VIKOBA iboreshe afya za watoto vijijini-TEC


IMEELEZWA kuwa mafanikio ya kiuchumi yaliyofikiwa na Vikundi  vya Benki za Kijamii Vijijini vinavyoendeshwa chini ya Mahusiano ya Dini Mbalimbali (IR-VICOBA), yaende sambamba na utoaji wa lishe bora kwa watoto katika familia ili kuwajenga  kiafya na kiakili.
Rai hiyo imetolewa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Raymond Saba, wakati akizungumza na Kamati ya Mahusiano ya Dini Mbalimbali,wawezeshaji na wawakilishi wa vikundi vya IR-VICOBA pamoja na wawezeshaji wakuu wa Mfumo wa Ufuatiliaji wa Rasilimali za Umma (PETS) wilayani Mbozi.
Padri Saba aliyekuwa ziarani wilayani humo kutembelea shughuli zinazotekelezwa chini ya Kamati ya Mahusiano ya Dini Mbalimbali kupitia TEC kwa ufadhili wa Shirika la Misaada la Makanisa ya Norway (NCA), alisema pamoja na kufikiria kujiongezea kipato kutokana na shughuli za uzalishaji wanazozifanya kutokana na fedha wanayokopa kwenye vikundi vyao, lakini hawanabudi pia kujali afya za familia hususani watoto.
“Kama ni ufugaji wa kuku basi pale wanapoanza kutaga  ni vyema kuwapatia watoto mayai ili kuwajenga kiakili badala ya kupeleka mayai yote kuyauza,” alisema.
Katibu Mkuu huyo wa TEC pia amewapongeza wana IR-VICOBA kwa utaratibu waliojiwekea katika kuwasaidia watoto yatima na wale wanaoishi mazingira hatarishi wilayani humo; hivyo akasema hii ni moja ya tunu ya vikundi hivyo na kielelezo tosha cha Upendo na Amani kama inavyosisitiza kaulimbiu ya Mahusiano baina ya Dini Mbalimbali.
Sanjari na hayo Padri Saba aliwasisitiza Wanambozi kuwa na uchumi wa kimapinduzi hasa kwa kufanya shughuli zao kwa kupiga hatua mbele zaidi badala ya kutegemea misaada toka kwa wafadhili wa nchi za Magharibi.
“Fanyeni shughuli zenu kwa kipiga hatua mbele zaidi na si kutegemea misaada toka  Ulaya, misaada toka Ulaya kwa sasa imepungua na itafikia hatua itaisha kabisa,” alisisitiza.
Katika hatua nyingine Afisa Miradi Mwandamizi wa NCA-Tanzania, Bi. Agustina Mosha, ambaye aliongozana na Katibu Mkuu huyo wa TEC katika ziara hiyo, pamoja na mambo mengine alisisitiza umuhimu wa utoaji wa taarifa kwa wakati ikiwa ni kuanzia kwenye  ngazi ya vikundi, wilaya hadi Taifa.
Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Miradi ya Maendeleo inayotekelezwa na chini ya Kamati ya Mahusiano ya Dini Mbalimbali wilayani Mbozi kupitia TEC, Mratibu wa Miradi hiyo Bw. John Mwallah, kwa sasa vikundi vya IR-VICOBA wilayani humo vina vikundi vipatavyo 228 vyenye hisa zenye thamani ya shilingi takribani bilioni tatu.
Licha ya huduma za kiroho, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) chini ya Ufadhili wa NCA linatekeleza  miradi ya maendeleo kwa kupitia Kamati za Mahusiano baina ya Dini Mbalimbali katika wilaya za Mbozi, Njombe, Ludewa, Kasulu, Karatu, Babati, Mtwara na Temeke.
Miongoni mwa miradi hiyo ni  vikundi vya Benki za Kijamii Vijijini (IR-VICOBA), utoaji elimu ya utawala bora na ufuatiliaji wa matumizi ya Rasilimali za Umma (PETS), miradi ambayo  ndani yake pia kuna masuala mtambuka kama  Jinsia, Usaidizi wa Kisheria na Mabadiliko ya Tabia nchi.
Hadi kufikia katikati ya mwaka jana TEC kupitia kamati hizo za Mahusiano ya Dini Mbalimbali ilikuwa na jumla 751 vya IR-VICOBA wanachama 19,324 kati ya yao wanawake ni 12,874 sawa na asilimia 67 huku idadi ya wanaume ikiwa ni 6,446 sawa na asilimia 33 ya wanachama wote.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU