WAWATA: Wanaume ndio chanzo cha kutoshiriki makongamano

Umoja wa Wanawake Wakristo Wakatoliki Tanzania WAWATA  Jimbo Katoliki Ifakara wamewalalamikia wanaume kuwa ndio chanzo cha kuwakwamisha wanawake kushiriki makongamano pamoja na kushiriki katika kazi mbalimbali za    Kanisa.
Hayo yamebainishwa wakati wa kongamano la WAWATA Jimbo Katoliki Ifakara lililofanyika katika Parokia ya Mofu kuanzia tarehe 6 mpaka siku ya kilele cha maadhimisho ya siku ya Mwanamke Duniani tarehe 8 Machi.
Katika risala ya wakinamama hao  iliyosomwa na katibu wa WAWATA Jimbo Katoliki Ifakara Bi Longina Mbano mbele ya naibu Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Padri Bonaventura Mchalange, wamesema kuwa kuna baadhi ya wanaume wamekuwa changamoto kwa kutowaruhusu wake zao kushiriki makongamano pamoja na vikao mbalimbali.
Aidha Bi Longina amesema kuwa changamoto nyingine inayowakabili ni mawasiliano magumu kutoka jimboni kwenda kwenye parokia kadhaa hivyo kufanya taarifa nyingi kushindwa kufika kwa wakati.
Kutokana na changamoto hizo WAWATA wamemwomba naibu Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara na maparoko kuwaunga mkono ili kufikia malengo waliyojiwekea katika kumwinua mwanamke na kumfanya kuwa mtegemezi wa Kanisa.
“ Baba naibu wa Askofu tunaomba utusaidie kutoa elimu kwa wanaume kupitia kwa maporoko ili kuweza kuwapa ruhusa wake zao kuja kushiriki nasi katika makongamano, pia tunaomba maparoko na waumini wote jimboni kutuunga mkono katika kongamano la kanda ya Mashariki litakalofanyika Jimboni Ifakara  kuanzia tarehe 23-26 Juni mwaka huu’’ amesema Bi, Mbano.
Naibu Askofu amesema yeye na mapadri wenzake na hasa maparoko watashirikiana kuhakikisha wanaume wanathamini umuhimu wa mwanamke katika Kanisa la Mungu.
‘’ Mwanamke ndio msingi wa Kanisa la Mungu kwani kila kiumbe huzaliwa na mama yake, hivyo viongozi wa Parokia, vigango na Jumuiya  mhakikishe mnakuwa imara kwa ajili ya kutetea haki ya wakina mama hawa,’’ amesema Naibu wa Askofu Padri Mchalange.
Naye Paroko wa Parokia ya Mofu Padri Markus Mirwatu ameupongeza uongozi wa WAWATA Jimbo kwa kufanyia maadhimisho hayo katika Parokia ya Mofu kwani imekuwa chachu ya kuwainua wanawake ndani ya Parokia hiyo.
‘’Nawaombeni WAWATA Jimbo tushirikiane kuwainua wanawake hawa wa hapa Mofu ambao siku zote wanaamini kuwa wao si kitu katika Kanisa hivyo nataka watambue kuwa wao ni bora sana  na waifanye kazi ya Mungu hasa ya uimbaji kwaya kanisani,’’ amesema Padri Mirwatu.
Kongamano hilo la WAWATA Jimbo Katoliki Ifakara limefanyika kwa siku 3 katika Parokia ya Mofu na kuhudhuriwa na wanawake takribani 385 kutoka katika Parokia zote 23 za Jimbo ambapo wamepatiwa elimu juu ya mambo mbalimbali kutoka kwa wakufunzi ambao ni Mapadri Godfrey Hongo Paroko wa Chita na Florence Mkenda (OFM Cap) Paroko wa Mbingu.
WAWATA hao walitembelewa na Mheshimiwa Susan Kiwanga Mbunge wa Jimbo la Mlimba ambaye aliwataka kuongeza juhudi katika kujiletea maendeleo kwa lengo la kupunguza umaskini.
Wanawake Wakatoliki Jimbo Katoliki Ifakara wameshirikiana na wanawake wenzao duniani kote kuadhimisha siku ya Mwanamke Duniani kwa kufanya kongamano hilo huku mwaka 2018 wakipanga kufanya kongamano katika Parokia ya Kisawasawa Dekania ya Kilombero.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU