AMECEA yaipongeza Tanzania miaka 150 ya uinjilishaji


MWENYEKITI wa Umoja wa wanachama Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki (AMECEA), Mwadhama Berhaneyesus Kardinali  Souraphiel wa Addis Ababa Ethiopia amelipongeza Kanisa Katoliki Tanzania kwa Jubilei ya miaka 150 ya uinjilishaji akisema ni ukomavu wa imani.
Akizungumza na Gazeti Kiongozi hivi karibuni Addis Ababa Ethiopia, Kardinali Souraphiel amesema kuwa, anafahamu Kanisa Katoliki Tanzania kuwa lina historia ndefu ya imani kuanzia mlango wa Imani Bagamoyo ambapo wamisionari wa Kwanza waliingia na kusimika msalaba.
“Ninawapongeza maaskofu, mapadri wa majimbo na mashirika ya kitawa pamoja na waamini wote kwa kuilinda imani Katoliki ambayo ni tunda la wamisioari wa Kwanza nchini humo.
Changamoto za wamisionari za wakati ule zilikuwa si za kawaida. Ninakumbuka wakati fulani Kardinali Pengo alinieleza mengi kuhusu historia ya Uinjilishaji nchini Tanzania ambayo ina mvuto wa kipekee. Mimi mwenyewe nilishawahi kufika Bagamoyo  kushuhudia asili ya Ukristo Tanzania.
Ninajivunia kuwa imani Katoliki imekuwa imara hadi sasa nchini Tanzania. Ninawaombea waamini wote pamoja na maaskofu kuendelea kuishikilia imani yao bila kujali changamoto mbalimbali ambazo ni sehemu ya utume.
Hongera Kanisa la Tanzania kwa utume. Mtuombee na sisi Kanisa la Ethiopia ambapo bado wakatoliki ni wachache na si kazi rahisi kuinjilisha hapa kwani dini zingine zina waamini wengi kuliko wakatoliki lakini pia ninafarijika kwani mapadri, waamini na maaskofu wanajituma kutekeleza utume wao kama inavyopaswa,” ameeleza Kardinali Souraphiel.
Hata hivyo Kardinali Souraphiel amefarijika warsha ya kuratibu rasilimali kufanyika katika nchi yake na Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia akisema kuwa ni heshima kwake na kwa waamini pamoja na maaskofu na mapadri nchini humo.
“Tumeshiriki mikutano mbalimbali ya AMECEA Dar es Salaam Tanzania ambapo nilipafurahia, tumeenda Malawi na Kenya kwa mara kadhaa. Hivi leo ninapoona wanahabari na Makatibu wa Idara ya Kichungaji kutoka nchi mbalimbali za AMECEA ninaona furaha ya ajabu.
Hata hivyo iwe ni moja ya maandalizi ya Sinodi ya Maaskofu AMECEA (plenary) itakaofanyika  mwezi Juni mwaka 2018 .
Hii ni mara ya kwanza Sinodi hiyo kufanyika Ethiopia ndiyo maana tuna shauku kubwa na tayari tumeanza maandalizi ya kuwapokea maaskofu zaidi ya 200, viongozi wa serikali, mapadri pamoja na waamini kutoka ndani na nje ya nchi.
Hii inaonyesha umoja na mshikamano katika jamii na ulimwengu wa sasa. Hata Kanisa Katoliki la Ethiopia kwa uchache wao linapata faraja kuwaona ndugu zao wakiwaimarisha kiimani na kufarijika kuwa wana ndugu zao kutoka mataifa mengine,” ameeleza.
Kardinali Souraphiel pia ameeleza kuwa, angefarijika sana kama Papa Fransisko ataitembelea Ethiopia wakati wa safari yake nchini Sudani kwani Ethiopia ni karibu na nchi hizo na waamini wa Ethiopia pia wanahitaji kuimarishwa kiimani na kwamba Ethiopia ni Mji Mkuu wa Umoja wa Mataifa ya Afrika.
“Tayari Umoja wa Mataifa ya Afrika (AU) umemualika Papa kuja Addis Ababa kuzungumza nao pengine yatazungumzwa mengi ambayo yatatatua migogoro katika nchi za Afrika. Ingawa Kanisa la Ethiopia halijamualika Papa lakini tungependa kufanya hivyo ili kama atakubali kufanya mazungumzo na viongozi wa Afrika hapa Addis Ababa nasi tungepata fursa ya kushirikishana naye masuala mbalimbali ya kiimani,” amesema Kardinali Souraphiel.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU