Msalaba wa Jubilei Bagamoyo ni shule ya matumaini

MSALABA wa Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara unaozungushwa kwenye parokia tatu za Bagamoyo ni shule ya matumaini. Mwaka 2017 Askofu Telesphor Mkude Askofu wa Jimbo Katoliki la Morogoro alizindua Msalaba wa Jubilei ambao ulitakiwa kutembezwa katika parokia zote za Bagamoyo: Parokia ya Epifania, Parokia ya Moyo Safi wa Bikira Maria na Parokia ya Kristo Mfalme. 
Bado msalaba unatembezwa katika parokia hizi. Msalaba huu utukumbushe siku ya Ijumaa Kuu Yesu Kristo alipokufa msalabani na kuzikwa baadaye alifufuka. Ukweli huu unatupa matumaini: hakuna Jumapili ya Pasaka bila Ijumaa Kuu, hakuna taji la utukufu bila taji la miiba, baada ya dhiki faraja. 
Padre Raniero Cantalamessa, Mhubiri wa nyumba ya kipapa alisema siku ya Ijumaa Kuu tarehe 14 Aprili 2017 kuwa, “Msalaba ni tumaini la pekee duniani”. Msalaba wa Kristo ni ujumbe wa Mungu wa “I love You.”  “Mungu alituthibitishia upendo wake msalabani wakati Kristo aliponing’inia na kuvuja damu na kufa, ni Mungu alikuwa anaiambia dunia, ‘Nakupenda,” alisema mchungaji Billy Graham. Ukweli huu unatupa matumaini.
 Yesu akiwa msalabani aliambiwa maneno saba. Neno la tatu kwa Yesu msalabani lilitoka kwa mwizi ambaye katika mapokeo ya Kanisa Katoliki anaitwa Dismas au Demacus. Huyu alikuwa upande wa kulia wa Yesu. Neno lake lilikuwa ni sala. Aliomba mara moja maishani akapata. Alitafuta mara moja maishani akapata. Alibisha hodi mara moja maishani mlango ukafunguliwa. Lakini tukumbuke bahati ya mwenzako isikulaze mlango wazi. 
Dismasi alisema: “Unikumbuke Bwana katika ufalme wako.” Sala ya unikumbuke mimi, ni sala ya imani. Sala ya unikumbuke mimi, ni sala ya matumaini. Sala hiyo inafunua imani katika Kristo kama mfalme wa kweli. Yesu kweli anaweza kuokoa, hata kama hajiokoi mwenyewe – wala mhalifu kutoka msalabani.
Maneno ya mwizi Dismasi msalabani yalikuwa neno la imani, matumaini na upendo. Juu ya hili Baba wa Kanisa Gregori alikuwa na haya ya kusema: “Fadhila tatu ambazo mitume walizungumzia mwizi akiwa amejaa neema alizipokea na kuzitunza pale msalabani. Mfano alikuwa na imani kwa Mungu atatawala ambaye alimuona kufani kama yeye. Alikuwa na matumaini yeye ambaye aliomba kuingizwa katika ufalme Wake. Alitunza fadhila ya ukarimu kwa ari katika kifo chake, alimkosoa ndugu yake na mwenzi mwenzi ambaye alikuwa kufani kwa kosa kama lake.” 
Mwizi Dismasi alitumia vizuri talanta zake pale msalabani. Alitumia talanta ya mdomo. Mikono na miguu vilikuwa vimefungwa. Mwili wake ulikuwa umefungiwa msalabani. Ulimi wake ulikuwa uko huru. Aliutumia kusali. Aliutumia kumwonya mwizi mwenzake na kumshauri.  Alitumia ulimi wake kutubu. Moyo wa mwizi ulikuwa hukufungwa. Mwizi alitumia moyo kuamini matendo ya haki. Huu ni mtazamo wa Baba wa Kanisa Mtakatifu Gregori.  
Alikuwa na haya ya kusema: “Msalabani misumari ilifunga mikono yake na miguu yake hakuna sehemu ambayo ilibaki huru bila kuteswa isipokuwa moyo na ulimi wake. Kwa mwanga wa Mungu, mwizi alimtolea chochote kilichokuwa huru, kama ilivyoandikwa, kwa moyo ili aamini matendo ya haki, kwa mdomo ili atubu kwa ajili ya wokovu.” 
 Padri Raniero Cantalamessa, Mhubiri wa nyumba ya kipapa alisema haya juu ya mwizi mwema, “hakuna sababu msingi ya kumkatia Mungu matumaini kama ilivyokuwa kwa Kaini na badala yake, watu wawe na matumaini thabiti kama ilivyojionesha kwa yule Mwizi mwema, aliyetambua dhambi zake na kuomba msamaha, lakini Kaini aliona ukubwa wa dhambi akashindwa kuomba toba na msamaha. 
Msalaba duniani ni kielelezo cha mateso na mahangaiko yote ya binadamu na daima utaendelea kuwa ni sehemu ya historia ya maisha ya binadamu, kwani Mwenyezi Mungu alimtuma Mwanaye wa pekee ulimwengu si kwa ajili ya kuhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.” 
Mmoja wa wale wahalifu waliotundikwa alimtukana akisema, “Je, wewe si Kristo? Basi, jiokoe mwenyewe na sisi pia” (Luka 23: 39). Mateso ni mtazamo. Mateso msalabani yalimfanya mwizi mkono wa kushoto avunjike moyo, lakini yalimfanya mwizi mkono wa kulia avunje rekodi-mwizi aliyeiba mbingu. 
Watu wanaweza kuwa na mateso yaleyale, tofauti ni mtazamo walio nao juu ya mateso hayo. Askofu Fulton Sheen alikuwa na haya ya kusema: “Watu wanaweza kuwa katika mazingira yanayofanana na kutenda namna tofauti kabisa. Wezi wote walifanana katika walichokikosa moyoni na bado walimtendea tofauti mtu aliyekuwa katikati yao. Njia za nje, mfano mzuri kwa vyenyewe havitoshi kumbadilisha mtu, moyo usipobadilika.” 
Ni moyo unaompeleka mtu mbinguni. Ni moyo unaompeleka mtu motoni. Mwizi upande wa kushoto alikuwa na mtazamo hasi. Mwizi upande wa kulia alikuwa na mtazamo chanya. Mwizi upande wa kushoto alimuona Yesu mfanya mazingaombwe ambaye angempa ukombozi wa kimwili. “Wokovu tu ambao mwizi upande wa kushoto angeelewa haukuwa wa kiroho au kimaadili, bali kimwili: ‘Jiokoe na utuokoe sisi!’ 
Okoa nini? Roho zetu? Hapana! Mtu hana roho! Okoa miili yetu! Dini ina faida gani kama haiwezi kuondoa maumivu?” alisema Askofu Fulton Sheen. Kuna ambao wanaona dini kama Hospitali ya Rufaa. Isipotibu na kuponya magonjwa ya kimwili wanaiacha na kutafuta dini nyingine. Huu ni mtazamo. Binadamu ana roho na mwili.  Dini ni Hospitali ya wadhambi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU