“Kufunga siyo fasheni” Askofu Mkude



ASKOFU wa Jimbo Katoliki Morogoro Mhashamu Telesphor Mkude amewaasa waamini kuachana na matendo maovu katika kipindi hiki cha Kwaresma na badala yake wajitahidi kufanya mema yanayompendeza Mwenyezi Mungu kwa uthabiti wa moyo na nia njema.

Askofu Mkude amesema hayo katika waraka wake maalumu wa kichungaji katika kipindi cha Kwaresma akiwahimiza waamini kujitoa sadaka kwa kufunga na kuwasaidia wengine wenye shida mbalimbali kwa lengo la kuwaonjesha upendo ambao waliukosa.

Aidha Askofu Mkude amesema kuwa Kwaresma  ni kipindi cha kusali, kusoma na kulitafakari neno la Mungu, pia kulitangaza kwa wengine ambapo kwa kufanya hivyo kutasaidia kusimamia misingi ya imani ya Kanisa Katoliki.

“Ni kipindi cha kusali zaidi, kutafakari, kusikiliza na kusoma vitabu mbalimbali ili tuwe na uelewa mpana zaidi, pia kulitangaza kwa wengine ili kuwaangazia nao wamjue Mungu, wampende na kumtumikia na kwa kufanya hivyo kutasaidia kusimamia misingi ya imani yetu vyema,” amesema Askofu Mkude.

Pamoja na hayo Askofu Mkude ameongeza kuwa wapo baadhi ya watu ambao wanaishi maisha ya shida, hivyo kipindi cha Kwaresma ni muda muafaka wa kuwatazama wao ambao wanahangaika kwa kukosa chakula na mahitaji mengine ya msingi.

“Kuna baadhi ya watu wanaishi katika maisha ya shida, hivyo kipindi hiki cha Kwaresma uwe ni muda muafaka wa kuwatazama wenye shida na wanaohangaika kwa kukosa chakula na mahitaji mengine ya msingi na usifunge ili uhifadhi kiwe kingi badaye utumie mwenyewe, hapo utakuwa unajidanganya,” amesema Askofu Mkude.

Hata hivyo ameeleza kuwa mtu yeyote anayepaswa kufunga ni yule ambaye anajitoa kwa moyo kufunga kwa nia njema na wala si kufunga kwa sababu ya kukosa chakula, bali kufunga ni kujikatalia kwa malengo ya kuwasaidia wahitaji.

“Mtu anayepaswa kufunga ni yule ambaye amejitoa kwa moyo kufunga kwa nia njema na si kwa kukosa chakula bali kufunga ni kujikataa kwa malengo ya kuhifadhi na kuwasaidia wahitaji kwa mavazi, chakula na mahitaji mengine muhimu, hivyo tutumie vizuri kipindi hiki kwa kujisafishia njia kwa kutubu pia,” amesema Askofu Mkude.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU