‘Madaktari waende Kenya lakini Tanzania pia ina uhitaji’

“SERIKALI ya Tanzania itafute namna ya kuwaajiri madaktari wake ili kuziba pengo kubwa la upungufu wa madaktari nchini.”
Hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara Mhashamu  Severine Niwe-Mugizi wakati akizungumza na Gazeti Kiongozi kuhusu maamuzi ya Serikali kutuma madaktari wake nchini Kenya.
Askofu Niwe-Mugizi japokuwa hajapinga uamuzi huo lakini amesema lazima serikali iangalie uhitaji wa madaktari katika hospitali na vituo vyote vya afya nchini hususani majimbo yaliyoko pembezoni mwa nchi.
“Sina pingamizi juu ya hilo kwani watu wa Kenya wanaumia kwa sababu hawana madaktari wa kuwatibu, lakini ninachotaka tukiangalie ni usalama wa madaktari wetu.
Ikumbukwe kuwa, Chama cha Madaktari Kenya kina mgogoro na serikali hivyo badala ya kusuluhisha tatizo hilo wanaamua waiingize Tanzania. Je, Chama hicho cha Madaktari Kenya hakitaiona Tanzania kuwa ni wasaliti? Pili Kenya ina changamoto za kiusalama kwani mara nyingi wanavamiwa na Al shabaab. Tatu muundo wa ajira zao upoje? Je, tukiwapeleka ndilo suluhisho?,” amehoji Askofu Niwe-Mugizi.
Ameiasa Serikali kuwa makini kutoiingiza nchi kwenye matatizo pia kuangalia matatizo ya nchi yao kwanza kabla ya kusaidia mataifa ya nje.
Kwa upande wake Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Methodius Kilaini amesema kuwa, tatizo la Kenya linawapa fursa watanzania kupata ajira ingawa haijaeleweka kuhusu muundo wa mikataba yao na kuwa itakuwa mikataba ya aina gani.
“Tanzania imekuwa na vyuo vingi vya Afya, imezalisha madaktari wengi ingawa hatuwezi kuwaajiri wote. Mimi mwenyewe inawezekana kwenye Jimbo kuna hospitali na vituo mbalimbali vya afya  lakini hatuwezi kuwaajiri wote. Hivyo badala ya kurandaranda na kulalamika mitaani watumie fursa ya kwenda huko kufanya kazi.
Hii ni kawaida nchi moja kupeleka madaktari ama wafanyakazi wake nchi za nje kufanya kazi. India ina madaktari wengi, Ufilipino pia na wengine lakini wamewatawanya kwenye nchi mbalimbali ili kuingiza pato la nchi na kutatua tatizo la ajira. Hivyo, kama kuna makubaliano yanayoeleweka, watapata huduma zote za msingi hususani usalama waende wakaokoe watu wanaoumia, wanaougua bila kupata matibabu,” amesema Askofu Kilaini.
Hali hii inafuatia makubaliano kati ya serikali ya Tanzania na Kenya mwishoni mwa wiki ambapo madaktari wapatao 500 watapata ajira nchini Kenya.
Kenya imeahidi kuwa itaendelea kuwasaka madaktari zaidi kutoka mataifa mengine Afrika ili kufanikisha huduma bora. Sekta ya afya nchini humo iliathirika zaidi baada ya madaktari kugoma kwa siku mia moja na kufifisha utoaji wa huduma za afya nchini humo.
Madaktari walioomba nafasi za kwenda nchini Kenya mpaka sasa ni zaidi ya 150.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU