‘Dhambi ya ubinafsi chanzo cha uharibifu wa mazingira’ Maaskofu




IMEELEZWA kuwa dhambi ya ubinafsi ni sababu kuu inayopelekea uchafuzi wa mazingira na kutishia uumbaji, hata kufikia hatua ya kutishia uhai wa mwanadamu kwa sababu ya kutafuta utajiri unaopindukia.
Hayo yamebainishwa  na Maaskofu Katoliki Tanzania katika ujumbe wa Kwaresima walioutoa hivi karibuni kwa waamini wote nchini, ukiwa na dhima isemayo ‘Furaha ya Injili na uumbaji’.
Wameeleza kuwa wanadamu wamepewa vyote na Mungu ili wavitunze, lakini pale wanapokuwa wakala wa uharibifu wa uumbaji, wanakuwa amesahau wajibu waliopewa wa kuilima na kuitunza nchi. Pia wametoa mwito kwa wanadamu kutumia kipindi hiki cha kwaresima kumrudia Mungu kutokana na kukosa utii wa kutunza mazingira.
“Tunashuhudia leo hii uharibifu mkubwa wa mazingira, mito inakauka, hewa inachafuliwa kutokana na shughuli za viwanda na motokaa, ardhi inachafuliwa kwa mifuko ya plastiki na taka ya sumu.. ukataji wa miti umepelekea mwanadamu kuumba jangwa na kusababisha mmomonyoko wa ardhi, uchimbaji wa madini unaacha athari kubwa za kimazingira na kudhuru afya ya mwanadamu. Mwanadamu anasahau kuwa kila kiumbe kina thamani kubwa mbele ya Mungu…” wameeleza.
Aidha wameweka wazi kuwa jamii inayopuuza mustakabali mwema wa mazingira na uumbaji, ni jamii isiyojijali yenyewe na isiyojali vizazi vijavyo. Wameonya kuwa ni hatari kubwa kupumbazwa na tama za kujitajirisha au uzembe wa kutojali ambao unapelekea kufanya uharibifu mkubwa kwa dunia iliyo makazi ya pamoja.
“Ubinafsi unapofusha macho ya dhamiri zetu na tunashindwa kulinda na kutetea mifumo ya kimazingira ambayo imeumbwa kwa ajili ya kututunza” wameongeza.
Pia Maaskofu wametahadharisha hali ya mwanadamu kujitafutia furaha kupitia vitu, starehe chafu, mali zisizo halali, na kusema kuwa hali hiyo siyo tu inatishia uumbaji, bali hupelekea mwanadamu kutishia uhai wake mwenyewe kwa sababu ya kutafuta utajiri unaopindukia.
“Kwaresima ni mwaliko wa kurudi na kuishi tena maisha ya kumpendeza Mungu. Ni mwaliko wa kufungua masikio ya mioyo yetu na kuisikiliza sauti ya Mungu, inayookoa na kututhibitishia furaha ya kweli” wamesema.


Na Pascal Mwanache, Dar es salaam

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU