Watoto walemavu na wazee waendelea kunyanyapaliwa

MOROGORO, Serikali imeshauriwa kusaidia kujenga vituo vya  afya katika vituo vya kulelea watoto wenye ulemavu mbalimbali kutokana na kunyanyapaliwa na baadhi ya wahudumu wa vituo  vya afya vya umma wanapokwenda  kupata huduma ya matibabu.
 Mkurugenzi wa Kituo cha Amani Centre kilichopo Mkoani Morogoro Padri Beatus Sewando, amebainisha hayo wakati akieleza changamoto mbalimbali zinazowakabili watoto wenye ulemavu hususani wanapoenda kupatiwa huduma za afya katika vituo vya afya.
 Padri Sewando amesema kuna baadhi ya wahudumu wa afya katika hospitali za umma ambao hutoa huduma mbaya kwa watoto wenye ulemavu hasa kutowasikiliza kwa wakati kiasi cha kusababisha vifo vya watoto hao.
 “Tunapokwenda kwenye hospitali za umma baadhi ya wahudumu wanawanyanyapaa mkishasema kwamba huyu ni mlemavu na wanapoona matendo anayoyatenda, huduma zinakuwa mbaya zaidi na inasababisha baadhi ya watoto kupoteza maisha, endapo wangepatiwa huduma kwa wakati wangepona,” amesema Padri Sewando.
 Aidha amefafanua kuwa watoto wenye ulemavu wanapofika katika hospitali hasa za umma hupokelewa tofauti na wale wasiokuwa na ulemavu, kiasi cha wasimamizi na walezi wa watoto hao kujisikia vibaya kwa mapokezi hayo na kuona wazi kuwa watoto hao wananyanyapaliwa.
 Pamoja  na hayo, Mkurugenzi huyo amesema kuwa kulingana na sera ya afya wazee na watu wenye ulemavu hupata matibabu bure, lakini imekuwa ni tofauti kwa watoto hao hali inayowalazimu baadhi ya watu wenye mapenzi mema kuwakatia baadhi ya watoto hao bima za afya.
 “Hili suala linapaswa kufuatiliwa na serikali yenyewe kama wametamka kitu waweke ufuatiliaji waone ile bure inafanyika kweli?, kwasababu malalamishi tunayasikia hata kwenye vyombo vya  habari hata kwa wazee ambao wanatakiwa watibiwe bure sijaona wazee wanaoridhika kiasi cha kuamini anapata huduma bure, akienda pale mzee ataandikiwa lakini dawa hamna hivyo kama serikali ina nia ya dhati kuwahudumia wazee na wenye ulemavu ifanye mpango kuwe na fungu na akiba maalumu ya dawa kwa ajili yao na kuwapa kipaumbele,” amesema Padri Sewando.
Hata hivyo amesema kuwa ana imani na serikali ya awamu ya tano kuwa itatekeleza na kusimamia vyema suala la huduma za afya kwa wazee na walemavu kwa sababu kwa muda mrefu imekuwa kinyume na utekelezaji wa sera husika.
 Wakati huohuo Padri Sewando amewaomba wahudumu wa afya kuwa na huruma na watoto walemavu na wazee kwa kuwajali na kuwapatia huduma sawasawa na wengine, kwani hawakupenda kuzaliwa walemavu na uzee haukwepeki na kuwapa huduma stahiki bila manung’uniko ni Baraka pia.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU