Changamoto za kihistoria katika Kanisa:Skapulari ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli



                                       Changamoto za kihistoria katika Kanisa
                                      Skapulari ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli
Na Philip Komba
Skapulari ya  kwanza kuanzishwa:
     Skapulari ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli, au inayoitwa pia kwa kifupi ‘Skapulari Kahawia’ au inayojulikana vilevile kwa jina moja tu ‘Skapulari’ ni skapulari inayojulikana zaidi kuliko aina zingine zote za skapulari. Aina hii ya skapulari ni pia ya kwanza kuanzishwa kati ya skapulari zote zinazotumiwa na wakristo wakatoliki wakati huu. Baadhi ya skapulari hizo zingine ni kama hizi zifuatazo: Skapulari ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, Skapulari ya Utatu, Skapulari ya Njia Tano, Skapulari Nyeupe, Skapulari Nyeusi, Skapulari Buluu, Skapulari ya Kijani, Skapulari ya Mtakatifu Mikaeli n.k.
     Kwa kuthibitisha umaarufu wa skapulari hii, hata kama ukiandika neno hili moja tu ‘Skapulari’ kama ilivyodokezwa hapo juu, kwa mfano, ‘Sherehe ya Skapulari’  itaeleweka ni skapulari hii tu ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli. Kwa kuzipambanua skapulari zile zingine ni lazima uonyeshe  kwa kutaja jina la skapulari hiyo, kwa mfano, Skapulari ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, au Skapulari ya Mtakatifu Mikaeli au Skapulari Nyeusi au Skapulari Buluu n.k.
Historia ya uanzishwaji wa Skapulari hiyo ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli :
     Kwa mujibu wa mapokeo matakatifu, Mama Bikira Maria alimtokea Mtakatifu Simoni Stock tarehe ya 16 ya Mwezi wa Julai, mwaka wa 1251 huko Uingereza akiwa ameshika skapulari mkononi mwake na akamwambia Mtakatifu Simoni Stock kama ifuatavyo: ‘Chukua skapulari hii mtoto wangu mpendwa kwa ajili ya Shirika lako la Kitawa la Karmeli; skapulari hii iwe kama beji ya Kikundi changu cha kutoa sadaka kwa jamii na pia kama alama maalum ya neema kwako na kwa wanachama wote wa Shirika la Wakarmeli. Yeyote anayekufa amevaa vazi hili hataunguzwa na moto wa milele. Hii ni alama ya wokovu, kinga ya majanga yote, ahadi ya amani na hati ya mapatano.’
     Pamoja na maneno hayo kuwekwa katika mtiririko huu tunaouona mahali pengi katika maandishi, kwa kweli hakuna mwenye uhakika  wa maneno yenyewe  hasa yaliyokuwa yametamkwa  na Mama Yetu wa Mlima Karmeli. Kwa mujibu wa ensaiklopidia ya masuala ya Kanisa Katoliki, maneno yanayosemekana yalitamkwa na  Bibi Yetu wa Mlima Karmeli yalikuwa yameonekana katika hati moja hapo mwaka 1642 iliyosema kuwa maneno hayo yalikuwa yamesemwa kwa sauti na Simoni stock kwa katibu wake ili huyu katibu ayaandike kama alivyokuwa anayasikia yakitamkwa na simoni Stock mwenyewe. Ingawa nyaraka za kihistoria hazina uthibitisho  wa maneno halisi yaliyokuwa yametamkwa na Bibi Yetu wa Mlima Karmeli, maudhui ya maneno yenyewe yanaaminika kuwa ni ya kweli. Hii ni kusema kuwa, ni kweli kwamba Bibi Yetu wa Mlima Karmeli alimhakikishia Mtakatifu Simoni Stock kimwujiza juu ya ulinzi wake maalum kwa Shirika lake la Wakarmeli na kwa wale wote ambao hujiunga na shirika hilo kwa njia ya ibada hata kama hatuwezi kuyapata maneno yenyewe halisi yaliyosemwa na huyu Bibi Yetu wa Mlima Karmeli.
Masharti ya Kupata Manufaa ya Neema za Skapulari:
Uhalisia wa maneno aliyopewa Mtakatifu Simoni Stock na Mama Yetu wa Mlima Karmeli:
     Ahadi na masharti yafuatayo yana uhusiano wa karibu na amri au tangazo linalosemekana lilitolewa na Papa Yohane wa XX11. Tangazo rasmi kuhusu  ahadi hizo lililokuwa limetolewa, inavyoaminika, tangu miaka ya 1400, halikuwa limesikika kutajwa kwa zaidi ya miaka 100 baada ya kutangazwa kwake hapo mwaka 1322 na hakukuwa na waraka wowote ulioandikwa na Papa Yohane wa XX11 kuhusu suala hili.  Imefika baadaye kusadikika tu kwa jumla  kwamba ingawa huo waraka unaosemekana uliandikwa na Papa Yohane wa XX11 hauonekani, zile ahadi na masharti ni halali na mapapa wengi wamewaruhusu Wakarmeli kuzitangaza ahadi hizo.

Ahadi zenyewe ni kama hizi zifuatazo:
     Mkristo aliyekwisha kupokelewa rasmi kama mwanachama wa Shirika la Karmeli ni lazima:
·         avae skapulari muda wote,
·         atunze usafi wa moyo kulingana na hali ya maisha yake,
·         asali kila siku sala  kwa heshima ya Mama Bikira Maria: Baba yetu moja, Salamu Maria moja, na Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu au,
azingatie siku zote za kufunga kwa mujibu wa maelekezo ya Kanisa Katoliki na pia ajinyime kula nyama siku za Jumatano na Jumamosi au
1)      asali Rozari kila siku au
2)      afanye shughuli nyingine yenye manufaa ya kiroho; lakini sharti hili libadilishwe tu baada ya kuruhusiwa na padri aliyepewa madaraka ya kubadili sharti hili.
Umbo na mwonekano wa Skapulari:
Skapulari ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli, kwa kawaida, huwa ni ya rangi ya kahawia ingawa ya rangi nyeusi huwa pia inakubalika. Skapulari hiyo ni lazima itengenezwe kwa kipande cha kitambaa cha sufu. Picha inayoonekana katika skapulari hiyo ni ile ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli akimpa skapulari Mtakatifu Simoni Stock. Skapulari inaweza pia kuwa na michoro ya picha tofauti na hiyo. Kwa mfano , inaweza kuwa na picha ya Bibi Yetu wa Guadalupe, picha ya Moyo Mtakatifu, picha ya Mtakatifu Benedikti au inaweza kutokuwa na picha yoyote yoyote. Ni jambo la kawaida sana skapulari kuandikwa maneno ya zile ahadi za Bibi Yetu wa Mlima Karmeli.

0754 054 004 kwa msaada wa mtandao.
    


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU