Kwaresima dira ya muelekeo wa maisha yetu






KUNA mambo mbalimbali ya kufanya katika kipindi cha Kwaresima. Kwanza sadaka, sala na kufunga. Sadaka inaweza kuwa pesa, sadaka inaweza kuwa kujitolea kwa jili ya wengine, sadaka inaweza kuwa kuwasadia wazazi na wasiojiweza katika shughuli mbalimbali. Sadaka ni pamoja na kufanya kazi katika muda wa ziada bila malipo.

Na katika sala tunafundishwa ama tunakumbushwa kusali na Baba aliye sirini ndani ya mioyo yetu. Siyo kupayuka. Pia tukisali tusisali kwa jili yetu tu, bali pia kwa jili ya watu wengine. Tusali kwa ajili ya wagonjwa.Tusali kwa ajili ya watu wanaoteseka kwa namna mbalimbali, hali kadhalika tusali kwa ajili ya kuliombea taifa letu na ulimwengu mzima.

Ikiwa ulikuwa na bomba la mdomo linalotoa matusi, dharau, majivuno, wivu, uwongo hivyo kwa sasa vinatakiwa vitiwe korokoroni yaani visiwepo katika kipindi cha Kwaresima. Ni bora ule kanda, ugali, pilipili ushibe lakini usitende dhambi kuliko kuacha kula kwa kigezo cha kufunga, lakini ikifika usiku unafanya ulozi, unatukana, una dharau wengine, unawasemea wengine uwongo, hutoi sadaka, husali huko si kufunga bali ni kujidanganya.

Tena, ukifunga usifanye matangazo mbele ya watu wa ulimwengu, bali iwe siri yako na Baba yako wa mbinguni. Nakumbuka andiko lililoandikwa na mwandishi mmoja wa gazeti hili. Aliandika habari ya Mhindi kijana mwanamapinduzi namna alivyokuwa akimwomba Mungu kwa sala.

Mhindi huyo angali kijana mwanamapinduzi anatajwa wakati akiwa kijana alimwomba Mungu ''Mungu nipe nguvu ya kubadili dunia'' hata hivyo hakufanikiwa, na baadaye akamwomba Mungu akiwa na miaka 40 kwa kusali hivi ''Mungu nipe neema ya kuwabadili wale ninaokutana nao''. Kweli akabadili wana familia na marafiki zake na akajisikia vizuri.

Sasa ni mzee anaanza kuona madhaifu yake sasa sala yake ipo hivi: ''Mungu nipe neema ya kubadilika'' kisha akasema angesali hivyo asingepotea katika maisha. Kwaresima ni uhalisia wa maisha yetu. Ni kipindi cha toba kwa kutafakari matendo makuu ya Mungu.

Katika kipindi hiki tunakumbuka mengi kuhusu huduma ya Yesu Kristo katika Miji mbalimbali ukiwemo Mkoa wa Yudea.Yesu alijaribiwa na Shetani 'eti' ampe miliki ya utajiri wa dunia na aachane na kazi anayoifanya. Lengo lake shetani alitaka awe mtawala kuliko Mungu. Unajiuliza huyu shetani utajiri huo aliumba yeye mpaka anataka kummilikisha Yesu?.Anajua hati ya miliki hizo ilipo?,anajua hizo hati zilitolewa na Manispaa gani huko Mbinguni?.

Yesu alishinda majaribu. Je, sisi tunaishi katika misingi ya kushinda majaribu katika maisha yetu ya kila siku?, je tukijaribiwa tunafanya nini au mawazo yetu yanaelekezwa wapi kutafuta ufumbuzi wa majaribu?.Mfano wa huyo Mhindi unaakisi kipindi cha Kwaresima, kwamba mabadiliko huanza na wewe, kisha jirani na baadaye ulimwengu mzima (changes begin with you, and begin in your mind; mabadiliko yanaanza na wewe, na yanaanza katika akili yako).

Mara nyingi watu wa ulimwengu hutazamia kuwabadilisha wengine ili hali wao wenyewe hawajabadilika. Hivi fisadi anaweza kumbadilisha fisadi mwenzake. Yesu Kristo wakati anahubiri Injili alikutana na vikwanzo vingi. Huduma ya Yesu haikuwa ya lelemama kama ambavyo wafausi wa kweli wa kristo wanavyoteswa katika nchi ambazo hazitaki kusikia habari ya Injili.

Kazi ya Yesu haijakamilika, kwani hata yeye alingia kwenye falme ambazo hazikutaka kusikia habari za Injili. Aliwindwa kwa tabasamu kwa nia mbaya. Lakini alitimiza majukumu yake kwa unyenyekevu. Ulimi wake ulimlinda hata hukumu yake kwa Pilato haikuwa na nguvu, ingawa naye Pilato kwa sababu ya uwogo wa umati wa watu uliomtaka Yesu asulubiwe, aliamua kutimiza matakwa ya wajinga walio wengi.

Hiyo ilikuwa michezo michafu dhidi ya Yesu ukiachilia mbali rushwa aliyoipokea Yuda ili amsaliti Yesu, ingawa Yuda alijutia kile alichofanya. Je, ni watu wangapi leo hii wakikosa wanajutia makosa yao nakuwa tayari kuacha dhambi?.Je, kuna ubaya gani katika Injili?. Yesu Kristo katika mafundisho yake anasimamia haki.

Haki ya kuchanganyika na wenye dhambi, pia anasimama ukweli dhidi ya yule mwanamke waliotaka kumuuwa kwa kupiga mawe, lakini wale wauwaji walipotakiwa kujibu swali la Yesu dhidi ya yule mwanamke walikimbia.Je, tunajifunza nini juu ya hukumu dhidi ya wengine?.

Injili inahimiza upendo, huruma, msamaha, amani, maridhiano, je, ni wapi katika maandiko ya Injili yanahimiza watu wauane ama wasipendane. Kwaresima inaakisi maisha yetu na maisha ya Yesu. Yeye alidharauliwa, alikatishwa tamaa lakini alisonga mbele. Kuanguka kwake Yesu na msalaba, kisha kuinuka kwake ni utambulisho wa mkristo kusonga mbele mpaka neno la Mungu litimie.

Maisha yetu yanazongwa na aina hiyo ya maisha aliyoishi Yesu. Tunapoanguka tunahimizwa kusimama na kusonga mbele hadi mwisho wa maono yetu. "Nyiyi ni chumvi katika dunia, hivyo chumvi ikikosa ladha itawezaje kutumika? ni sawa na uzuri pasipo faida bali hutupwa na kukanyagwa na miguu ya wanadamu.

Ninyi ni mwanga katika dunia, mji ulioinuliwa kilimani kamwe haufichiki. Wala taa haiwashwi halafu ikafunikwa ndani ya kikapu, bali huinuliwa katika ngazi yake na hutoa mwanga kwa watu wote walio ndani ya nyumba. Mwanga wenu ung'are kwa watu wote ili waone mema yenu wamtukuze Mungu aliye mbinguni"

Hayo ni maneno Matakatifu. Mafunzo hayo yalikuwa muhimu sana kwa wanafunzi wake pia ni muhimu sana kwetu hivi leo. Maelezo fulani yanaeleza kuwa katika miaka ya nyuma chumvi ilitumika kutunza vyakula kama nyama na samaki ili isiharibike, chumvi ilikua muhimu kama ilivyo friji katika miaka hii....

Hapa Kristo anatufundisha maisha yetu kama wanafunzi wake yanapaswa kuwa ya mfano na ushawishi kwa jamii ili jamii ipokee ufalme wa mbingu. Ufalme wa mbingu ni mema yote ya Mungu. Chumvi huleta mabadiliko, hubadili ladha ya chakula mara tu inapochanganyika katika chakula husika, hivyo nasi pia tukiwa wakristo maisha yetu yanapaswa kuleta mabadiliko.

Chumvi ina ladha,ikiingia katika chakula kinakuwa na ladha. Hapa Kristo anatufundisha kwamba pamoja na tamaa, chuki, wivu, uchoyo, usaliti, mapigano na hata mauaji yaliyoenea katika jamii ya sasa tukimruhusu Roho Mtakatifu aishi maisha ya Kristo kupitia sisi, jamii itakuwa na ladha kama yetu sisi ambao ni chumvi.

Chumvi huleta kiu, tazama maisha katika jamii zetu kila mtu anahamaki, kuteseka na kutapatapa na mizigo ya dhambi iwe ni rushwa, tamaa, anasa, pombe na dawa za kulevya ilimradi ni dhambi lazima inamtesa. Hivyo sisi tuliompokea Yesu Kristo kwa ubatizo, kipaimara, ndoa na kukataa maisha ya kuoa kwa ajili ya kuelekeza nguvu ya utumishi wa ki-Mungu, sharti tuchochee furaha, amani kwa watu walioko katika gereza la dhambi nao watubu dhambi zao na kumpokea Yesu.

Chumvi huenea, na ni wazi kwamba chumvi kidogo sana inaweza kuleta ladha katika chungu kikubwa hivyo ndivyo Injili hufanya kazi. Habari za Yesu zilianza na kikundi kidogo tu cha watu na kuenea dunia nzima. Hivyo na sisi tusife moyo kuishi maisha katika Bwana tukiamini kuwa kazi yetu ni kubwa na mwisho wake ni wokovu. Wapo watu ambao hufikiria imani za wengine ni upuuzi, na kwamba wao imani zao ni sahihi. Watu hao sharti waulizwe ikiwa hawana upendo kwa wengine imani yao yatoka wapi?.



Wapendwa wote wa Mungu, tunayo sababu ya kutambua kipindi cha Kwaresima ni kipindi kinachoweka wazi maisha yetu ya ulimwengu, na tunafundishwa aina ya ulimwengu tunamoishi.Yesu Kristo katika ukamilisho wake wa neno la Mungu aliishi katikati ya watu wa mataifa mbalimbali, mikoa, miji na wafalme wenye nguvu na waliotumia madaraka yao vibaya kuwangamiza wengine.

Ni wivu tu.Wivu ni roho mbaya inayomwingia mtu na kumfanya asifurahie mafanikio ya kubarikiwa kwa watu wengine. Ni ile hali ya kuwa na “kijicho” yaani hali ya kutafuta namna yoyote ile ya kuzima mafanikio ama baraka za mtu mwingine.

Shetani anaona wivu kwa nini tuna afya njema, kwa nini tumebarikiwa, kwa nini tuna furaha. Wivu dhidi ya Yesu ilikuwa ni sababu ya kuteswa kwake na kufa msalabani hata yule nyoka wa bustanini aliyefanya udanganyifu aliona wivu dhidi ya maisha ya Adamu na Eva akaamua kuwaharibia.

Mungu atupe nguvu ya kuyashinda majaribu. Kwaresima iwe njema na yenye kuleta mabadiliko kuanzia ndani ya mioyo yetu, akili zetu na hatimaye mabadiliko hayo mema yawe chumvi ya ulimwengu.

 Na Brown Sunza

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU