Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

Na Charles Rwehumbiza
UINJILISHAJI BAGAMOYO NA TANZANIA KWA UJUMLA
Kutokea Bagamoyo, wamisionari wa Shirika la Roho Mtakatifu waliweza kuendelea kuinjilisha sehemu mbalimbali za Tanzania kama vile Mhonda (Morogoro), Mandera (Morogoro), Kilema Kibosho (Moshi) na Kondoa, n.k. Kutokana na ugumu wa watu wa Bagamoyo kukubali Injili na uamuzi wa wamisionari wenye asili ya Uholanzi kuhamia Morogoro mjini.
 Bagamoyo iliachwa kwa kipindi kirefu bila huduma za mapadri au wakiwa wanapata  huduma ya Misa Takatifu  mara moja kwa mwezi. Jambo hili lilisababisha ukuaji wa Kanisa la Bagamoyo kuwa duni sana hadi mwaka 1992 padri mwafrika wa kwanza alipoingia na kuweka makazi ya kudumu Bagamoyo. 
Padri huyu wa kwanza mwafrika kuinjilisha Bagamoyo sio mwingine ila Padrei Valentine Bayo wa Shirika la Roho Mtakatifu. Tangu aingie Bagamoyo, Padri Bayo chini ya usimamizi wa shirika lake, ameweza kuipa Bagamoyo hadhi iliyo nayo leo hii. Hakika haitakuwa vibaya kumwita Padri Bayo “Baba wa Uinjilishaji Mpya Bagamoyo”.
Anastahili jina hilo kwani ameitoa Bagamoyo kutoka parokia na jengo moja la Kanisa hadi kuwa na parokia tatu, yaani Moyo Safi, Epifania na Kristo Mfalme pamoja na vigango vyao vingi Bagamoyo mjini na vijijini. 
Utume wa Padri Bayo na Shirika lake haukubakia tu kwenye usimamizi wa sakramenti bali ulijikita kwenye maeneo yote yanayohusiana na ukombozi wa mwanadamu, yaani elimu, afya na huduma nyingine za kijamii. 
Hadi leo hii, shule za Marian ni mojawapo ya shule zinazoongoza kwa ufaulu Tanzania. Vijana wengi wa Bagamoyo na mikoa mingine waliopitia kwenye shule za ufundi Marian wameweza kujipatia taaluma za ufundi na ajira katika fani mbalimbali zikiwemo useremala, ushonaji, uashi, ufundi vyuma, rangi, upishi na huduma za hoteli. Hakika elimu imekuwa njia kuu ya uijilishaji mpya Bagamoyo, kwani leo hii tunashuhudia uwepo wa Chuo kikuu kishiriki cha Marian Bagamoyo kinachojikita kwenye Elimu ya Sayansi.

CHANGAMOTO ZA UNJILISHAJI BAGAMOYO
Kanisa linapojiandaa kwa sherehe za miaka 150 ya uinjilishaji Bagamoyo na Tanzania kwa ujumla, linakiri kuwa changamoto bado ni nyingi. Kanisa la Bagamoyo linaonekana bado kama changa kwani sehemu zake nyingi hasa za vijijini bado ziko kwenye hadhi ya uinjilishaji wa kwanza. 
Hata hivyo, Bagamoyo ni wilaya inayokua kwa kasi, ukuaji unaochochea wahamiaji na wawekezaji wengi kuingia Bagamoyo. Ukuaji huu umeongoza hata Kanisa Katoliki la Tanzania kufikiria kuanzisha jimbo la Bagamoyo ifikapo mwaka 2018. Ukuaji huu unaashiria, bila shaka, mahitaji zaidi ya wachungaji na miundombinu ya Kanisa.
Miongoni mwa miundombinu itakayohitajika kwa jimbo jipya ni nyumba za malezi ikiwemo seminari. Hata hivyo itakumbukwa kuwa iliyokuwa seminari ndogo ya jimbo la Morogoro, St. Peters, na kuhamishiwa Morogoro mjini mwaka 1969, sasa inatumiwa na Wakala wa serikali wa Maendeleo na Uongozi wa Elimu ya Msingi Tanzania (Chuo cha ADEM). 
Inasemekana kuwa Kanisa lilikubaliana na Serikali kuwa seminari hiyo itumiwe na serikali kwa muda lakini kinachoonekana sasa ni kuwa, sio seminari tuu, ila hata eneo la Kanisa linaloizunguka linadaiwa kumilikiwa na ADEM. Jambo hili bado liko mahakamani likisubiri maamuzi licha ya ukweli kwamba linategemea zaidi msukumo kutoka jimboni Morogoro.

KUINGIA KWA WAMISIONARI WA AFRIKA TANZANIA
Miaka kumi baada ya wamisionari wa Shirika la Roho Mtakatifu kuingia Bagamoyo, walikuja wamisionari wengine wakiwemo Wabenediktini na Wamisionari wa Afrika (White Fathers). Hawa wote walikaa na wamisionari wa Shirika la Roho Mtakatifu kwa kipindi cha miezi mitatu wakijifunza juu ya mila na desturi za waafrika pamoja na kuzoea hali ya hewa ya Afrika Mashariki. 
Miongoni mwa hao wamisionari walikuwa Wamisionari wa Afrika (White Fathers) walioingia Bagamoyo mwaka 1878 wakitokea Algeria. Kulingana na mikakati ya uinjilishaji kipindi kile Wamisionari wa Afrika walitumwa kuelekea mikoa ya kati na kanda ya ziwa, jambo lililowapeleka hadi Tabora, Uganda na  Bukoba. 
Baadhi ya Wamisionari wa Afrika wa kwanza wamezikwa kwenye makaburi ya Kanisa Katoliki Bagamoyo na mwaka 2000 kundi la wamisionari hawa walirudi Bagamoyo na kusimika mnara wa kumbukumbu kwenye mlango wa makaburi hayo. Mnara huu ulikuwa ishara ya shukrani kwa Shirika la Roho Mtakatifu kwa ukarimu wao uliowawezesha kuzoea mazingira ya Tanzania Bara.
Tarehe 18 Novemba, 2017 Askofu Msaidizi wa jimbo la Bukoba, Mhashamu Methodius Kilaini, kama mwana historia alialikwa na Wamisionari wa Afrika kule Bagamoyo ili kuwapatia semina juu ya utume wao hapa Tanzania na Afrika kwa ujumla. 
Kwa siku nzima Askofu Kilaini alikuwa nao katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Stella Maris, Msalabani, Bagamoyo. Semina hiyo ni mojawapo ya matukio ya Shirika la White Fathers kuadhimisha miaka 150 tangu kuanzishwa kwake huko Algeria mnamo mwaka 1868 kwa lengo la kuinjilisha bara la Afrika.
Katika maadhisho ya Jubilei ya miaka 150 ya Uinjilishaji, tumeshuhudia maadhimisho mbalimbali ambayo ni matunda ya  Uinjilishaji huo.Hapo tarehe 27 Desemba, 2017 Jimbo la Bukoba limefanya sherehe kubwa parokiani Kashozi likisherehekea miaka 125 tangu kuhubiriwa Injili kwa mara ya kwanza hapo mwaka 1892. Tunawashukuru wamisionari wa Afrika kwani ndio walioleta Habari Njema ya Kristu jimboni Bukoba wakiwa wanatokea Uganda. Wamisionari hawa walijenga kanisa la kwanza huko Kashozi mwaka 1892 ambalo sehemu yake kubwa ilibomolewa na tetemeko la ardhi la Septemba 10, 2016. 
Tunda lingine la Uinjilishaji ni maadhimisho ya miaka 100 ya upadre Tanzania. Maadhimisho haya yalizinduliwa Rubya huko Bukoba tarehe 1 Oktoba 2016 na kufungwa kitaifa tarehe 15 Agosti 2017. Maadhimisho hayo hayo yamefanyika pia huko Rwanda na Jimboni Bunda huko Ukerewe. 
Ningependa kumalizia kwa kuonesha kumbukumbu moja muhimu ya wamisionari wa kwanza Bagamoyo inayofanana sana na makanisa ya kwanza huko Bukoba: “Miembe Misafa.” 
Miembe hii yenye umri ilioteshwa miaka ya 1870 pande zote mbili za barabara ya karibu urefu wa kilomita moja kuelekea Kanisa la Moyo Safi wa Bikira Maria. Miembe hii inatengeneza “nyarulembo” inayokutwa kwenye makanisa ya zamani huko Bukoba. 
Kwa wasiojua, “Nyarulembo” ni uwanja mkubwa mrefu wenye miti mikubwa kila upande huku na huku iliyooteshwa au kusimikwa kuelekea ikulu ya mfalme. Karibuni wote tuingie ikulu ya Mfalme wa milele kwa kuadhimisha jubilee hii ya miaka 150 ya uwepo wa “Mfalme” wetu huko Bagamoyo.  Kristu Mfalme wetu aendelee kututawala na kutuongoza daima.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU