Askofu Anyolo- Wasaidieni waamini kuzielewa nyaraka za Kanisa


MWENYEKITI wa Idara Uchungaji Umoja wa Wanachama Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki   AMECEA Askofu Philip Anyolo, amewataka waratibu wa Idara za Kichungaji nchi wanachama wa AMECEA kuwa makini na kukuza mshikamano katika kukabiliana na changamoto zao za kikanda hasa kuwafafanulia waamini nyaraka mbalimbali za Kanisa.
Askofu Anyolo amesema hayo wakati wa warsha ya siku nne juu ya uratibu madhubuti wa rasilimali fedha na watu pamoja na namna ya kuandika miradi iliyofanyika katika Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia-Addis Ababa (CBCCE) .
Askofu Philip amewataka washiriki kupendekeza miongozo ya kina juu ya majukumu na wajibu wa waratibu wa Uchungaji na kutafakari juu ya matokeo ya nyaraka za  Kitume ikiwemo "Amoris Laetitia" (Furaha ya upendo juu ya familia iliyoandikwa na Papa Fransisko), katika Kanisa na nhi za AMECEA.
Kutafakari na kutafsiri nyaraka hizi namna zinavyoweza kusaidia huduma za Kichungaji katika ngazi ya AMECEA, Kitaifa, Jimbo, Jumuiya hadi familia.
“Papa Fransisko ametoa nyaraka muhimu za familia, mazingira na mengineyo. Nyaraka hizi zina maana na ni muhimu kwa kila mkristo mkatoliki. Ndiyo maana inafaa kushirikiana na ofisi za mawasiliano katika kutafsiri na kuzisambaza kwa waamini. Pia kupata tafsiri halisi kutoka kwa wataribu wa kichungaji ili waelewe na kufanyia kazi.
Pia ninawasihi kujadili yale ambayo tumekubaliana hapa katika warsha hii ili kusaidia wengine kufanya hivyo. Tunataka Ofisi zetu za Kichungaji ziwe na nguvu za kujibu changamoto mbalimbali za kifamilia na na kutoa miongozo mbalimbali ya kichungaji ili kufikia malengo yetu," amesema Askofu Anyolo.
Aidha amewasisitiza waratibu wa kichungaji kuhakikisha kwamba wanashiriki mikutano inayofanyika katika kanda zao na katika nchi za AMECEA ili kupeana mbinu mbalimbali za kichungaji ikifahamika kuwa sekta ya Uchungaji ni nyeti maana inagusa maisha ya watu kiroho na kimwili.
“Ni vyema kuungana na  kujifunza kutoka kwa kila mmoja. Kujenga mahusiano chanya kati yetu na kuimarisha imani yetu,” amesisitiza Askofu Anyolo.
Semina hiyo ya Waratibu wa Kichungaji imehudhuriwa na   washiriki 14 kutoka nchi 8 za AMECEA yaani; Ethiopia, Eritrea, Kenya, Malawi, Tanzania, Uganda na Zambia na kuwezeshwa na wafanyakazi kutoka Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki cha Afrika Mashariki (CUEA) kwa ufadhili wa USCCB.




Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU