Siku ya Wanawake Duniani,Kitaifa kufanyika kila baada ya miaka mitano

KILA mwaka Machi 8, Watanzania wataungana na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, katika kuadhimiasha Siku ya Wanawake Duniani lakini Serikali ya Tanzania imesema sherehe hizo kitaifa zitafanyika kila baada ya miaka mitano.
Taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Sihaba Nkinga,  wakati akizungumza  na waandishi wa habari katika Ofisi ya Wizara hiyo iliyoko Chuo Kikuu cha Dodoma ilisema kuwa,
Maadhimisho hayo kwa mwaka huu yatafanyika katika ngazi ya mkoa kufuatia uamuzi wa Serikali wa mwaka 2005 kuwa yatakuwa yanafanyika kitaifa kila baada ya miaka mitano.
"Uamuzi wa kuadhimisha siku hii kitaifa kila baada ya miaka mitano,  ulikusudia kutoa nafasi kwa Serikali yenyewe na wadau wengine kuweza kupima mafanikio ya shughuli za maendeleo ya wanawake, changamoto zilizoko na kuweka mikakati ya utatuzi wa changamoto hizo", alisema.
Katibu Mkuu amesema, Kaulimbiu ya Siku ya Wanawake Duniani kitaifa kwa mwaka 2017 inasema  ‘Tanzania ya Viwanda; Wanawake ni Msingi wa Mabadiliko ya Kiuchumi.’ Kaulimbiu hii inasisitiza kuwajengea  wanawake uwezo wa kitaaluma, kibiashara, upatikanaji wa mitaji, masoko na mikopo ili waweze kushiriki kwa usawa, na kunufaika na fursa zilizopo badala ya kuwa wasindikizaji tu.
  Dhamira ya Kaulimbiu ya ‘Tanzania ya Viwanda; Wanawake ni Msingi wa Mabadiliko ya Kiuchumi’ inalenga kuhamasisha jamii na wadau wote nchini kuongeza fursa za kiuchumi kwa wanawake ili kuwawezesha kushiriki na kunufaika na fursa za maendeleo katika kipindi hiki ambapo Tanzania inaelekea katika uchumi wa viwanda.
Kaulimbiu  hii imetoholewa kutokana na Kauli Mbiu ya Umoja wa Mataifa inayosema ‘Women Economic Empowerment in the Changing World of Work’ ambayo kwa tafsiri ya Kiswahili ni ‘Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi Katika Dunia ya Mabadiliko ya Kazi.’
Kaulimbiu ya Umoja wa Mataifa inalenga kuzihamasisha Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa kuwawezesha wanawake kiuchumi ili kuendana na kasi ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia katika sekta za umma na binafsi.

Kaulimbiu ya Kitaifa ya Siku ya Wanawake Duniani  ya mwaka huu imeandaliwa kwa kuzingatia Mazingira ya Nchi yetu; vipaumbele vya kimaendeleo na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU