa na kuwa tarehe 1 ya mwezi Julai. Badiliko hili lilitokana na nia ya Papa ya kupunguza idadi ya sherehe zinazoangukia siku za Jumapili.
Mwaka wa 1933, Papa Pius wa X1 alipandisha hadhi ya sikukuu hiyo kwa kumbukumbu ya kutimiza miaka 1900 tangu Bwana wetu Yesu Kristo asulubiwe na kufa msalabani. 
Wakati wa mapitio ya Kalenda Kuu ya Kanisa Katoliki yaliyofanywa na Papa Yohani wa XX111 hapo mwaka 1960, Sikukuu hiyo ya Damu Takatifutika ya Yesu iliongezewa hadhi tena na kuwekwa katika daraja la Kwanza la sherehe muhimu za Kanisa Katoliki.
Hata hivyo, ilipofika mwaka 1969 Sikukuu hii ya Damu Takatifu ya Yesu iliondolewa kabisa kutoka Kalenda Kuu ya Kanisa Katoliki. Uamuzi huu ulitokana na ukweli uliofika kuafikiwa na Viongozi wa Kanisa Katoliki kuwa Damu Takatifu ya Mwokozi, Bwana wetu Yesu Kristo inaunganishwa na kusherehekewa katika sikukuu za ibada zingine za hadhi ya juu kama zile za Mateso yake, Sherehe ya Mwili Wake pamoja  na Damu yake Takatifu, Sherehe ya Moyo wake Mtakatifu, na sherehe ya Kutukuka kwa Msalaba. Kwa hiyo haikuonekana kama kulikuwa na ulazima wa kuwa na sikukuu ya pekee tena kwa heshima ya Damu Takatifu ya Yesu.

Umhimu wa Damu Takatifu ya Yesu: 
     Kwa mujibu wa imani ya Kanisa Katoliki, Damu ya Bwana wetu Yesu Kristo ina thamani kubwa sana kwa sababu Damu hiyo ni malipo yake Yeye Mwenyewe Bwana wetu Yesu Kristo ya ukombozi wa wanadamu. Bila kule kumwagika kwa damu hiyo, kusingekuwa na maondoleo ya dhambi. Yesu Kristo, ‘Neno lililogeuka kuwa Mwili’ hakuutoa mwili wake kwa ukombozi wa ulimwengu huu kwa namna nyepesi nyepesi tu; bali alikuwa tayari kuutoa huo Mwili wake kwa kifo cha msalabani, kifo cha umwagikaji wa damu kwa ajili ya ukombozi wa wanadamu wote.
Tunaamini kuwa Bwana wetu Yesu Kristo  aliutoa mwili wake na damu yake  ambavyo sote tunakiri kuwa ni vya thamani kubwa sana kwa ajili ya wanadamu wote, bila kujali madhehebu yao ya dini au tofauti za imani zao. Yeye alilipia kila aina ya dhambi zilizokuwa zimetendwa na wanadamu wote kwa jumla kwa umwajikaji wa hiyo damu.


0754 054 004 kwa msaada wa mtandao.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU